Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Elibariki Emmanuel Kingu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Singida Magharibi

Primary Question

MHE. ELIBARIKI I. KINGU aliuliza: - Je, lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara ya Singida – Sepuka - Ndago hadi Kizaga kwa kiwango cha lami?

Supplementary Question 1

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri ya kuwahakikishia Wana-Singida Magharibi kwamba kabla ya mwezi ujao tutakuwa tumesainiwa mkataba wa ujenzi wa barabara ya lami, kilometa 76; tunaipongeza sana Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu; je, Serikali sasa iko tayari kuifanyia upembuzi yakinifu barabara ambayo inatoka Singida – Mtunduru – Ighombwe – Iyumbu mpaka Tabora ambayo itaunganisha na barabara inayokwenda Kwamtoro – Kiteto mpaka Tanga ili kuwarahisishia wananchi wa Singida mawasiliano ya Tanga, Singida na Tabora?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; je, Serikali iko tayari kuipandisha hadhi barabara ya Puma – Ihanja – Iseke – Mwintiri – Igelansoni mpaka Itigi ili kuwapunguzia adha wananchi kutokana na uharibifu mkubwa wa barabara hii unaotokana na hali za mvua zinapokuwa zikinyesha?

Name

Atupele Fredy Mwakibete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Busokelo

Answer

NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Elibariki Immanuel Kingu, Mbunge wa Singida Magharibi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa ufuatiliaji wa karibu katika barabara hizi zote na hatimaye tunakwenda kusaini mkataba mwezi ujao (Juni).

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali lake la kwanza kuhusu upembuzi yakinifu katika hii barabara ya Singida – Mtunduru – Ighombwe – Ngungira mpaka Iyumbu yenye kilometa 113, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Singida Magharibi kwamba katika bajeti ya mwaka tutakaoanza 2023/2024 ambao mlipitisha bajeti siku ya Jumanne, tumetenga fedha takribani shilingi 165,041,665 kwa ajili ya kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina, na kwa maana hiyo barabara hii ipo katika mpango kama maandalizi ya kuja kuijenga kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili, kupandisha hadhi barabara ya Puma – Ihanja – Mwintiri – Iyumbu; barabara hii inahudumiwa na Wakala wa Barabara Mijini na Vijiji (TARURA) na sisi Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi tuko tayari kama itapandishwa hadhi kwa kufwata utaratibu ule ambao umewekwa, kwa maana ya kupitia kwenye vikao maalum, kupitia DCC, inakwenda kwenye Road Board ya Mkoa, na hatimaye Mwenyekiti wa Bodi anaandika barua kwa Mheshimiwa Waziri ili Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi atume timu kwenda kuikagua hii barabara na hatimaye tutoe hiyo ridhaa ya kupandishwa hadhi barabara hii, ahsante.