Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Muharami Shabani Mkenge

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bagamoyo

Primary Question

MHE. MUHARAMI S. MKENGE aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kusamehe gharama za matibabu kwa marehemu ili kupunguza maumivu kwa wafiwa?

Supplementary Question 1

MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza, kwa kuwa wananchi wengi wanapata changamoto wakati wa kwenda kutoa miili ya marehemu kwa kuweka dhamana ya Vitambulisho vya Taifa na kusababisha kukosa vitambulisho hivyo kwa muda mrefu kwa kupata huduma za kijamii mtaani.

Je, ni lini sasa Serikali itapanga utaratibu mwingine wa dhamana ili kuwaacha wananchi wabaki na Vitambulisho vyao vya Taifa, waweze kuendelea kuvitumia katika huduma za kijamii? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka kugawana gharama za matibabu nusu kwa nusu na wafiwa ili kuweza kuwasaidia watu wasio na uwezo kuondokana na mzigo wa madeni? (Makofi)

Name

Dr. Godwin Oloyce Mollel

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Siha

Answer

NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nampongeza Mheshimiwa Mbunge kwa kufuatilia vizuri kwenye eneo hili ambalo limekuwa likiwatesa Wabunge walio wengi. Kupitia swali hili namhakikishia Mheshimiwa Mbunge na Wabunge wote kwamba, tutaongeza nguvu sana kwenye kuona ni namna gani tunasimamia eneo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, kwa swali lake la kwanza, kwa maana ukichukua kadi ya mpiga kura unaweza ukamsababisha mwananchi huyu akakosa huduma nyingine wakati anaendelea kulipa deni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu, tutaenda kutafuta njia nyingine. Waraka haujasema chukua kitambulisho cha mwanannchi ya Taifa. Waraka unasema uwekwe utaratibu ambao mwananchi anaweza, tuna communication nyingi na njia nyingi za kuwasiliana ambazo hazihitaji kuchukua ile kadi ya Taifa, Kitambulisho cha Taifa. Kwa hiyo, tutakwenda kulishughulikia Mheshimiwa Mbunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, suala la kugawana; moja, kwanza kwa sasa gharama ambazo watu wanalipa kwenye hospitali za Serikali wanachangia, hawalipi package nzima ambayo inatakiwa kulipwa. Pia, tuna utaratibu ambao moja, huyo mwananchi akiufuata anasamehewa kabisa au kupunguziwa gharama kama hawezi kuzilipa zote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kuna mifumo mingi ambayo inaweza ikafanya. Sisi ni kusimamia na kuhakikisha wale watendaji walioko kule hospitalini ambao wanatakiwa kuwafuatilia watu na kuona namna ya kusaidiwa wafanye kazi zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shida ni kwamba, kuna baadhi ya watendaji wetu hawafanyi kazi zao kwa uadilifu. (Makofi)

Name

Salma Rashid Kikwete

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Mchinga

Primary Question

MHE. MUHARAMI S. MKENGE aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kusamehe gharama za matibabu kwa marehemu ili kupunguza maumivu kwa wafiwa?

Supplementary Question 2

MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa kuwa ugonjwa wa Kisukari unaongezeka siku hadi siku na kusababisha vifo vya watu wengi. Je, ni lini mashine za dialysis zitapelekwa katika Hospitali yetu ya Mkoa wa Lindi ili kupunguza vifo vitokanavyo na maradhi hayo na maradhi mengine? (Makofi)

Name

Dr. Godwin Oloyce Mollel

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Siha

Answer

NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nampongeza Mheshimiwa Mbunge, Mama Salma Kikwete kwa namna ambavyo anafuatailia shughuli za jimbo lake lakini pia masuala ya afya kwenye Mkoa wa Lindi. Kwanza nimwambie kwamba, kwenye jengo jipya ambalo linajengwa ndani ya hospitali ya mkoa, Jengo la OPD, humo ndani kunajengwa na sehemu ya kuweka vifaa vya dialysis. Jengo hilo litaisha mwaka huu mwezi wa nne, Mmaana yake na vifaa tayari viko site. Kuna mashine tisa ziko Mkoa wa Lindi zinasubiri jengo liishe zifungwe. Nakuhakikishia mwezi wa sita tutaanza kutoa huduma hiyo kwenye Mkoa wa Lindi. (Makofi)

Name

Margaret Simwanza Sitta

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Urambo

Primary Question

MHE. MUHARAMI S. MKENGE aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kusamehe gharama za matibabu kwa marehemu ili kupunguza maumivu kwa wafiwa?

