Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Dr. Raphael Masunga Chegeni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Busega

Primary Question

MHE. DKT. RAPHAEL M. CHEGENI aliuliza:- Vijiji vya Nyakaboja, Kabita, Chumve, Kalemela, Kalago, Badugu na Nyaluhande vimepitiwa na nguzo na nyaya za umeme, lakini wananchi hao hawana huduma ya umeme:- Je, ni lini Serikali itawapatia umeme wananchi wa maeneo hayo ili wasiendelee kuwa walinzi wa nguzo za TANESCO?

Supplementary Question 1

MHE. DKT. RAPHAEL M. CHEGENI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii. Kwanza napenda nipongeze majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri pamoja na kazi inayofanywa na Wizara hii ya Nishati katika kuwapatia umeme Watanzania. Hata hivyo, nina maswali madogo mawili:
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; pamoja na jitihada hizi kuna vijiji 10 vimesahaulika, Vijiji hivi ni kama Mwamigongwa, Rwangwe, Ilumya, Igabulilo, Mwamalole, Mwabayanda, tayari tulishaongea na Wizara kwamba kuna vijiji ambavyo katika mzunguko huu vimerudiwa kutajwa majina tena, tukasema wafanye substitution; Je, Wizara inalifanyaje suala hili ili kusudi vijiji hivi ambavyo vimerudiwa visirudiwe tena na ambavyo havina umeme viweze kupatiwa umeme? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa umeme unasambazwa na moja ya agizo ni kwamba Taasisi za Serikali ziweze kupata umeme huu ikiwemo zahanati, shule na kadhalika na kuna baadhi ya maeneo ambayo umeme hu unasambazwa kwa mitaa michache. Je, nini kauli ya Serikali kuhakikisha kwamba umeme unasambazwa kulingana na mahitaji ya watumiaji? (Makofi)

Name

Subira Khamis Mgalu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa. Kwanza nimpongeze sana kwa kazi nzuri ya kufuatilia miradi ya nishati katika Jimbo lake, lakini la pili amevitaja vijiji kumi ambavyo kwa maelezo yake vimesahaulika na ameunganisha hapo na vijiji ambavyo vimetajwa kwenye REA Awamu ya Tatu mzunguko wa kwanza ambapo inaonekana vina miundombinu ya umeme.
Mheshimiwa Spika, msimamo wetu wa Wizara ni kwamba vijiji vyote vyenye miundombinu ya umeme ambavyo vipo kwenye Awamu ya Tatu mzunguko wa kwanza vifanyiwe marekebisho na vijiji ambavyo havina miundombinu ya umeme. Kwa kuwa, amevitaja vijiji vyake kumi na kwa kuwa ameshafanya mawasiliano na Wizara na REA kwamba nia ya mradi huu wa Awamu ya Tatu ni kupeleka umeme kwenye maeneo ambayo hakuna miundombinu. Kwa hiyo, nataka niwaelekeze REA kwamba wafanye substitution kwa sababu ni jambo la kawaida na tumekuwa tukifanya katika maeneo mengine.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili, ametaka tamko la Serikali juu ya maeneo ya Taasisi za Umma, ni kweli tumetoa tamko, tulitazama upungufu wa REA awamu zilizopita kwamba Taasisi nyingi za umma ikiwemo miradi ya maji, ikiwemo zahanati, vituo vya afya zilirukwa. Kwa hiyo, mradi wa REA Awamu ya Tatu tuliona tusirejee changamoto za REA awamu zilizopita.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naendelea kusisitiza agizo la Wizara na Serikali kwamba maeneo ya Taasisi za Umma yapatiwe vipaumbele katika kupeleka miundombinu ya umeme. Naomba nimthibitishie Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo hili la Busega na maeneo yote kwamba hilo ndiyo tamko la Serikali ya Awamu ya Tano. Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)