Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Muharami Shabani Mkenge

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bagamoyo

Primary Question

MHE. MUHARAMI S. MKENGE aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga gati ya kuegesha boti na vyombo vya usafiri Bagamoyo ili kuvutia watalii kutembelea Mbuga ya Saadan?

Supplementary Question 1

MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa Zanzibar inatembelewa na watalii wengi sana kwa kipindi cha mwaka mzima na wengi wanatamani kuja Bagamoyo kuja kuangalia vivutio vilivyopo pamoja na kutembelea Mbuga ya Wanyama ya Saadan, lakini kikwazo kikubwa wanachokipata ni sehemu ya kupaki boti kwa ajili ya kushuka ili waweze kufanya utalii. Je, Serikali ina mpango gani kuliingiza suala hili katika bajeti ya mwaka ujao ili kuunga mkono juhudi za Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan katika suala zima la Royal Tour?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa shughuli nyingi sana za usafiri kati ya Bagamoyo na Zanzibar za mizigo pamoja na abiria zinafanyika kwa boti za kawaida na majahazi ya kawaida. Je Waziri yuko tayari kutembelea Bagamoyo ili aone shughuli zinazoendelea pale ili alitilie umuhimu suala hili?

Name

Atupele Fredy Mwakibete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Busokelo

Answer

NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE): Mheshimiwa Spika, ahsante, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Muharami Shabani Mkenge, Mbunge wa Bagamoyo.

Sasa napenda kujibu maswali yake mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza anataka kujua nini committent ya Serikali katika bajeti ijayo kwa ajili ya ujenzi wa haya magati. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tumekuwa na mpango kabambe wa kuainisha bandari zote nchini ikiwemo na Bandari ya Bagamoyo katika ujenzi wa hizi gati na nimhakikishie kwamba tayari kwenye mwaka wa fedha ujao, ambako tutasoma bajeti yetu, tumetenga fedha kwa ajili ya kujenga gati katika Bandari hii ya Bagamoyo.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa, kwa mwaka huu wa fedha ambao unaendelea, tayari tumetenga kiasi cha Shilingi milioni 68 kwa kushirikiana na wenzetu wa Maliasili na Utalii ambapo tumeweka front dock yard kwa ajili ya kupokea majahazi, lakini pamoja na boti kwa sasa.

Mheshimiwa Spika, swali la pili anataka kujua ama anaomba nitembelee Bandari ya Bagamoyo na nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwa kushirikiana na yeye mara baada ya Bunge la Bajeti, nitafika Bandari ya Bagamoyo kujiridhisha. (Makofi)