Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Primary Question

MHE. ORAN M. NJEZA aliuliza:- Je, kuna Mkakati gani wa Kujenga Viwanda Maalum na Maghala ya ubaridi kwenye eneo la Tanganyika Packers Mbalizi?

Supplementary Question 1

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naanza kwa kumshukuru Mheshimiwa Waziri na Serikali kwa ujumla kwa majibu mazuri sana na pia kwa mikakati mizuri kuhakikisha eneo hili linatumika kiuchumi kwa nchi yetu ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa vile hili eneo liko mkabala na TAZARA na uwanja wa kimkakati wa Songwe na barabara ya TANZAM, je, Serikali ina mpango gani wa kutenga eneo kwa ajili ya bandari kavu na kujenga bandari kavu katika eneo hilo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ajili ya umuhimu wa eneo hilo, je, ni lini Serikali itaanza upimaji na kutenga maeneo ya eneo hili muhimu?

Name

Exaud Silaoneka Kigahe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mufindi Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Ni kweli Mkoa wa Mbeya ni moja ya mikoa ya kimkakati ambayo Serikali inauangalia kuhakikisha unawekezwa vizuri, kwa maana ya miundombinu wezeshi. Kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge, ni kweli eneo hili ni la kimkakati kwa sababu linapitiwa na barabara kuu inayoenda Zambia. Pia, kuna uwanja wa ndege na reli ya TAZARA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya maeneo ambayo Serikali inaweka mkazo ni kuweka miundombinu wezeshi yote. Hili suala la bandari kavu ambalo litasaidiana na miundombinu hii mingine nalo ni moja ya maeneo ambayo tunayaangalia ili kuboresha eneo hili ili liwe sehemu ya kusaidia kukuza biashara, kuuza nje lakini pia kuingiza bidhaa ambazo zinatoka maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana tunasema eneo hili ni kwa ajili ya uwekezaji mauzo nje kwa sababu tunategemea baada ya miundombinu kukamilika na bandari kavu pia itasaidia kuuza nje, kwa maana ya kuuza bidhaa zinazozalishwa katika eneo lile kwenda nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu upimaji, katika bajeti hii inayokuja tunayoenda nayo ni moja ya maeneo maalum ambayo tutaangalia namna ya kuyapima ili yaweze kutumika kwa ajili ya ujenzi wa viwanda na miundombinu mingine ikiwemo bandari kavu katika eneo hili la Mbeya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.

Name

Ally Mohamed Kassinge

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kusini

Primary Question

MHE. ORAN M. NJEZA aliuliza:- Je, kuna Mkakati gani wa Kujenga Viwanda Maalum na Maghala ya ubaridi kwenye eneo la Tanganyika Packers Mbalizi?

Supplementary Question 2

MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa swali la nyongeza. Kumekuwa na mpango wa muda mrefu wa Serikali kujenga kiwanda cha mbolea kinachotokana na gesi asilia ya Songosongo pale Mjini Kilwa Masoko. Kauli ya mwisho ya Serikali ni kwamba iko kwenye mazungumzo na mwekezaji. Nataka kufahamu na wana-Kilwa pia wanataka kufahamu;

Je, mpango wa kujenga kiwanda cha mbolea Kilwa-Masoko bado uko pale pale au umesitishwa?

Name

Exaud Silaoneka Kigahe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mufindi Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Ni sahihi kabisa moja ya mipango ya Serikali ni kuhakikisha tunajenga viwanda vingi vya kutosheleza mahitaji ya mbolea nchini. Ninyi ni mashahidi, tumeshaanza kujenga hicho cha Intracom hapa Dodoma lakini pia tunacho kile cha Minjingu ambacho kinaboreshwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiki cha Kilwa-Masoko ni mahsusi kwa sababu hawa watatumia gesi asilia ambayo nayo ni muhimu sana kwa ajili ya kuzalisha mbolea ambazo zinahitajika hapa nchini. Kwa hiyo, mpango wa Serikali ni kuhakikisha tunaendelea kutafuta wawekezaji na kukamilisha mipango hiyo. Ujenzi wa kiwanda hiki cha mbolea katika eneo hili la Kilwa-Masoko utatekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.