Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Ritta Enespher Kabati

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. RITTA E. KABATI aliuliza:- Zao la mbao linachangia pato la Taifa katika nchi yetu na zao hili linazalishwa kwa wingi katika Wilaya ya Mufindi katika Mkoa wa Iringa:- Je, zao hili linaingiza fedha kiasi gani kwa mwaka.

Supplementary Question 1

MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize nafasi niulize maswali madogo mawili ya nyongeza na nimshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake. Pamoja na Serikali kukiri kuwa zao la mbao linachangia pato la Taifa kwa kiasi kikubwa nchini, lakini barabara zinazoingia katika maeneo ya misitu ni mbovu sana na hazipitiki hasa wakati wa mvua. Je, Serikali ina mpango gani wa kuweka lami katika maeneo hayo ambako mbao hizo zinavunwa? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa serikali imekuwa ikimuuzia mwekezaji wa nje (MPM Mgololo) nusu bei ya magogo, je, iko tayari sasa kuwauzia wajasiliamali wetu bei sawa na hiyo ili kuitikia wito wa uchumi wa viwanda. (Makofi)

Name

Eng. Ramo Matala Makani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Ritta kwanza kwa kuonesha nia na dhamira ya kuunga mkono jitihada za Serikali katika kuendeleza viwanda nchini na hasa viwanda vinavyopata malighafi yake kupitia misitu; lakini pia nijibu maswali yake ya nyongeza mawili kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la kwanza la uboreshaji wa miundombinu ya barabara. Kwanza ni jambo ambalo hata upande wa Serikali ni la interest, kwamba maeneo ya mashamba yaweze kupitika kirahisi kwa ajili ya kuweza kuyahudumia mashamba yenyewe. Hata hivyo kuhusiana na suala la barabara zainazokwenda kwenye mashamba yenyewe ambazo zipo kimsingi chini ya Halmashauri ya Wilaya, barabara za makundi haya mawili zinashughulikiwa kwa namna tofauti.
Mheshimiwa Naibu Spika, hizi barabara ambazo zipo chini ya Halmashauri; katika Halmashauri ambazo zina mashamba Serikali inachokifanya ni kuweza kuchangia nguvu na uwezo wa kuweza kuhudumia barabara hizo kupitia uazimishaji wa mitambo mbalimbali ya ujenzi wa barabara. Mahali ambapo Serikali za Halmashauri zenyewe huweka mafuta kwenye mitambo hiyo na kuwezesha ujenzi wa barabara hizo. Serikali itaendelea kutumia njia hiyo ili kuweza kuhakikisha kwamba barabara hizo zinaendelea kuwa bora zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa barabara za ndani, tutaendelea kuziboresha kama ambavyo tunaendelea kufanya. Nimshauri tu Mheshimiwa Ritta kwamba haiwezekani kufanya barabara hizo zikafikia kiwango cha lami kwa sasa kwa sababu ya majukumu mengine ya Serikali ya uendelezaji wa miundombinu katika maeneo mengine, hizi za mashambani zitakuwa bora lakini katika kiwango hicho hicho cha barabara za udongo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la pili la mwekezaji wa Kiwanda cha Karatasi pale Mgololo (MPM); suala hili ni pana, kubwa na la kina na Serikali mara kwa mara imekuwa ikitoa maelezo kuhusu suala hili la mwekezaji huyu ambaye historia yake ni ndefu inaanzia wakati wa Sera ya Ubinafsishaji ya Taifa huko miaka ya nyuma. Hata hivyo, kwa hali ilivyo sasa maelezo ninayoweza kuyatoa hapa kwa sasa hivi ni kwamba kwanza ieleweke kwamba miti ambayo ilikuwa inauzwa au ambayo inauzwa kwa mwekezaji ni magogo yanayotokana na miti ambayo ni ya umri mdogo.
Mheshimiwa Naibu Spika, umri wa uvunaji wa miti
kwa ajili ya bidhaa ya mbao ni miaka 25 na zaidi, lakini magogo haya ambayo yanauzwa kwa ajili ya uzalishaji wa bidhaa ambayo inakwenda kuwa malighafi kwa ajili ya uzalishaji wa karatasi inayoitwa pulp ni miaka kuanzia 14.
Kwa hiyo, si magogo yale yale ambayo anauziwa mwekezaji huyu ambayo wanauziwa wazalishaji wa mbao katika maeneo haya.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa ninachoweza kusema ni kwamba, kwa sababu ya kina cha maelezo katika suala hili, Mheshimiwa Waziri ameandaa maelezo ya kutosha kwa kirefu kuhusiana na suala hili kwa sababu ya kupokea hoja mbalimbali kutoka kwa wananchi wa maeneo hayo hayo na Mheshimiwa Ritta Kabati kwa kuwa ameungana na wananchi wa maeneo hayo kutaka kujua ni namna gani wananchi wananufaika zaidi na Taifa linanufaika zaidi basi muipe fursa Serikali tuweze kupata nafasi Mheshimiwa Waziri atakuja kutoa maelezo ya kina zaidi katika wakati ambao ataweza kutoa maelekezo.