Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Andrew John Chenge

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bariadi

Primary Question

MHE. ANDREW J. CHENGE (K.n.y. MHE. DKT. PUDENCIANA W. KIKWEMBE) aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kuleta baadhi ya sheria zilizopitwa na wakati Bungeni ili ziweze kupitiwa upya ziendane na wakati uliopo hasa zikiwemo Sheria za Usalama Barabarani?

Supplementary Question 1

MHE. ANDREW J. CHENGE: Mheshimiwa Spika, naishukuru sana Serikali kwa majibu yake. Nina maswali mawili ya nyongeza.
La kwanza, muuliza swali alilenga hasa katika Sheria ya Usalama Barabarani. Je, Serikali ina mpango gani wa kufanya marekebisho katika sheria hiyo?
Swali la pili; natambua kazi nzuri inayofanywa na Tume ya Kurekebisha Sheria; je, Serikali inaweza kwa wakati muafaka ikatoa report za kazi ambazo zimefanywa na Tume hiyo kama mapendekezo kwa Bunge lako tukufu? Ahsante. (Makofi)

Name

Anthony Peter Mavunde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Dodoma mjini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA NA VIJANA (MHE. ANTHONY P. MAVUNDE K.n.y. WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA): Mheshimiwa Spika, nikianza na swali la kwanza, ni kweli kwa mujibu wa sheria iliyoanzisha Tume ya Kurekebisha Sheria Sura Na. 171 iliyofanyiwa marejeo mwaka 2002, moja kati ya kazi ya Tume ni kuandaa report ambayo hupelekea mabadiliko ya sheria au kutungwa kwa sheria mpya.
Mheshimiwa Spika, katika Sheria za Usalama Barabarani tayari Tume imeshafanya kazi yake na tunayo report ya Tume ya mwaka 2004 ambayo imeshawasilishwa kwa Mheshimiwa Waziri. Pindi pale itakapoonekana kuna mahitaji ya kufanya marekebisho katika sheria husika, sharia hii itawasilishwa hapa Bungeni kwa ajili ya kuweza kufanyiwa marekebisho kama ambavyo Mheshimiwa muuliza swali amesema.
Mheshimiwa Spika, la pili, kuhusiana na report za Tume kuwasilishwa katika Bunge; kwa mujibu wa sheria Tume hii inapaswa kutoa taarifa yake ya kila mwaka ya namna ambavyo imezipitia sheria. Tunao mpango mkakati wa kuanzia mwaka 2013 mpaka mwaka 2018 wa marekebisho hayo ya sheria.
Mheshimiwa Spika, suala la uwasilishwaji wa taarifa hii, itakuwa ni kati ya Serikali na Bunge kuona namna bora ya kuwasilisha, lakini kwa hivi sasa taarifa zetu zinapatikana katika mitandao yetu mbalimbali na utaratibu mwingine wa Kiserikali kuhakikisha kwamba wananchi wengi wanazipata.
Mheshimiwa Spika, kwa maombi ya Mheshimiwa Mbunge, kama Serikali tumesikia na tutaona namna bora ya kuweza kulifanyia kazi jambo hilo.

Name

Magdalena Hamis Sakaya

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Kaliua

Primary Question

MHE. ANDREW J. CHENGE (K.n.y. MHE. DKT. PUDENCIANA W. KIKWEMBE) aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kuleta baadhi ya sheria zilizopitwa na wakati Bungeni ili ziweze kupitiwa upya ziendane na wakati uliopo hasa zikiwemo Sheria za Usalama Barabarani?

Supplementary Question 2

MHE. MAGDALENA H. SAKAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.
Mheshimiwa Spika, zipo sheria nyingine ambazo kuchelewa kuletwa Bungeni zina-cost maisha ya watu moja kwa moja. Kwa mfano, Sheria hii ya Usalama Barabarani, suala la sasa hivi Bodaboda ku-overtake kushoto linasababisha ajali nyingi sana na watu wengi wanapoteza maisha. Sheria inasema overtake kulia, lakini wewe una- overtake kushoto na ajali nyingi zinatokea kwa utaratibu huo.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa maisha ya watu yanapotea kila siku, Serikali haioni haja ya kuleta sheria hii kwa fast-track Bungeni ili kuokoa maisha ya watu wanaoteketea kila siku kwa sababu ya Sheria ya Barabarani kuwa imepitwa na wakati?

Name

Kangi Alphaxard Lugola

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mwibara

Answer

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kusimama ndani ya Bunge hili tukufu nikiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, nichukue fursa hii kuendelea kumshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuniamini kwamba ninatosha na ninaweza kumsaidia kazi hii ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi. Pia nakushukuru wewe kwa ushirikiano ambao unanipatia. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nampongeza Naibu Waziri, Mheshimiwa Mavunde namna ambavyo amejibu swali la msingi.
Mheshimiwa Spika, ni kweli kabisa katika kupambana na ajali za barabarani, na sisi tunajua kabisa bodaboda kama alivyosema Mheshimiwa Sakaya limekuwa ni tatizo kubwa. Tayari hivi tunavyozungumza, majibu mazuri kabisa ya Mheshimiwa Mavunde ni kwamba marekebisho ya Sheria ya Usalama Barabarani yako katika hatua za mwisho. Aiamini Serikali kwamba tutaileta hapa Bungeni kwa ajili ya Bunge hili kuweza kuipitisha. Ahsante. (Makofi)