Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Edward Franz Mwalongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Primary Question

MHE. EDWARD F. MWALONGO aliuliza:- • Je, Serikali inatumia pesa kiasi gani kuhudumia mfungwa mmoja kwa siku kwa huduma ya chakula tu? • Vitendo kama kulala chini, kulala bila blanketi au shuka, kulala bila neti vimekuwa vya kawaida kabisa katika Magereza yetu nchini; je, hii nayo ni sehemu ya adhabu ambayo wafungwa wanapewa kwa mujibu wa sheria?

Supplementary Question 1

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Naibu Waziri amejibu kipengele kimoja tu cha swali na kipengele kinachofuata hajakisoma. Kwa kuwa nimepewa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza nafikiri atakisoma atakaporudi kwenye jukwaa.
Mheshimiwa Spika, Gereza la Njombe lina msongamano mkubwa sana na katika msongamano huu wako akina mama wenye watoto wadogo mle ndani ya Gereza.
Je, Serikali sasa iko tayari kuwapa chakula maalum watoto wale ili kutokuwaathiri makuzi yao na kuwafanya wakue wakiwa na afya bora? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, swali la pili, katika Gereza la Njombe, yuko Mahabusu anaitwa Erick Mgoba. Mahabusu huyu amepelewa Hospitali ya Rufaa kwa kushirikiana na Gereza la Njombe ili apatiwe matibabu. Alivyofika Hospitali ya Rufaa Mbeya akatakiwa kulipa shilingi 300,000 ili atibiwe na akarudishwa Njombe bila kutibiwa na afya yake ni mbaya.
Je, Serikali iko tayari kumtibu mahabusu huyu ili kuokoa maisha yake? (Makofi)

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI MAMBO YA NDANI YA NCHI:
Mheshimiwa Spika, kwanza nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba mbali ya upungufu wa fedha ambazo tunatumia kwa kumlisha chakula mfungwa, ambayo nimezungumza katika jibu langu la msingi kwamba ni shilingi 1,342; lakini tunahakikisha kwamba chakula ambacho anakula mfungwa ni chakula chenye kiwango cha kutosha. Tunapima hivyo kulingana na calories ambayo nadhani ni 2,200 na kitu kwa kila mfungwa; 2,200 kwa mfungwa mwanaume na 2,500 kwa wafungwa wanawake.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, suala la watoto na wafungwa wa kike na wa kiume kwa ujumla, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba wanapata chakula chenye ubora na chenye kiwango cha kuridhisha, juu ya upungufu wa fedha, lakini kiwango tunahakikisha kwamba kinakuwa kwa maana ya lishe, inakuwa ni lishe ambayo iko sawa kabisa kitabibu.
Mheshimiwa Spika, la pili, kuhusiana na matibabu ya mfungwa ambaye amemzungumza amesema kama tuko tayari, naomba baada ya Bunge hili mimi na yeye tukutane tuone jinsi gani tunalishughulikia hili jambo. Ni lazima tuhakikishe kwamba mfungwa huyu anapata matibabu. (Makofi)

Name

Rev. Peter Simon Msigwa

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Iringa Mjini

Primary Question

MHE. EDWARD F. MWALONGO aliuliza:- • Je, Serikali inatumia pesa kiasi gani kuhudumia mfungwa mmoja kwa siku kwa huduma ya chakula tu? • Vitendo kama kulala chini, kulala bila blanketi au shuka, kulala bila neti vimekuwa vya kawaida kabisa katika Magereza yetu nchini; je, hii nayo ni sehemu ya adhabu ambayo wafungwa wanapewa kwa mujibu wa sheria?

Supplementary Question 2

MHE. MCH. PETER S. MSIGWA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Na mimi nikupongeze kwa kurudi salama, tuliku- miss pia.
Mheshimiwa Spika, elimu ya kisasa ya sheria sasa hivi ina-encourage kupunguza misongamano kwenye Magereza, wanapokwenda kwenye Mahakama wahakikishe wanapunguza misongamano na kuwapeleka watu Magerezani bila sababu.
Mheshimiwa Spika, kama swali la msingi ambavyo limeulizwa ukienda kwenye Magereza yetu, kuna msongamano mkubwa sana. Kwa mfano, Gereza la Segerea ambalo nili-happen kulitembelea juzi, capacity yake ni mahabusu 700, lakini sasa hivi lina mahabusu na wafungwa 2,400. Wanalazimika watu kulala upande mmoja mmoja kwa zamu baada ya muda tena inapigwa alarm, halafu wageukie upande mwingine. Huu ni ukiukwaji kabisa wa haki za binadamu. Kuna watoto wengi ambao wako under age wamekaa pale, wengine wanatakiwa waende shuleni. Hii tuna-cripple Taifa la baadae, wala hatuwasaidii wale watoto ambao wako Magerezani. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, sasa swali langu; kwa kuwa hii modern law inafundisha kupunguza mahabusu kwa kadri iwezekanavyo wasiende Magerezani; ni kwa nini Serikali imekuwa ikipeleka wanasheria kutetea kesi za Serikali ambao wamekuwa wakilazimisha wale ambao wanaweza wakapata bail waende kukaa mahabusu, kama ambavyo kesi zetu sisi zilikuwa zina bail, lakini Mawakili wa Serikali wakawa wanalazimisha twende kule tukaongeze msongamano?

