Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 12 Sitting 3 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 38 2018-09-06

Name

Maftaha Abdallah Nachuma

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Mtwara Mjini

Primary Question

MHE. MAFTAHA A. NACHUMA aliuliza:-
Je, kwa nini Serikali haisemi ukweli Bungeni juu ya fidia kwa wananchi wa Mtwara Mjini?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maftaha Abdallah Nachuma, Mbunge wa Mtwara Mjini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, mgogoro mkubwa wa fidia uliopo sasa katika Manispaa ya Mtwara Mikindani unahusu eneo la Mjimwema na Tangira unaotokana na upimaji wa viwanja 10,000 uliotarajiwa kufanywa kwa njia ya ubia baina ya Manispaa ya Mtwara Mikindani, pamoja na Taasisi ya UTT- PID mwaka 2003. Upimaji huu haukufanyika kama ilivyopangwa kutokana na amri ya kusitishwa kwa miradi yote ya upimaji wa viwanja ambavyo Halmashauri mbalimbali zilikuwa zikishirikiana na UTT-PID iliyotolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu, TAMISEMI mwaka 2004.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na katazo hilo, Manispaa ya Mtwara Mikindani iliendelea kuomba kibali cha kuendelea na mradi huo, kwa kuwa shughuli mbalimbali tayari zilikuwa zimeshafanyika zikiwemo uthamini kwa ajili ya fidia. Baada ya ufuatiliaji, Ofisi ya Rais, TAMISEMI ilitoa kibali cha kuendelea na mradi huo kwa barua yenye Kumb. Na. GB.2013/234/01/117 ya tarehe 2/09/2016.
Hata hivyo mwishoni wa mwaka 2017 Taasisi ya UTT- PID ilikiri kutoweza kuendelea na mradi huo kutokana na ukosefu wa fedha uliosababishwa na taratibu za utekelezaji wa mradi huo kuchukua muda mrefu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwezi Januari, 2018 Baraza la Halmashauri ya Manispaa ya Mtwara Mikindani liliamua kuendelea na mradi huo kwa kuwapimia wananchi maeneo yao na kisha kuwapa viwanja kulingana na ukubwa wa maeneo yao na hatimaye kuwamilikisha kisheria badala ya kusubiri fidia ambayo kimsingi haipo. Jumla ya shilingi milioni 170 zilitengwa katika bajeti ya Halmashauri kwa ajili ya kugharamia zoezi la upimaji na ufunguzi wa barabara za msingi katika eneo la mradi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa eneo la Tangira katika Kata ya Mitengo waliridhia kuendelea na utaratibu wa kupimiwa viwaja katika mashamba yao. Mpaka sasa jumla ya viwanja 1,212 vimepimwa. Aidha, jumla ya viwanja 2,800 vinatarajiwa kupimwa katika eneo la Mjimwema Kata ya Magengeni. Kwa maeneo mengine upimaji wa viwanja utaendelea baada ya kukamilika kwa majadiliano baina ya Serikali na wananchi ambao ni wamiliki wa asili wa mashamba husika.