Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Primary Question

MHE. CONSTANTINE J. KANYASU aliuliza:- Wananchi wa Mtaa wa Katoma na Magema katika Kata za Mtakuja na Kalangalula kwa muda mrefu wamezuiwa kuendeleza ardhi zao kwa sababu Mgodi wa GGM ulipima na kuweka vigingi vya mpaka ndani ya makazi yao. Je, ni lini mgodi huo utawalipa fidia ili kupisha shughuli za mgodi huo?

Supplementary Question 1

MHE. CONSTANTINE J. KANYASU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Naomba nimshukuru Mheshimiwa
Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri, lakini katika jibu lake naomba nifanye marekebisho kidogo kwamba kwanza
haiwezekani watu wakalipwa halafu wakadai, kwa sababu wanaolipwa wanalipwa kwa coordinates na eneo
linajulikana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niulize maswali mawili ya nyongeza. Kwa miaka 17 wananchi wa maeneo ya
Mizingamo, Ikumbiyaga, Compound pamoja na Mtakuja wako ndani ya eneo ambalo ni leseni ya mgodi, lakini
hawaruhusiwi kujenga, hawaruhusiwi kupima, hawaruhusiwi kuuza, lakini mgodi haujajiandaa kulitumia eneo hilo sasa wala kesho. Sasa ni nini hatima ya wananchi wa eneo hilo, kama mgodi sheria inasema utalipa tu fidia pale ambapo watataka kulitumia, lakini hawaruhusiwi kufanya chochote kwa miaka 17? Swali langu la kwanza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, kwa muda tofauti, Serikali kupitia Waziri wa Wizara husika, Naibu Waziri wa Mazingira, wamekuja na wameshuhudia aina ya uchimbaji wa madini wa Mgodi wa GGM ukiwa na madhara makubwa kwa wananchi wa Kata ya Kalangalala, Mjini Geita. Matokeo ya uchimbaji mbovu ni mipasuko ya nyumba inayotokana na mitetemo mikubwa, watu wengi wamezimia, lakini maji machafu yanatoka kwenye eneo la kuchimba na Mkurugenzi wa Mgodi aliyekuwepo ambaye alitaka kuleta suluhisho la migogoro hiyo, mgodi ulipoona anataka kuchukua hatua, ukamfukuza. Maagizo yote yaliyotolewa na Serikali hayajawahi kutekelezwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lini sasa Serikali itahakikisha mgodi unawalipa fidia wananchi ambao nyumba zao
zimepasuka kutokana na mitetemo ya uchimbaji wa dhahabu Geita?

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nampongeza sana Mheshimiwa Kanyasu jinsi ambavyo anapambana na kuhangaikia maendeleo ya wananchi wa Geita Mjini. Hongera sana Mheshimiwa Kanyasu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na swali la kwanza, ni kweli kabisa maeneo ya Compaund, Nyakabale,
Katoma pamoja na eneo lingine la Kagema, yako katika maeneo ya beacon. Kama ambavyo nilieleza kwenye jibu
langu la msingi, wananchi hawa ambao mgodi unahitaji eneo lile, tutakapolihitaji wakati wa uchimbaji, tutawalipa
fidia kwa wale ambao hawajalipwa fidia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa wako wananchi wachache ambao baada ya kulipwa fidia, pia walirejea katika maeneo yale. Kama haitoshi, mgodi ulilipa fidia ya umbali wa mita 570 badala ya mita 200 ili kuhakikisha
kwamba hakuna mwananchi ambaye anabaki bila fidia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo nimhakikishie Mheshimiwa Kanyasu kwamba suala hilo tumelipokea,
tutaendelea kulifanyia kazi. Kama kuna wananchi hawajafidiwa, basi itabidi wafidiwe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na suala la pili, kuhusu mipasuko. Kwanza kabisa niendelee kumpongeza
Mheshimiwa Kanyasu na Wabunge wote wa Geita, wakiwemo Mheshimiwa Mbunge wa Busanda na
Waheshimiwa wengine, pamoja na Mheshimiwa dada yangu yule wa Chama cha Upinzani wa Mkoa, waliita Mkutano, nilifika kule mwenyewe nikaangalia taarifa ya kampuni.
Taarifa ya kampuni ya awali ilionesha kwamba mpasuko hausababishwi na kampuni. Tuliunda tume, ikaleta matokeo, ikaonesha baadhi ya maeneo kwa kweli yanasababishwa na mpasuko wa kampuni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama haitoshi, tuliunda tume nyingine kwenda kutathmini majengo yaliyoharibika.
Nimhakikishie Mheshimiwa Kanyasu, ilionekana nyumba takribani 890 zilisababishwa kwa kiasi fulani na mlipuko wa Mgodi wa GGM.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu Mheshimiwa Kanyasu alitaka kujua ni lini sasa Serikali itatoa tamko? Tarehe
20 mwezi huu wa Aprili, timu ya wataalamu saba wakishirikiana na uongozi wa Wilaya pamoja na Jimbo lako
Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Mheshimiwa Mbunge na GGM watakwenda sasa kuangalia nyumba ngapi zinahitaji fidia ili fidia sasa itakapothibitika waweze kulipwa fidia wale ambao itaonekana kuwa halali.