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Spika, mahabusu kuwekwa ndani kwa muda mrefu siyo suala tu la kwamba Serikali haitaki kesi ziishe mapema, lakini kuna sababu nyingi za msingi za baadhi ya watuhumiwa kutoachiwa.
Mheshimiwa Spika, moja, mara nyingine ni kwa sababu ya usalama wao. Kwa mfano, kama ni watu ambao wametenda makosa ambao unahisi kwamba wakienda nje wanaweza wakapata matatizo, mara nyingi Serikali inajaribu kuwalinda. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ya pili, kuna watuhumiwa ambao wakitoka nje wanaweza vilevile kwenda kuharibu ushahidi. Kwa hiyo, Serikali inaangalia hivyo vitu vyote. Siyo suala la kwamba hutaki kesi iishe, lakini yawezekana unapowaachia kurudi, wanaenda kusababisha kesi ichelewe kwa sababu wataharibu ushahidi. Nashukuru sana. (Makofi)

Name

Esther Nicholus Matiko

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. EDWARD F. MWALONGO aliuliza:- • Je, Serikali inatumia pesa kiasi gani kuhudumia mfungwa mmoja kwa siku kwa huduma ya chakula tu? • Vitendo kama kulala chini, kulala bila blanketi au shuka, kulala bila neti vimekuwa vya kawaida kabisa katika Magereza yetu nchini; je, hii nayo ni sehemu ya adhabu ambayo wafungwa wanapewa kwa mujibu wa sheria?

Supplementary Question 3

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Ni kweli kabisa kwamba msongamano kwenye Magereza yetu Tanzania, Tarime na hata Segerea nilipoenda ni mkubwa sana.
Mheshimiwa Spika, swali langu la nyongeza ambalo nauliza hapa, Mheshimiwa Waziri wakati anatoa takwimu za gharama kwa wafungwa, amesema ni shilingi 1,200 kwa chakula. Nilipokuwa Segerea kwenye swali langu ninaloenda kuuliza, kule kuna wamama wamefungwa wanadaiwa shilingi 150,000 mathalani, lakini amefungwa miezi sita. Kwa gharama ambazo amezitoa Mheshimiwa Naibu Waziri unakuta zinavuka pale tena mpaka shilingi 270,000. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kuna mama ambaye amefungwa miezi sita, anaumwa ugonjwa wa fibroid ana-over breed, kila siku jioni ambulance inampeleka Amana.
Je, ni kwa nini Serikali isitumie busara ya zaidi kwa hawa akina mama ambao wengine wana watoto wachanga ambao unakuta wanafungwa kwa kesi za shilingi 100,000 au 200,000 wasiweze kuzi-waive uki-compare na gharama ambazo wanaenda kuhudumia kwenye ile jamii? Ahsante sana. (Makofi)

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Spika, suala la kwamba fedha ambayo wanadaiwa ni kidogo, ni suala la kisheria. Kwa hiyo, kama Mheshimiwa Mbunge anafikiri sheria ile imepitwa na wakati na haitendi haki, ni rahisi yeye kuleta hoja Bunge hili libadilishe sheria kwa sababu sheria ndiyo zinasema hivyo. (Makofi)

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, nipongeze kwa majibu mazuri yaliyotolewa. Nataka tu kumuomba Mheshimiwa Mwalongo kwa ile hoja ya jambo mahususi alilolileta kwamba baada ya Bunge, basi tuonane ili nilipate vizuri kwa sababu jambo lake alilolileta lile ni mahususi ili tuweze kulifanyia kazi.
Mheshimiwa Spika, hoja nyingine ambazo tumezipata, niweke tu kumbukumbu sawa, siyo kila Magereza yana msongamano. Tuna baadhi ya Magereza ambako katika mikoa ile kiwango cha uhalifu ni kidogo, hata msongamano Magerezani ni mdogo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nilienda Mkoa wa Lindi, Gereza lilikuwa na uwezo mkubwa kuliko kiwango cha wahalifu. Hivyo hivyo, nilienda kwa Mheshimiwa Shangazi kule, kiwango cha Gereza la kule ni kikubwa kuliko wahalifu walioko mle.
Kwa hiyo, nitoe rai kwa Watanzania na jamii nzima ya Watanzania kuepuka kufanya uhalifu kwa kweli, kwa sababu sisi kama Serikali hatupendi watu kuwa magerezani, lakini tunawapeleka kwa sababu ya uhalifu wanaoufanya.
Mheshimiwa Spika, hatuwezi tukaacha wahalifu wakawa nje na kama watu watafanya uhalifu, ni kwamba wataenda magerezani. (Makofi)