Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 11 Sitting 16 Energy and Minerals Wizara ya Nishati 133 2018-04-24

Name

Dr. Raphael Masunga Chegeni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Busega

Primary Question

MHE. DKT. RAPHAEL M. CHEGENI aliuliza:-
Vijiji vya Nyakaboja, Kabita, Chumve, Kalemela, Kalago, Badugu na Nyaluhande vimepitiwa na nguzo na nyaya za umeme, lakini wananchi hao hawana huduma ya umeme:-
Je, ni lini Serikali itawapatia umeme wananchi wa maeneo hayo ili wasiendelee kuwa walinzi wa nguzo za TANESCO?

Name

Subira Khamis Mgalu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Raphael Masunga Chegeni, Mbunge wa Busega, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Busega ina Vijiji 59, kati ya vijiji hivyo vijiji 18 vimepatiwa umeme kupitia miradi ya Electricity V na REA Awamu ya II. Kijiji cha Kalemela kilipatiwa umeme kupitia REA Awamu ya Kwanza. Kijiji cha Badugu kimepatiwa umeme kupitia mradi wa Electricity V na baadhi ya maeneo ya Kijiji cha Nyaluhande vimepitiwa umeme kupitia mradi wa REA Awamu ya Pili.
Mheshimiwa Spika, Vijiji vya Kabita, Nyakaboja na Kalago vitapatiwa umeme kupitia mradi wa REA Awamu ya Tatu mzunguko wa kwanza ambao utekelezaji wake umekwishaanza kupitia Mkandarasi White City Guangdong JV Limited. Kazi za mradi wa kupeleka umeme katika Wilaya ya Busega zinajumuisha ujenzi wa kilometa 49.7 za njia ya umeme, msongo wa kilovoti 33, kilometa 116 za njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 0.4, ufungaji wa transforma 58 na kuunganisha wateja wa awali 1,783. Gharama za mradi ni shilingi bilioni 5.5. Mradi unatarajiwa kukamilika Julai, 2019.
Mheshimiwa Spika, Kijiji cha Chumve pamoja na vijiji vingine vilivyobaki vitapatiwa umeme kupitia mradi wa REA Awamu ya Tatu mzunguko wa pili unaotarajiwa kuanza mwezi Julai, 2019 na kukamilika mwezi Juni, 2021. Mheshimiwa Spika, ahsante.