Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Kiswaga Boniventura Destery

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Magu

Primary Question

MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA aliuliza:- Serikali ilitenga eneo la Sayaka Salama Bugatu kuwa hifadhi ya msitu, lakini msitu wenyewe haukui huku wananchi, wafugaji na wakulima wakikosa maeneo ya mifugo yao na kilimo. Je, Serikali ina mpango gani wa kuwarudishia wananchi maeneo hayo ili waweze kuyatumia kwa kilimo na mifugo.

Supplementary Question 1

MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza msitu unaozungumzwa haupo, hata athari zinazozungumzwa kwamba vijiji vinavyozunguka watapata athari ya upepo siyo kweli, kwa sababu hata wewe ukisimama mle mita mia tatu unaonekana huo ni msitu?
(a) Je, Serikali kwa sababu inasema ni chujio haioni kwamba sasa ni wakati muafaka wa kulipunguza eneo hilo ikawapa wananchi upande mwingine, na upande mwingine ili wakaendelea na shughuli za kijamii na eneo linalobaki wakaliboresha kwa kupanda wenyewe misitu endelevu.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu majibu haya ni ya kudanganywa, je, Naibu Waziri yupo tayari kuambatana nami kwenda kuliona eneo ambalo linasemwa ni hifadhi?

Name

Eng. Ramo Matala Makani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la kwanza, nataka hapa kwa ufupi kabisa tuelewane kwamba, dhana hii ni kwa Watanzania wote kwa nchi nzima. Dhana ya kwamba changamoto za mahitaji ya ardhi kwa ajili ya matumizi mengine ya kibinadamu zitamalizwa kwa kuendelea kumega au kwa kuchukua maeneo yaliyohifadhiwa ni dhana ambayo siyo ya maslahi kwa Taifa hili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tukiendelea kufikiria kwamba ardhi iliyohifadhiwa ambayo ipo hivyo ilivyo leo kwa sababu imehifadhiwa kwa muda wote ambao imehifadhiwa, dhana hiyo itatufikisha mahali ambapo uhifadhi huo utapotea na ukipotea athari zake ni pana na kubwa na zinatugusa wote nchi nzima.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli inawezekana ukifika katika msitu huo huoni miti juu, lakini msitu unahifadhiwa kwa ajili ya tafsiri ya misitu ya miti unayoiona ipo juu, lakini pia ni kwa sifa za ardhi pale chini, ndiyo maana tumesema chujio, unaweza usione miti lakini, viumbe vilivyopo pale chini kwenye udongo sifa za ardhi ile iliyopo pale na yenyewe pia ni sehemu ya uhifadhi na ni muhimu.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika sehemu ya pili ya swali lake, kwanza siyo kweli kwamba majibu ni ya kudanganywa, lakini hakuna mwisho wa kufanya vizuri, kila unapodhani umefanya vizuri bado kuna kufanya vizuri zaidi. Nipo tayari kuambatana naye kwenda kuboresha uelewa nilionao tayari, kwenda kupata majibu ya pamoja mimi naye wakati tutakapoweza kupanga wote kwa pamoja, ili tuweze kupata hayo majibu sahihi na kuweza kutatua matatizo haya kwa maslahi ya Taifa letu.