Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Maftaha Abdallah Nachuma

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Mtwara Mjini

Primary Question

MHE. MAFTAHA A. NACHUMA aliuliza:- Je, kwa nini Serikali haisemi ukweli Bungeni juu ya fidia kwa wananchi wa Mtwara Mjini?

Supplementary Question 1

MHE. MAFTAHA A. NACHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza swali langu halijajibiwa. Niliuliza kwa nini Serikali haisemi ukweli ndani ya Bunge? Kwa sababu hapa nina Hansard mbili Serikali ikiahidi kulipa fidia wananchi hawa, lakini pia kuna maelezo ambayo siyo sahihi sana kwenye maelezo ya Mheshimiwa Naibu Waziri. Hata hivyo nina maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, Serikali hii ya Awamu ya Tano inafanya mambo makubwa sana, imeweza kununua ndege, imeweza kuwa na mkakati wa kujenga standard gauge, lakini pia imeweza kuweka mkakati wa kujenga Stiegler’s Gorge, inashindwaje kulipa fidia ya shilingi bilioni nane kwa wananchi wa Jimbo la Mtwara Mjini maeneo ya Mjimwema? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, naomba kujua, katika kuilazimisha Halmashauri sasa kuwaeleza wananchi waweze kupimiwa viwanja, wapo wananchi waliokubali na wengine hawajakubali. Je, kwa kuwa hili suala la Taasisi ya UTT-PID ipo ya chini ya Serikali Kuu, Serikali iko tayari hivi sasa kuja Mtwara Mjini na kuweza kutoa elimu kwa wananchi hao wa Mjimwema na Tangira ili waweze kukubaliana na maamuzi ya Serikali? Ahsante.

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa kutokana na swali lake jinsi alivyouliza, majibu ya Serikali ni sahihi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, alitaka kujua kwa nini Serikali haisemi ukweli Bungeni juu ya fidia ya wananchi wa Mtwara? Na sisi tumeongelea habari ya fidia aliyoitaka ya UTT. Mpaka sasa hivi anavyozungumza UTT haidaiwi kulipa fidia yoyote kwa wananchi wale kwa sababu tayari Manispaa imeshachukua mradi ule na zoezi limeshaanza na wananchi wanapimiwa na kuna makubaliano ambayo wameingia kati ya wananchi na Manispaa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kule hakuna anayedai fidia, kwa maana hiyo, kwa sababu tayari baada ya UTT kujitoa wananchi kupitia Halmashauri yao wameamua kuchukua eneo lile na kuanza kupimiwa na viwanja wanapewa kama sheria inavyosema. Kwa hiyo, Serikali imejibu kulingana na swali lake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili analotaka habari ya kutoa elimu, sisi tuko tayari wakati wowote tunatoa elimu, tuna vipindi mbalimbali na hata wakitaka twende kule tutakwenda kwa sababu ndiyo kazi yetu kuelimisha wananchi ili waweze kuelewa haki zao za msingi na waweze kufanya mambo yao pasipo kubughudhiwa.