Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Ignas Aloyce Malocha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kwela

Primary Question

MHE. IGNAS A. MALOCHA aliuliza:- Je, ni lini Serikali itatoa fedha za kukamilisha ujenzi wa Kituo cha Afya kilichopo Kata ya Ilemba katika Halmashauri ya Sumbawanga?

Supplementary Question 1

MHE. IGNAS A. MALOCHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza kabisa, naipongeza Serikali kwa kutoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa hospitali za wilaya, vilevile upanuzi wa vituo vya afya, tunapongeza sana jitihada hizo za Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pamoja na majibu hayo ninayo maswali mawili ya nyongeza. Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga ni kweli imekuwa ikitenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya Ilemba lakini katika bajeti zake mfululizo imekuwa ikitenga fedha kwa maana ya kumalizia jengo hilo lakini mfululizo wa miaka karibu minne Serikali haijatoa fedha. Mheshimiwa Waziri atakubaliana na mimi kwamba eneo hilo lina mwingiliano mkubwa sana wa watu kutokana na biashara ya mpunga na samaki na kunakuwa na milipuko mingi ya magonjwa, wananchi wanakufa, wanapata taabu sana. Naomba Serikali sasa itambue kilio hicho iweze kutupatia fedha kumalizia kituo hicho cha afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na ujenzi wa Kituo cha Afya Ilemba, vipo vituo vingine vilishaanza kujengwa katika maeneo ya Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga, Vituo vya Afya vya Muze, Kaoze, Kiteta, Kalambanzite pia zahanati 12 na hii yote inatokana na sera ya kila kata kuwa na kituo cha afya na kila kijiji kuwa na zahanati, jambo ambalo Serikali yenyewe imepanga na tumewahamasisha wananchi. Ni nini kauli ya Serikali katika kukamilisha majengo haya?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ignas Aloyce Malocha, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla ya kujibu, naomba uniruhusu kipekee nimpongeze Mheshimiwa Malocha na wananchi wake wa Jimbo la Kwela kwa jinsi ambavyo wameitikia wito mkubwa wa kuhakikisha kwamba ujenzi unafanyika. Kipekee, naomba nimpongeze hata Mkuu wa Mkoa, nilimuona akishiriki yeye mwenyewe katika kuchimba msingi katika ujenzi wa hospitali ya wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya pongezi hizo, naomba niendelee kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge, kwanza tunathamini sana jitihada ambazo zinafanywa na yeye binafsi na wananchi wake. Kwa kadri bajeti ya Serikali
inavyoruhusu, maeneo yote ambayo ameyataja, pia hajataja Kituo cha Afya Mpui, naomba nimhakikishie, kwa kadri bajeti itakavyoruhusu hatuwezi tukaacha nguvu za wananchi zikapotea bure. Iko kwenye Ilani yetu ya CCM, tumeahidi, tutatekeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.

Name

Joram Ismael Hongoli

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lupembe

Primary Question

MHE. IGNAS A. MALOCHA aliuliza:- Je, ni lini Serikali itatoa fedha za kukamilisha ujenzi wa Kituo cha Afya kilichopo Kata ya Ilemba katika Halmashauri ya Sumbawanga?

Supplementary Question 2

MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Lupembe, Halmashauri ya Wilaya ya Njombe tuliomba fedha kwa ajili ya vituo vya afya hasa ikizingatiwa kwamba hatujapata hata kituo kimoja mpaka leo na tuliomba kwa ajili ya Kituo cha Afya Kichiwa ili kiweze kutoa huduma ya upasuaji lakini pia Kituo cha Afya cha Lupembe ambapo tumejenga huduma ya upasuaji kupitia mapato ya halmashauri na tumejenga jengo dogo la akina mama kupitia mchango wa Mbunge na wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wanataka kujua ni lini Serikali italeta hizo fedha kama zilivyopelekwa kwenye halmashauri nyingine na sisi Jimbo la Lupembe tuweze kupata angalau zile shilingi milioni 500 kwa ajili ya kuwa na vituo angalau viwili vitakavyotoka huduma ya upasuaji? Sasa hivi akina mama wanapata shida sana na wanatembea umbali mrefu kwa ajili ya kutafuta huduma hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli, katika maeneo ambayo hatukujenga kituo cha afya ni pamoja na Jimboni kwake Mheshimiwa kule Lupembe. Mheshimiwa hajataja kuwa miongoni mwa wilaya ambazo zinakwenda kujengewa hospitali za wilaya ni pamoja na wilayani kwake. Pia amewahi kupata fursa ya kuongea na Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana akamuahidi kwamba ikipatikana fursa ya kupata vituo hata viwili au kimoja, hatutasahau kituo chake. Naomba wananchi waendelee kuunga mkono Serikali, tumeahidi, tutatekeleza.

Name

Willy Qulwi Qambalo

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Karatu

Primary Question

MHE. IGNAS A. MALOCHA aliuliza:- Je, ni lini Serikali itatoa fedha za kukamilisha ujenzi wa Kituo cha Afya kilichopo Kata ya Ilemba katika Halmashauri ya Sumbawanga?

Supplementary Question 3

MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Wilaya ya Karatu ina zaidi ya umri wa miaka 20 na haina hospitali ya wilaya badala yake wananchi wamekuwa wakipata huduma hiyo katika vituo vya afya binafsi na hata vile vya chini. Tayari kama Halmashauri tumeshatenga eneo la kutosha la kujenga Hospitali ya Wilaya. Je, ni lini Serikali sasa itatenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa hospitali hiyo?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la kaka yangu, Mheshimiwa Mbunge wa Karatu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, licha ya ujenzi wa vile Vituo vya Afya 350 ambavyo tunaendelea navyo kama tunavyofahamu mpango wa Serikali katika mwaka huu wa fedha tunajenga hospitali mpya 67. Hata hivyo, mwaka huu wa fedha tena 2019/2020 bajeti tunayoenda nayo tutachukua maelekezo jinsi gani tufanye zile wilaya ambazo hazina hospitali za wilaya twende tukamalize tatizo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafahamu Mkoa wa Arusha tulielekeza nguvu kazi kule maeneo ya Ngorongoro na
Longido hata hivyo katika bajeti ya mwaka huu ambao tunaenda kuipanga, si muda mrefu Aprili, 2019 tuka-take consideration ya maeneo hayo. Lengo ni kwamba wananchi wote wapate huduma kama inavyokusudiwa.