Supplementary Question 3

MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, kwa kuwa wako wananchi ambao huwa wanaumwa na mbwa na kwa kuwa ili kukabiliana na kichaa cha mbwa hutakiwa kuchoma sindano si chini ya tatu, wakati mmoja hadi tano na sindano moja si chini ya shilingi 30,000. Je, Serikali haioni kuna umuhimu wa kuondoa gharama hizi ili wananchi wapate sindano hizo bure, kutokana na kwamba wengi hasa vijijini hawana uwezo wa kulipa kiasi hicho? (Makofi)

Name

Dr. Godwin Oloyce Mollel

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Siha

Answer

NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza hili swali na hili tatizo la kichaa cha mbwa, Mheshimiwa Mbunge Mama yetu Mama Sitta kwa kweli amekuwa akihangaika nalo hasa kwenye wilaya yake. Mimi niseme, tayari tumeshafanya hesabu kuona kesi za kuumwa na mbwa ziko ngapi nchini na tumeona kwamba inawezekana kugharamia hili kwa Serikali na tumeshatenga bajeti na sasa MSD wameshanunua dawa za vichaa vya mbwa na zimesambazwa sehemu mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kuwaambia Ma-DMO wote na Waganga Wakuu wa Mikoa, wasimamie vizuri kuhakikisha hakuna Mtanzania anayeumwa na mbwa na kucheleweshewa kupata tiba akitafuta fedha kwa ajili ya kupata hiyo sindano. Watibiwe mara moja na wapate sindano hiyo haraka sana. (Makofi)

Name

Vedastus Mathayo Manyinyi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Musoma Mjini

Primary Question

MHE. MUHARAMI S. MKENGE aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kusamehe gharama za matibabu kwa marehemu ili kupunguza maumivu kwa wafiwa?

Supplementary Question 4

MHE. VEDASTUS M. MATHAYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sera ya CCM inasema wazi, watoto chini ya miaka mitano matibabu ni bure. Akinamama wajawazito matibabu ni bure lakini kumekuwa na tatizo sugu la kuendelea kuchajiwa fedha; je, ni lini Serikali itahakikisha kwamba hilo tatizo linaisha? (Makofi)

Name

Dr. Godwin Oloyce Mollel

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Siha

Answer

NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, moja, hilo tatizo litaisha kwa sisi kushirikiana kwa pamoja. Kama ambavyo jana nilisema, miongozo na taratibu za Serikali ziko wazi, lakini inapofika kwenye vituo vyetu, zahanati zetu kule wilayani, watu hawafuati maelekezo ya Serikali; kwenye Serikali kwenye eneo husika, tunalo Baraza la Madiwani ambalo linatakiwa wakati wote kwenye mijadala yao wajadili na sehemu ya tiba na kuona watu wake kwenye eneo hilo wanahudumiwaje na Mkuu wa Wilaya kupitia Kamati ya Ulinzi na Usalama kufuatilia wakati wote na kuhakikisha haya maelekezo ya Serikali yanafuatwa vizuri.

Mheshimiwa Mbunge, tumekuja na Bima ya Afya kwa Wote. Ninakuomba Mheshimiwa Mbunge tushirikiane kwa pamoja inapofika wakati wa utekelezaji. Tushirikiane kwa pamoja kwa sababu tukishirikiana pamoja nakuhakikishia kwamba, tukienda kwenye Bima ya Afya kwa wote, hii migogoro yote itaenda kuisha na hatutaendelea kubishana kwa mambo madogo madogo kama haya.