Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Francis Kumba Ndulane

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kaskazini

Primary Question

MHE. FRANCIS K. NDULANE aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga Vituo vya Polisi katika Tarafa za Kipatimu, Njinjo na Nanjilinji Wilayani Kilwa?

Supplementary Question 1

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza, nina maswali mawili: -

Kwanza, kwa kuwa katika Tarafa mbili zilizobaki ambazo Serikali bado haijawekeza ujenzi wa vituo vya Polisi, kumekuwa na changamoto kubwa ya mapigano kati ya wafugaji na wakulima lakini wakati huo huo Tarafa hizo zipo umbali mrefu sana kutoka kule ambapo vituo vya Polisi vipo hivi sasa: -

Je, Serikali haioni kwamba kuna umuhimu katika Tarafa za namna hii zenye changamoto kubwa ya wakulima na wafugaji kuweza kuwekeza kama ilivyowekeza katika sekta nyingine ujenzi wa Vituo vya Afya kwa kuanzia na bajeti ya mwaka huu? (Makofi)

Pili, ningeomba Mheshimiwa Waziri anifahamishe ni lini atakuwa na nafasi ya kuweza kutembelea katika Wilaya ya Kilwa ili tuweze kushirikiana na Wizara yake katika kutatua changamoto ambazo zinakabili upatikanaji wa vituo vya Polisi. (Makofi)

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza kwa pamoja ya Mheshimiwa Francis Ndulane, Mbunge wa Kilwa Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza alitaka kujua mpango wa Serikali wa kujenga vituo vya Polisi kama vile ambavyo tunafanya katika vituo vya Afya na shule, nataka nimpe taarifa Mheshimiwa Mbunge kwamba wazo lake tumeshaanza kulifanyia kazi, tulikuwa na mazungumzo kati ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi pamoja na Wizara ya TAMISEMI.

Nichukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI, Mheshimiwa Innocent Bashungwa kwa kulipokea wazo hili na hivi sasa tunavyozungumza wataalam wetu, Makatibu Wakuu wa Wizara hizi mbili na wataalam wetu wanakaa kuangalia uwezekano huo kupitia kwenye Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hili ni jambo ambalo tunalichakata na kama litakuwa limekwenda vizuri tunaweza tukaliwasilisha hapa Bungeni kulingana na mapendekezo ambayo wataalam watatupatia.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na suala la mimi kutembelea, hilo halina mjadala. Nimhakikishie Mheshimiwa Francis Ndulane kwamba tutapanga ratiba ili tuweze kwenda katika Jimbo lake kuhamasisha wananchi, kama vile nilivyojibu kwenye swali la msingi kwamba kama wananchi wataweza kufanya utaratibu wa kupata eneo na hata wakianza wa kwa nguvu zao, kama ambavyo kuna maeneo Waheshimiwa Wabunge wamefanya, naye pia alifanya hivyo katika baadhi ya vituo vyake, hata juzi hapa Waziri wa Ardhi, Mheshimiwa Dkt. Angeline Mabula katika Jimbo lake pale, alifanya jitihada za kuhamasisha wananchi kujenga Kituo cha Polisi Ilemela. Kwa hiyo, jitihada kama hizi tutaziunga mkono.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Ndulane ninajua jitihada zake katika kupigania wananchi wake na hivyo basi nimhakikishie tutashirikiana kutafuta njia mbadala ya haraka wakati tukisubiri mipango ya muda wa kati na muda mrefu wa Serikali kutatua changamoto hii kwa kudumu.

Name

Tecla Mohamedi Ungele

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. FRANCIS K. NDULANE aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga Vituo vya Polisi katika Tarafa za Kipatimu, Njinjo na Nanjilinji Wilayani Kilwa?

