Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Angelina Adam Malembeka

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA (K.n.y. MHE. SAADA MKUYA SALUM) aliuliza:- Vituo vingi vya afya vya kijeshi vinahudumia maafisa wa jeshi na wananchi waliopo karibu na vituo hivyo. Hata hivyo vituo hivi vinakabiliwa na upungufu wa dawa, vifaa tiba na wataalam wenye ujuzi. (a) Je, Serikali inafahamu idadi ya vituo vyake vilivyopo Zanzibar? (b) Je, kuna mkakati gani unafanyika kuhakikisha kuwa vituo hivyo vinapatiwa dawa, vifaa tiba na wataalam wa kuhudumia wananchi?

Supplementary Question 1

MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri nina maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Kwanza nilitaka kufahamu ni mikakati gani iliyowekwa na Serikali katika kuongeza vifaa tiba na wataalam katika Hospitali zote za Jeshi zikiwepo za Zanzibar?
Pili, ni lini Waziri atafanya ziara katika vituo hivyo ili kuona hali halisi ya utendaji kazi katika vituo hivyo? Ahsante.

Name

Dr. Hamisi Andrea Kigwangalla

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, mikakati ya Serikali katika kuongeza vifaa tiba, dawa na watumishi kwenye Vituo vya Afya vya Kijeshi ni kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwanza Serikali kwenye bajeti zake kila mwaka imekuwa ikiongeza bajeti ya huduma za afya kwa ajili ya makamanda na wapiganaji wetu kwa sababu wanapewa umuhimu wa kipekee katika nchi yetu, lakini sambamba na kuongeza bajeti Serikali pia imeongeza mikakati ya kufundisha wataalam mahsusi kwa ajili ya majeshi na hivi karibuni tumepata wafadhili kutoka Ujerumani kupitia Serikali ya nchi hiyo ambao ni marafiki zetu ambapo wametujengea chuo kikubwa na cha kisasa cha kijeshi kwa ajili ya kutoa wataalam kwenye sekta za tiba na chuo hiki nikupe taarifa Kamati yako ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama inayoongozwa na Mheshimiwa Adadi mwezi Aprili, 2016 ilitembelea kwenye chuo hiki ambacho kimejengwa kwa msaada wa Serikali ya Ujerumani na wakajionea namna kilivyo kizuri na cha kisasa.
Mheshimiwa Spika, pia Kamati ilitupa ushauri kwamba kituo kile badala ya kuishia kutoa stashahada kiende mpaka ngazi ya degree na Jeshi likachukua ushauri ule na limekubali kukipandisha hadhi chuo hicho na mkakati wa kukiweka sawa inaendelea.
Sambamba na mkakati huo ili kutatua changamoto ya upatikanaji wa dawa, vifaa tiba na vitenganishi kwenye jeshi kwa sababu ya umuhimu wao tayari mikakati ya kuajiri wataalam wapya wakimemo madaktari bingwa na madaktari wa kawaida pamoja na wataalam wengine imeendelea kutekelezwa. Mpaka kufikia mwezi Machi madaktari takribani 143 waliajiriwa mahsusi kwa ajili ya kutoa huduma majeshini.
Mheshimiwa Spika, lakini pia kupitia chuo hiki ambacho kimeaznishwa tunaamini katika miaka ya karibuni kutakuwa hakuna changamoto ya watumishi lakini pia kupitia kwenye kuongeza bajeti yetu tunaamini changamoto ya upatikanaji wa dawa, vifaa tiba na vitenganishi nayo itakuwa imepatiwa ufumbuzi. Lakini suluhisho la kudumu ambalo Serikali inalifanya kwa sasa ni kutengeneza Bima ya Afya mahsusi kwa ajili ya makamanda na wapiganaji wetu na bima hii tayari imeshapata baraka za Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli na sasa hivi ndani ya Serikali mchakato wa kuirasimisha unaendelea ili ufike katika ngazi ya Baraza la Mawaziri na utekelezaji ufanyike.
Swali lake la pili, kwamba je Waziri itakuwa tayari kwenda kufanya ziara ninaomba nilichukue na nilifikishe kwa Waziri mwenye dhamana ili aweze kuzungumza na Mheshimiwa Mbunge na pengine kumpa majibu mahsusi kwamba ni lini ataenda kuvitembelea vituo hivi.