Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 14 Sitting 1 Good Governance Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora) 5 2024-01-30

Name

Nicodemas Henry Maganga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Primary Question

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA aliuliza:-

Je, Serikali inachukua hatua gani kwa Watumishi wanaohusika kutumia vibaya fedha za miradi ya Serikali?

Name

Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nicodemas Henry Maganga, Mbunge wa Mbogwe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kusimamia masuala ya nidhamu katika Utumishi wa Umma kwa kuzingatia matakwa ya kifungu cha 6(1)(b) cha Sheria ya Utumishi wa Umma Sura 298 ambacho kimewapa Mamlaka Wakuu wa Taasisi kusimamia masuala ya nidhamu kwa watumishi walio chini yao pale wanapokiuka kiapo cha ahadi ya uadilifu.

Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia uvunjifu wa maadili katika utekelezaji wa majukumu ikiwemo utekelezaji wa miradi ya maendeleo, Serikali imeendelea kuwachukulia hatua mbalimbali za kinidhamu Watumishi wa Umma wanaotumia vibaya fedha za miradi ya maendeleo ikiwemo kuwasimamisha kazi na kuwaanzishia mashauri ya kinidhamu.

Mheshimiwa Spika, mathalan, katika kipindi cha Julai, 2022 hadi Desemba, 2023, TAKUKURU ilifuatilia matumizi ya rasilimali za umma kwenye utekelezaji wa miradi 2,541 yenye thamani ya shilingi trillioni 8.26, ambapo miradi 467 ilibainika kuwa na upungufu mbalimbali ikiwemo uvujaji na kutokuwa na thamani ya fedha. Kutokana na matokeo hayo, hatua kadhaa zilichukuliwa kwa mujibu wa Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Sura 329, ikiwa ni pamoja na kuanzisha uchunguzi kwa miradi 274 ambapo watumishi 51 walichukuliwa hatua za kinidhamu.