Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 14 Sitting 6 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 67 2019-02-04

Name

Flatei Gregory Massay

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Vijijini

Primary Question

MHE. FLATEI G. MASSAY aliuliza:-

Serikali iliahidi kuanzisha Baraza la Ardhi la Wilaya ya Mbulu. Aidha, wataalam wa Serikali walifika Mbulu na kukabidhiwa majengo kwa ajili ya Baraza hilo katika Mji wa Dongobesh na Mheshimiwa Mbunge akachangia shilingi milioni tatu za kuongeza miundombinu.

Je, ni lini Baraza la Ardhi la Wilaya ya Mbulu litaanzishwa?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Flatei Gregory Massay, Mbunge wa Mbulu Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, hadi sasa tuna jumla ya Mabaraza 97 ambayo yameundwa, ambapo kati ya hayo Mabaraza 53 yanatoa huduma na Mabaraza 44 likiwemo Baraza la Mbulu hayajaanza kutoa huduma kutokana na changamoto za uhaba wa rasilimali watu. Ili Baraza liweze kuanza kufanya kazi linahitaji kuwa na angalao Mwenyekiti mmoja, Katibu Muhtasi, Msaidizi wa Kumbukumbu, Msaidizi wa Ofisi, Dereva na Mlinzi.

Mheshimiwa Spika, hivi karibuni Serikali imeipatia Wizara Wenyeviti 20 ambao ni wajiriwa wapya. Wenyeviti tisa kati ya hao ni kwa ajili ya kuongeza nguvu katika maeneo hayo yaliyoelemewa kwa wingi wa mashauri katika Wilaya za Mbulu, Sumbawanga, Kibondo, Kigoma, Temeke, Bukoba, Mwanza, Musoma na Ulanga. Wenyeviti 11 kwa ajili ya mabaraza 11 ambayo hayana Wenyeviti katika wilaya za Ukerewe, Maswa, Kilosa, Same, Kyela, Shinyanga, Lindi, Iramba, Nzega, Lushoto na Tunduru. Taratibu za mafunzo ya awali zinafanywa ili Wenyeviti hawa waweze kupangiwa vituo na kuanza kazi katika Mabaraza hayo ambayo yana uhitaji mkubwa.

Mheshimiwa Spika, ili kuhakikisha kwamba Baraza la Mbulu linaanza kufanya kazi mapema iwezekanavyo, Wizara imeshatuma barua kwenda Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Manyara kupata mapendekezo ya wananchi wenye sifa, ili Mheshimiwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi aweze kufanya uteuzi wa Wazee wa Baraza la Ardhi na Nyumba kwa Wilaya ya Mbulu.

Mheshimiwa Spika, natoa rai kwa Wakuu wa Mikoa na Wilaya zitakazopata Wenyeviti wapya wa Mabaraza kutuma mapendekezo ya Wajumbe wa Mabaraza kwa wakati, kila wanapotakiwa kufanya hivyo, ili wananchi wasikose huduma kwa kukosekana Wajumbe wa Baraza. Aidha, Wakuu wa Mikoa na Wilaya wanashauriwa kuangalia uwezekano wa kutoa maeneo ya ofisi kwenye majengo yaliyo katika hali nzuri ili kurahisisha uanzishwaji wa Mabaraza katika Wilaya ambazo Mabaraza hayajaanza kazi.