Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 17 Energy and Minerals Wizara ya Madini 145 2021-04-27

Name

Ndaisaba George Ruhoro

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngara

Primary Question

MHE. NDAISABA G. RUHORO aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba Wananchi wa Jimbo la Ngara wananufaika na uchimbaji wa Madini ya Nickel unaotarajia kuanza katika eneo la Kabanga?

Name

Prof. Shukrani Elisha Manya

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ndaisaba George Ruhoro, Mbunge wa Jimbo la Ngara, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mbunge Mheshimiwa Ndaisaba kwa jinsi ambavyo anafanya ufuatiliaji kuhakikisha kwamba, wananchi wake wa Jimbo la Ngara wananufaika na mradi tarajiwa wa uchimbaji. Serikali imefanya mageuzi makubwa katika Sekta ya Madini kupitia Marekebisho ya Sheria ya Madini ya mwaka 2017 na kutungwa kwa sheria mpya za usimamizi wa rasilimali za Taifa kwa manufaa ya wananchi wa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, Sheria ya Madini, Sura 123, imeweka bayana kuwa, makampuni yote ya uchimbaji madini ni lazima yawasilishe mpango wa ushirikishwaji wa Watanzania katika miradi ya uchimbaji kwa maana ya local content plan ambao ni lazima ubainishe manufaa yatakayopatikana kwa wananchi kutokana na uanzishwaji wa miradi ya madini. Hivyo, kwa kuzingatia matakwa hayo ya Sheria, Serikali itahakikisha kwamba inachambua kikamilifu mpango utakaowasilishwa na Kampuni ya Tembo Minerals Corporation Limited inayotarajia kuwekeza katika mradi mkubwa wa uchimbaji wa madini ya nickel katika Jimbo la Ngara na kuusimamia kwa kushirikiana na Mamlaka zingine za Serikali kuhakikisha kuwa unatekelezwa na unaleta manufaa kwa wananchi wa Ngara na Taifa kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, mbali na suala hili la local content, wananchi wa maeneo yanayozunguka mradi watanufaika kama ambavyo makampuni mengine yote yanafanya kupitia malipo ya ushuru wa Huduma kwa maana ya Service Levy lakini pia na miradi itakayotekelezwa kupitia mpango wa Corporate Social Responsibility kwa maana ya CSR.

Mheshimiwa Spika, Wizara kupitia Tume ya Madini itaandaa mpango mahsusi wa uendeshaji wa semina elekezi kwa wananchi wa Halmashauri ya Ngara na halmashauri yenyewe na maeneo jirani ili kuwawezesha kubaini fursa zilizopo ikiwa ni pamoja na bidhaa na huduma mbalimbali ambazo wataweza kuzitoa katika mradi huo ili waweze kujiongezea kipato. Ahsante.