Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Grace Victor Tendega

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza:- Je, kuna mkakati gani wa kutenga fedha ili kuweka uwiano sawa kwa bajeti za Halmashauri kwani Halmashauri nyingi haziwezi kujiendesha?

Supplementary Question 1

MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Halmashauri nyingi zinakosa fedha za kujiendesha zenyewe kutokana na Serikali Kuu kuchelewesha zile asilimia ambazo zinawekwa na zinatengwa kwamba, kwa kisheria asilimia 20 ndiyo inabaki asilimia 80 inakwenda Serikali Kuu.

Je, Serikali iko tayari kutengeneza mfumo ambao utafanya Halmashauri zinapokusanya fedha zile asilimia 20 zibaki moja kwa moja katika Halmashauri zake, badala ya kusubiri zirejeshwe kama ambavyo Serikali inakuwa hairejeshi wakati mwingine?

Swali langu la pili, kwa kuwa Halmashauri ndiyo watekelezaji wakuu wa sera na mipango ya Serikali Kuu kwa ngazi ya chini. Je, Serikali haioni umuhimu wa kurejesha vyanzo vyote vya mapato ambavyo vinakusanywa katika Halmashauri ili viweze kuwasaidia kuendesha Halmashauri hizo? (Makofi)

Name

Deogratius John Ndejembi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chamwino

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Grace Tendega kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza la Serikali kuwa tayari kutengeneza mfumo kwa ajili ya kubakiza asilimia hizi kulekule kwenye Halmashauri ni wazo zuri na tunalipokea, tutakaa na timu ya wataalam kuona wamefikia wapi kwa sababu tayari pia wao walikuwa wanalifanyia kazi kwa ajili ya kutengeneza mfumo huo. Tutakaa kuona wamefika wapi na wenzetu vilevile wa Hazina kuona wamefikia wapi kwa ajili ya kuweza kutengeneza mfumo huu lakini ni wazo zuri.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili, tayari Serikali Kuu imeanza kuzirudishia Halmashuri vyanzo vile ambavyo wanakusanya. Mfano, katika mwaka wa fedha huu tunaoenda kuuanza wa 2023/2024 vyanzo vya makusanyo vile vya mabango ya matangazo vimerudishwa kule kwenye Halmashauri zenyewe ili ziweze kukusanya na tunaendelea kuangalia kama Serikali kwa ujumla wake ni vyanzo vipi viweze kuendelea kurudishwa kwenye Halmashauri zile ili kuziongezea uwezo.

Mheshimiwa Spika, vilevile Serikali kuu imekuwa ikipeleka fedha nyingi kwenye miradi ya maendeleo kwenye Halmashauri hizi hata zile ambazo hazina uwezo kutoka Serikali Kuu kwa ajili ya kuwasaidia katika ujenzi wa madarasa, katika ujenzi wa zahanati, katika ujenzi wa vituo vya afya na kadhalika ili kuwapunguzia mzigo Halmashauri hizi.