Name

Boniphace Mwita Getere

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bunda

Primary Question

MHE. CONSTANTINE J. KANYASU aliuliza:- Wananchi wa Mtaa wa Katoma na Magema katika Kata za Mtakuja na Kalangalula kwa muda mrefu wamezuiwa kuendeleza ardhi zao kwa sababu Mgodi wa GGM ulipima na kuweka vigingi vya mpaka ndani ya makazi yao. Je, ni lini mgodi huo utawalipa fidia ili kupisha shughuli za mgodi huo?

Supplementary Question 2

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.
Katika Jimbo langu la Bunda kuna vijiji vya Nyabuzume na Nyaburundu. Kuna wachimbaji wadogo wenye PL wa muda mrefu sana. Tatizo wale wachimbaji wanachimba, madini yanapatikana, lakini pale wanaambiwa kwamba wana leseni za utafiti. Serikali ya kijiji iliwaomba kutoa huduma za maendeleo katika maeneo hayo ya Nyabuzuma na Nyaburundu, hawataki kutoa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujua ni sheria ipi inawataka hawa wachimbaji ambao wanapata madini,
hawataki kusaidia vijiji hivyo vinavyohusika?

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa hakuna sheria inayowakataza
wachimbaji wadogo au wachimbaji wakubwa wasilipe levy au mapato yoyote yanayotokana na uchimbaji wao. Sheria ya Madini pamoja na Sheria ya Fedha inawataka walipe.
Kwa hiyo, Mheshimiwa Getere kama kuna shida, wasiliana na sisi tukusaidie ili Halmashauri yako iweze kupata
fedha hizo.

Name

Anna Joram Gidarya

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. CONSTANTINE J. KANYASU aliuliza:- Wananchi wa Mtaa wa Katoma na Magema katika Kata za Mtakuja na Kalangalula kwa muda mrefu wamezuiwa kuendeleza ardhi zao kwa sababu Mgodi wa GGM ulipima na kuweka vigingi vya mpaka ndani ya makazi yao. Je, ni lini mgodi huo utawalipa fidia ili kupisha shughuli za mgodi huo?

Supplementary Question 3

MHE. ANNA J. GIDARYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mgodi wa Tanzanite uliopo Mkoa wa Manyara ni mgodi ambao unachukua idadi kubwa
ya vijana, lakini kumekuwa na vifo mfululizo miaka tisa sasa ambavyo havijawahi kufanyiwa utafiti wa kina ni kwa nini vifo hivi vinatokea.
Je, ni lini sasa Serikali itakaa na hawa wawekezaji wa vitalu husika ili kuanzisha utaratibu wa kifuta jasho kwa
familia zile ambazo zinapata maafa?

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa yapo madhara yanayotokana na uchimbaji, siyo katika mgodi wa Tanzanite One peke yake, hata katika migodi mingine. Sheria zinataka kama kuna mtu ameathirika na uchimbaji au na dhuluma yoyote, taratibu za kisheria lazima zifuatwe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili tumelichukua kwa muda mrefu, tunashirikiana na Wizara ya Kazi pamoja na
Kitengo cha Maafa ili kutathmini ukubwa wa tatizo la namna hiyo ili hatua zifuatwe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua ya pili, tumeunda timu inayojumuisha Wizara yetu, Wizara ya Kazi pamoja na
Halmashauri husika ili mwezi wa tano tuanze kuyatathmini madhara hayo. Baada ya tathmini itakapofanyika
Mheshimiwa Mbunge, tutakujulisha hatua kamili zitakazochukuliwa.