Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Dr. David Mathayo David

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Same Magharibi

Primary Question

MHE. DKT. DAVID M. DAVID aliuliza:- Vijiji 48 vya Jimbo la Same Magharibi vyenye zaidi ya kaya 2,943 havijapatiwa umeme wa REA japokuwa vina mahitaji makubwa ya umeme. Je, ni ipi ratiba ya kuwasambazia umeme wananchi hawa?

Supplementary Question 1

MHE. DKT. DAVID M. DAVID: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napenda sana kumpongeza Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri sana, lakini naipongeza Wizara hii kwa kuwa makini katika kufanya kazi katika sekta hii ya nishati na madini.
Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijauliza maswali
mawili ya nyongeza ningependa kuwapa pole wananchi wa Jimbo la Same Magharibi, hususan kata ya Hedaru ambao wamepoteza nyumba nyingi pamoja na mifugo na mazao kutokana na mvua kubwa iliyonyesha usiku wa kuamkia juzi.
Tunamuomba Mwenyezi Mungu Subhuhana Wataallah, aweze kutupa mvua za kiasi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa napenda kuuliza
maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-
Swali la kwanza, katika Mradi wa REA Awamu ya Pili, mkandarasi ambaye anaitwa SPENCON alishindwa kufanyakazi na kwa hiyo, vijiji vingi pamoja na vitongoji vingi vya Jimbo la Same Magharibi hususan vijiji 48, umeme haujakamilika kutokana na kwamba, mkandarasi huyo alishindwa kazi.
Je, REA Awamu ya Tatu, vijiji hivi ambavyo vilikosa umeme pamoja na vitongoji vyake, Serikali ina mkakati gani katika kuhakikisha kwamba, vitongoji vyote vinapata umeme na vijiji vyangu vyote vya Jimbo la Same Magharibi katika Awamu hii ya Tatu ya REA?
Swali la pili, je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari baada ya Bunge hili la Bajeti kuongozana na mimi kwenda katika Jimbo la Same Magharibi, ili akajionee mwenyewe vijiji na vitongoji ambavyo havina umeme katika Jimbo langu? Ahsante sana.

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, awali ya yote niungane na Mheshimiwa David kuwapa pole wananchi wake kwa tatizo walilopata.
Mheshimiwa Nibu Spika, kulingana na maswali yake mawili ni kweli kabisa katika utekelezaji wa REA Awamu ya Pili, Mikoa miwili ya Kilimanjaro na Singida haikukamilika ipasavyo na ni kweli kabisa mkandarasi SPENCON hakufanya kazi yake vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kutoa taarifa pia ya hatua za Serikali ambazo zilichukuliwa kutokana na kutofanya kazi vizuri kwa mkandarasi huyo.
Hatua ya kwanza tulichukua asilimia 10 ya mkataba wake ambayo ni retention kimkataba kabisa. Hatua ya pili, kazi hiyo sasa atapewa mkandarasi mwingine ili aikamilishe vizuri na wananchi wa Same waendelee kupata umeme. Lakini hatua ya tatu, tunaendelea sasa kuchukua hatua za kisheria, ili Wakandarasi wa namna hiyo sasa wapate fundisho waache kuwakosesha miundombinu wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Dkt. David Mathayo David kwamba wananchi wa Same, vijiji vyako vyote 48 vitapata umeme. Naelewa viko vijiji vya milimani kwa Mheshimiwa Dkt. David kijiji cha Muhezi, Malaloni kule Malalo pamoja na kwa Hinka, vitapata umeme.
Mheshimiwa Naibu Spika, kadhalika naelewa vile vijiji 48 anavyosema Mheshimiwa, yapo maeneo kama kule Hedaru, yako maeneo kule ambako Mheshimiwa tumesema Chekereni, Mabilioni pamoja na Jificheni Mabilioni, pamoja na kijiji cha Njiro vyote vitapata umeme. Hivyo, ninakuhakikishia kwamba vijiji ambavyo havijapata umeme kwenye REA II, sasa vyote vitapata umeme. Siyo vijiji tu hata vitongoji vyake na taasisi za umma pamoja na maeneo mengine muhimu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na suala lake la pili la kuongozana naye, kwanza kabisa niko tayari, ninaweza nikasema utakaponikaribisha utakuwa umechelewa,
ukichelewa sana utanikuta kwenye Jimbo lako, kwa hiyo, niko tayari kutembelea kwenye Jimbo lako.