Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 11 Sitting 42 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 550 2023-06-07

Name

Eng. Ezra John Chiwelesa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Biharamulo Magharibi

Primary Question

MHE. ENG. EZRA J. CHIWELESA aliuliza:-

Je, nini kauli ya Serikali kuhusu ucheleweshaji fedha zinazotumwa Nje ya Nchi kutokana na Mabenki kuwa na uhaba wa fedha za Kigeni?

Name

Hamad Hassan Chande

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kojani

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Engineer Ezra John Chiwelesa, Mbunge wa Biharamulo Magharibi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Benki Kuu ya Tanzania imechukua hatua kadhaa katika kupunguza athari kwenye soko la ndani la fedha za kigeni ili kusaidia shughuli za biashara na miamala kuendelea kufanyika. Hatua hizo ni pamoja na:-

a) Kuanzia Machi 2023 Benki Kuu imeongeza kiasi cha fedha za kigeni kinachouzwa katika soko la jumla la fedha za kigeni kutoka Dola za Marekani milioni moja hadi Dola za Marekani milioni mbili kila siku.

b) Kuongeza kiwango kinachoruhusiwa kuuzwa kwa muamala mmoja kwa njia ya rejareja kwenye soko la fedha za kigeni baina ya Mabenki kutoka Dola za Marekani 250,000 hadi Dola za Marekani 500,000.

c) Kuhakikisha ukwasi wa Shilingi ya Tanzania unabakia katika viwango vinavyoendana na mahitaji halisi ya kiuchumi kwa kutumia nyenzo mbalimbali za sera ya fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, benki za biashara nchini zimeendelea kutunza amana ya kutosha katika akaunti kwenye benki nje ya nchi ili kufanikisha miamala ya ulipaji wa bidhaa na huduma mbalimbali zinazoagizwa na kuuzwa nje ya nchi. Aidha, nazielekeza benki zote nchini, kuhakikisha kuwa zina akiba ya kutosha ya fedha za kigeni kabla ya kupokea fedha kutoka kwa mteja anayetarajia kuzituma nje ya nchi ili kuepuka ucheleweshaji.