Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 3 Public Service Management Ofisi ya Rais TAMISEMI. 25 2016-04-21

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Primary Question

MHE. JAPHET N. HASUNGA aliuliza:-
Mwaka 2002 Serikali ilipitisha Sheria ya Utumishi wa Umma ya mwaka 2002 na Marekebisho yake ya mwaka 2008 yaliweka Mfumo wa Wazi wa Upimaji na Ujazaji wa Mkataba wa Utendaji Kazi (OPRAS):-
(a) Je, ni kwa kiasi gani mfumo huu umetekelezwa nchini?
(b) Ni lini mfumo wa kupima taasisi (institutional performance) utaanzishwa na kuanza kutangazwa hadharani?

Name

Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAMISEMI, UTUMISHI NA UTAWALA BORA (MHE. ANGELLAH J. KAIRUKI) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Japhet Ngailonga Hasunga, Mbunge wa Vwawa, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, mfumo wa kupima utendaji kazi kwa uwazi ulianzishwa mwezi Julai, 2004 ikiwa ni sehemu ya mikakati ya kutekeleza Sera ya Menejimenti na Ajira katika Utumishi wa Umma ya mwaka 1998 kama ilivyohuishwa mwaka 2008 pamoja na Sheria ya Utumishi wa Umma, Sura 298.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2012/2013, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma kwa kushirikiana na Tume ya Utumishi wa Umma ilifanya Tathmini ya Uzingatiaji na Utekelezaji wa Mfumo wa OPRAS katika taasisi za umma. Tathmini hiyo ilihusisha taasisi za umma 110 katika kipindi cha awamu tatu. Katika tathmini hiyo, lengo lilikuwa ni kufuatilia taasisi zilizokuwa na utekelezaji wa kiwango cha juu. Napenda tu kuliarifu Bunge lako kwamba matokeo ya tathmini hiyo yalionesha kwamba utekelezaji uko katika asilimia 51.
Mheshimiwa Spika, hatua zilizochukuliwa ili kuhakikisha kwamba mfumo huu unatekelezwa na watumishi wote, Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora iliagiza waajiri kuhakikisha kwamba mtumishi atapandishwa cheo tu kwa kuzingatia matokeo ya OPRAS. Hatua hii imesaidia sana kuongeza kiwango cha utekelezaji kwani sasa kila mtumishi anatekeleza mfumo huu kama sharti la kupandishwa cheo.
Mheshimiwa Spika, kuhusu lini Serikali itaanzisha na kutangaza mfumo wa kupima taasisi (institutional performance) hadharani, napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba Serikali inatarajia kuanza utekelezaji wa Mikataba ya Utendaji kazi katika mwaka wa fedha 2016/2017. Mikataba hii itatekelezwa na taasisi zote za umma ikiwa ni pamoja na Wizara, Idara Zinazojitegemea, Wakala za Serikali, Sekretarieti za Mikoa, Mamlaka za Serikali za Mitaa, Mashirika ya Umma na Taasisi nyingine za umma. Mfumo huu utaiwezesha Serikali kupima utendaji kazi kwa kila taasisi ya umma kwa kila mwaka.