Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 58 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 486 2017-07-03

Name

Ritta Enespher Kabati

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. RITTA E. KABATI aliuliza:-
Zao la mbao linachangia pato la Taifa katika nchi yetu na zao hili linazalishwa kwa wingi katika Wilaya ya Mufindi katika Mkoa wa Iringa:- Je, zao hili linaingiza fedha kiasi gani kwa mwaka.

Name

Eng. Ramo Matala Makani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ritta Enespher Kabati, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba mbao ni miongoni mwa mazao yanayochangia pato la Taifa na pia kutoa ajira kwa wananchi. Zao hili linazalishwa kwa wingi katika Wilaya ya Mufindi kutoka katika shamba la miti la Serikali la Sao Hill. Aidha, kiasi cha fedha kinachopatikana kwa mwaka hutegemea kiasi cha meta za ujazo kilichopangwa kuvunwa ambacho nacho kutegemeana na kiasi kinachoruhusiwa kitaalam kuvunwa kwa mwaka kulingana na mpango wa uvunaji wa kila shamba (annual allowable cut).
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na mdororo wa uchumi mwanzoni mwa miaka ya 1980, Serikali ilibinafsisha viwanda vyake vikiwemo viwanda vya bidhaa za misitu. Serikali ilibakia na jukumu la kuhifadhi misitu pamoja na kukuza miti katika mashamba yake. Hivyo, Serikali huuza miti iliyosimama kwa wawekezaji binafsi ambao huvuna na kuchakata magogo kwa ajili ya mbao, karatasi, nguzo na mazao mengine; shughuli za uchakataji zinabaki kuwa jukumu la sekta binafsi. Kwa kuwa Serikali haihusiki moja kwa moja na uchakataji, takwimu halisi zilizopo wizarani ni za ujazo wa miti inayouzwa kwa wadau mbalimbali na kiasi cha fedha kilichopatikana.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka 2015/2016, jumla ya meta za ujazo wa miti zipatazo 767,946.46 zilivunwa kutoka kwenye mashamba ya Serikali na kuiingizia Serikali jumla ya Sh.58,312,894,416.20. Aidha, kwa mwaka 2016/2017, mashamba ya Serikali yalivunwa na kuuza miti yenye meta za ujazo 754,931 kwa viwanda vya kuzalisha mbao na kuipatia Serikali fedha zipatazo Sh.55,102,043,000.00 ikiwa ni mrabaha na tozo, ushuru wa Halmashauri za Wilaya (CESS) na kodi ya ongezeko la thamani (VAT).
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa misitu ya asili, mapato yanayotokana na zao la mbao, ni wastani wa shilingi bilioni 18.3 kwa mwaka.