Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Innocent Edward Kalogeris

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini

Primary Question

MHE. INNOCENT E. KALOGERIS aliuliza:- Je, lini Serikali itajenga Mahakama za Mwanzo katika Tarafa za Bwakira, Mvuli na Matombo – Morogoro Vijijini?

Supplementary Question 1

MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa majibu mazuri ya Serikali na hasa, sasa tunakwenda kujenga Mahakama katika Tarafa ya Bwakira Kata ya Bwakira Chini. Naipongeza Serikali, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Tarafa ya Bwakira Chini kuna hakimu ambaye anaitwa Deogratius Amatungiro, ni Hakimu ambaye amegeuza Mahakama kama duka la kuuza haki kwa wananchi kiasi ambacho wananchi wa Tarafa ya Bwakira Chini wamemchoka: Je, Mheshimiwa Waziri uko tayari kwenda nami katika Kata ya Bwakira Chini, Kata ya Kisaki na Kata ya Mngazi ambayo ndiyo Tarafa ya Bwakira, ukasikilize malalamiko ya wananchi? Kwa sababu viongozi mbalimbali wamepita lakini hakuna hatua yeyote ambayo imechukuliwa ili yeye kama msimamizi au ndiyo msimamizi katika Mahakama na Wizara ya Sheria uondoke naye huyo hakimu kwa sababu tumemchoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ni lini tunatarajia kwamba hiyo Mahakama ya Bwakira Chini itaanza kujengwa? Ahsante.

Name

Pauline Philipo Gekul

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Babati Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru, naomba sasa nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Innocent, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili ameuliza ni lini Mahakama hii katika Kata ya Bwakara Chini itajengwa? Nilijibu katika majibu yangu ya msingi kwamba mwaka huu wa fedha mhimili wetu wa Mahakama imetenga kujenga Mahakama za Mwanzo zaidi ya 60 na tuna zaidi ya shilingi bilioni 88 ambazo Bunge hili wametupititishia. Kwa hiyo, Mheshimiwa Innocent Mahakama hii tunajenga mwaka huu na ndiyo maana nimesema Mkandarasi sasa anatafutwa ili kazi hii ianze. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza, amemlalamikia Mheshimiwa Hakimu katika Mahakama hii ya Bwakira ambayo tunakwenda kujenga, japo inaendelea katika eneo la godauni. Naomba nimwelekeze Mheshimiwa Mbunge na Wabunge wenzangu kwamba tuna Kamati zetu za Maadili kwa Maafisa wa Mahakama na Wenyeviti wa Kamati hizi ni Ma-DC wetu katika Wilaya zetu lakini na Waheshimiwa Ma-RC. Kwa hiyo, Mheshimiwa Innocent kwa kuwa kanuni zetu zinatuhitaji, kama kuna malalamiko yoyote kwa Maafisa wetu wa Mahakama, tunapaswa kuandika kwa maandishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Mbunge aandike kwa maandishi ampelekee Mheshimiwa DC wa Morogoro ili Kamati ya Maadili ya Maafisa wa Mahakama katika Wilaya yake sasa waanze uchunguzi, na kama kuna tuhuma zitakuwa zimethibitika, basi hatua zitachukuliwa, ahsante.