Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Edward Franz Mwalongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Primary Question

MHE. EDWARD F. MWALONGO aliuliza:- Baada ya ukarabati wa Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi vya FDC – Njombe na kile cha Ulebwe kilichopo Wanging‟ombe. (a) Je, ni fani zipi zitaanza kutolewa katika vyuo hivyo? (b) Je, ni wananchi wangapi wanatarajia kufaidika na vyuo hivyo?

Supplementary Question 1

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri. Nina maswali mawili madogo ya nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, Chuo cha Ulebwe ni chuo ambacho kina eneo linalozidi hekta 94 na kwa sasa hivi ninavyoongea, kina wanafunzi 64 tu.
Je, Serikali haioni kwamba sasa kutokana na mazingira mazuri ya Ulebwe kuna ulazima wa kubadilisha mifumo katika chuo kile na kuimarisha fani za kilimo na mifugo ili kusudi vijana wa Njombe waweze kunufaika na chuo kile? (Makofi)
Swali la pili, vijana wengi wamekuwa hawasomi hivi vyuo kwa sababu ya mfumo wanautumia kufundishia ambao ni wa VETA ambao sasa unatumia zaidi lugha ya Kiingereza katika mitaala pamoja na mafunzo yote na vijana wengi hawana uwezo wa lugha hiyo ya Kiingereza; je, Serikali iko tayari kuandaa mitaala ya Kiswahili ili iweze kuwasaidia vijana wadogo wanaomaliza elimu ya msingi na sekondari waweze kunufaika na haya mafunzo? (Makofi)

Name

Eng. Stella Martin Manyanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nyasa

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, kufuatia kubadilisha mafunzo katika chuo hicho, napenda tu kumfahamisha Mheshimiwa Mwalongo kwamba kwa mujibu wa Katiba yetu kifungu cha 9(i) kinazungumzia kwamba utajiri wa nchi na rasilimali utaelekezwa zaidi katika kuhakikisha kwamba unatoa umaskini, maradhi na ujinga katika maeneo yetu yote. Vilevile inaendelea kwa kusema kwamba haki ya kupata mafunzo au elimu ni ya Watanzania wote.
Mheshimiwa Naibu Spika, vyuo hivi vya FDC vilianzishwa kwa lengo la kuhakikisha kwamba wananchi wote hata wale ambao hawajafika kidato cha nne au darasa la saba wanapata mafunzo na kuweza kuwasaidia kukimu katika maisha yao ya kila siku.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ni mtazamo wangu kuona kwamba vyuo hivyo viimarishwe ili kuweza kutoa mafunzo kwa wananchi wengi zaidi ambao bado tunao katika maeneo yote. Sio wote kwamba wamefika darasa la saba au kidato cha nne.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile suala la kufanya mafunzo haya lazima yafanane na VETA, Wizara inaona kwamba iko haja ya kuona kwamba mafunzo yanayotolewa katika vyuo hivi vya FDC yanakidhi uwezo wa wananchi hao kuweza kuyatumia kikamilifu kwenye kazi zao na hivyo siyo lazima yafundishwe kama ilivyo Vyuo vya VETA.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hali hiyo, naona kwamba kwa siku za nyuma kulitokea na mkanganyiko kidogo wa kuona kwamba Vyuo vya VETA ni bora kuliko FDCs, lakini tungependa kuona kwamba FDCs zifanye kazi kwa malengo yake na VETA zifanye kazi kwa malengo yake, lakini vyuo vyote viimarishwe na kuweza kutoa mafunzo stahiki kwa walengwa wanaohusika.