Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Faida Mohammed Bakar

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. FAIDA MOHAMMED BAKAR aliuliza:- Kumekuwa na ukiukwaji mkubwa wa huduma za afya na haki za uzazi katika baadhi ya sehemu jambo ambalo linaweza kuhatarisha maisha ya wanawake:- Je, ni lini Serikali itamaliza tatizo hilo?

Supplementary Question 1

MHE. FAIDA MOHAMMED BAKAR: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri naomba kuuliza kama ifuatavyo.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kauli chafu za baadhi ya wahudumu zinatuumiza sana mioyo yetu sisi wanawake hasa pale tunapokwenda kujifungua. Nikisema mfano hapa utalia, sitaki niseme mfano maana yake mambo mengine aibu. Je, Serikali inawachukulia hatua gani wahudumu kama hao na wako wengi tu? (Makofi)
Swali la pili, kwa kuwa, katika Tanzania kuna wale Wakunga wa jadi ambao hasa hasa vijijini wanatusaidia sana sisi wanawake wakati tunapojifungua. Naomba kujua kwamba, je, Serikali inawathamini vipi Wakunga hawa wa jadi ili kuwaweka katika mazingira mazuri au mazingira rafiki? Ahsante sana. (Makofi)

Name

Dr. Hamisi Andrea Kigwangalla

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba tu Mheshimiwa Dada yangu Mheshimiwa Faida Mohammed Bakar asitoe machozi na naomba nimjibu kama ifuatavyo; kwamba Serikali inawachukulia hatua gani wahudumu ambao wanatoa lugha chafu kwa wateja. Kwanza Serikali imeweka utaratibu mzuri sana wa kukusanya maoni na malalamiko ya wateja kwenye mahospitali yote. Pia Mheshimiwa Waziri wa Afya, Mheshimiwa Ummy Ally Mwalimu ambaye ni champion wa haki za uzazi na watoto hata kabla hajawa Mbunge amefika tu Wizarani na ameanzisha utaratibu wa kuwa na namba maalum ambapo maoni ya wateja kutoka popote pale, kona yoyote ya nchi yetu wanaweza wakayawasilisha kwenye namba hiyo na sisi moja kwa moja tukayashughulikia.
Mheshimiwa Spika, sambamba na jitihada hizo Mabaraza ya Weledi kwa maana ya Mabaraza ya Wauguzi, Mabaraza ya Madaktari, Mabaraza ya Wafamasia yana utaratibu wa kimaadili wa kuchukua hatua dhidi ya wataalam ambao wamesajiliwa na Mabaraza hayo pindi ushahidi utakapopelekwa kwenye mabaraza hayo na wana nguvu ya kimahamaka wakikaa kwenye Baraza la Kimaadili pale wanakuwa na nguvu ya Mahakama ya Hakimu Mkazi na kwa maana hiyo wanaweza kuchukua hatua za kisheria ikiwemo kuwaadhibu wataalam hawa kwa kuwapeleka jela.
Swali la pili, kwamba Serikali ina mikakati gani ya kuboresha huduma hizi? Tumejipanga vizuri Wizarani kuboresha huduma za akinamama wajawazito na watoto na hasa kuanzia ngazi ya kwenye jamii, kwa maana ya kuwatumia vizuri wakunga wa jadi. Serikali inawawezesha vipi jibu ni kwamba Serikali yetu ina utaratibu wa kuwapa mafunzo wakunga hawa wa jadi kwa maana ya traditional birth attendant kule kule kwenye maeneo yao, lakini pia kuwapa vifaa.
Mheshimiwa Spika, wanapewa vifaa kama gloves, pia kama wakigundua kuna tatizo kwa mama mjamzito mapema kabla hata siku ya kujifungua haijafika, wamepewa maelekezo ya namna ya kuwapa rufaa kuingia kwenye mfumo rasmi ya kutoa huduma za afya ya uzazi kwa akinamama. Kwa maana hiyo, wanapewa mafunzo wanathaminiwa, wanapewa vifaa na wanapewa maelekezo ya kuwa absorbed kwenye mfumo rasmi wa huduma ili akinamama hawa waondokane na hatari za kutibiwa katika hali ya complications na watu ambao hawana special skills za kuweza kutoa huduma hizo.

WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nataka tu kumthibitishia Mheshimiwa Faida na Waheshimiwa Wabunge na Watanzania tumeshatoa maelekezo kwa watumishi wetu wote katika sekta ya afya kuvaa vitambulisho. Kwa hiyo, pindi unapohudumiwa kitu cha kwanza ni vizuri uangalie anayekuhudumia ni nani, ni Ummy Ally Mwalimu na pale unapopata matatizo, tuletee jina la huyo mhudumu na tumesema hatutavumilia lugha chafu kwa wahudumu wetu kwa hiyo, tuletee jina na tutawapeleka katika Baraza la Wauguzi na Wakunga Tanzania na nimeshalielekeza baraza liongeze jitihada katika kuhakikisha tunarudisha nidhamu na maadili katika utumishi wa sekta ya afya. Kwa hiyo, Mheshimiwa Faida naomba usilie suala lako tunalifanyia kazi. (Makofi)