Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Primary Question

MHE. JAPHET N. HASUNGA aliuliza:- Mwaka 2002 Serikali ilipitisha Sheria ya Utumishi wa Umma ya mwaka 2002 na Marekebisho yake ya mwaka 2008 yaliweka Mfumo wa Wazi wa Upimaji na Ujazaji wa Mkataba wa Utendaji Kazi (OPRAS):- (a) Je, ni kwa kiasi gani mfumo huu umetekelezwa nchini? (b) Ni lini mfumo wa kupima taasisi (institutional performance) utaanzishwa na kuanza kutangazwa hadharani?

Supplementary Question 1

MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri naomba niulize maswali mawili ya nyongeza:-
Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kwa kuwa imeonekana taasisi nyingi hazifuati mfumo huu wakati Sheria ya Utumishi wa Umma ya mwaka 2008 iliweka ni lazima kwa kila mtumishi kujaza hizo fomu na kutekeleza mfumo huu. Je, ni hatua gani ambazo Serikali imekusudia kuchukua kwa taasisi na watumishi ambao hawafuati huu mfumo ambao ni wa lazima kwa mujibu wa sheria?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa kutangaza hadharani taasisi ambazo zimefanya vizuri katika kutekeleza mfumo huu kungesaidia sana kuwapa motisha wafanyakazi wanaofanya kazi katika taasisi hizo. Je, Mheshimiwa Waziri atakubaliana nami kwamba umefika wakati sasa taasisi zinazofanya vizuri na zile ambazo zinafanya vibaya zitangazwe moja kwa moja hadharani?

Name

Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAMISEMI, UTUMISHI NA UTAWALA BORA (MHE. ANGELLAH J. KAIRUKI): Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwanza, kuhusiana na hatua gani ambazo Serikali inakusudia kuchukua kwa watumishi ambao hawazingatii mfumo huu, nipende tu kumwambia kwamba, kuanzia mwaka 2012, Katibu Mkuu Utumishi alitoa Waraka na ilielekeza kwamba kuanzia kipindi hicho hakuna mtumishi wa umma atakayepandishwa cheo endapo hajaweza kujaza fomu ya OPRAS. Vile vile tunakusudia kuweka tozo maalum kama adhabu kwa ajili ya watumishi ambao hawatazingatia sharti hili.
Mheshimiwa Spika, katika swali la pili alitaka kufahamu endapo Serikali iko tayari kutangaza hadharani taasisi zinazofanya vizuri. Nipende tu kusema kwamba, tunafikiria pia kuweka tuzo, lakini tunapokea ushauri na tutaangalia ni kwa namna gani suala hili linaweza kutekelezwa kwa kutangaza hadharani.