Supplementary Question 2

MHE. TECLA M. UNGELE: Mheshimiwa Spika, ahsante kunipatia nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, maeneo mengi Mkoa wa Lindi yana changamoto ya usalama hasa katika migogoro ya wakulima na wafugaji hata wakati wa msimu wa korosho na ufuta usalama wa wananchi unakuwa mgumu. Maeneo mengi yapo mbali na Makao Makuu ya Wilaya, mfano Kilimarondo ipo kilometa 120, Nambiranje Wilaya ya Ruangwa napo ni mbali, pia Nangaru Wilaya ya Lindi.

Je, Serikali itajenga lini Vituo vya Polisi maeneo hayo ili kuwahakikisha usalama wa wananchi. Ahsante? (Makofi)

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kuhusiana na changamoto hiyo ama uhitaji huo wa vituo vya Polisi katika Mkoa wa Lindi, lakini kuna kazi ambayo tayari tumeshaanza kuifanya. Kwa mfano, katika bajeti hii ambayo tunaendelea nayo kuna maeneo ambayo Serikali inaendelea na ujenzi wa vituo vya Polisi na hata bajeti inayokuja tumezingatia hilo.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo hatuwezi kutatua changamoto hii kwa wakati mmoja kwa maeneo yote, lakini nitakapokuja kwenye ziara kuitembelea Kilwa Kaskazini nitamuomba Mheshimiwa Mbunge nae tuwe pamoja ili tuangalie namna gani tunaweza kuharakisha utatuzi wa changamoto hii. (Makofi)

Name

Salma Rashid Kikwete

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Mchinga

Primary Question

MHE. FRANCIS K. NDULANE aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga Vituo vya Polisi katika Tarafa za Kipatimu, Njinjo na Nanjilinji Wilayani Kilwa?

Supplementary Question 3

MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naamini Serikali inafanya kazi kubwa katika sekta zote, ninaamini na kujua kwamba ulinzi na usalama ni jambo muhimu sana katika ustawi wa wananchi na raia wake.

Mheshimiwa Spika, Jimbo langu la Mchinga lina Kata 11 na Tarafa nne, Tarafa mbili tu ndiyo zenye Vituo vya Polisi. Je, Serikali ina mpango gani kuhakikisha kwamba Tarafa hizi Mbili zilizobaki zinapata Vituo vya Polisi? (Makofi)

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Salma Kikwete Mbunge wa Mchinga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nijibu kwa ujumla wake kwamba mahitaji ya vituo vya Polisi kwa kweli ni makubwa labda nitoe mfano mmoja tu. Vituo Daraja ‘B’ vilivyopo ni 93 wakati mahitaji ni 563 utaona tofauti ilivyokuwa pana sana, kwa hiyo changamoto hii ipo maeneo mengi ikiwemo kwenye Jimbo la Mheshimiwa Salma Kikwete Mchinga.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie kwamba kama Serikali tunatambua changamoto hiyo na tupo katika hatua ambazo nyingine nilizieleza katika majibu yangu ya awali na hivyo basi tupewe muda ili tuweze kutatua changamoto hii kwa mapana yake kwa ujumla katika maeneo yote ambayo yana changamoto ikiwemo Jimbo la Mchinga. (Makofi)

Name

Mohamed Lujuo Monni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chemba

Primary Question

MHE. FRANCIS K. NDULANE aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga Vituo vya Polisi katika Tarafa za Kipatimu, Njinjo na Nanjilinji Wilayani Kilwa?

Supplementary Question 4

MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Polisi cha Wilaya ya Chemba ujenzi wake umesimama kwa miaka minne sasa, naomba kumuuliza Waziri ni lini sasa watatoa fedha za kumalizia? Ahsante. (Makofi)

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika utaratibu wa kumaliza vituo vya Polisi tumekuwa tukitumia njia mbalimbali ikiwemo kutumia Mfuko wetu wa Tuzo na Tozo ambao upo chini ya Jeshi la Polisi, ambao katika mwaka huu wa fedha tumeshaufanyia ujenzi na ukarabati wa vituo kadhaa katika maeneo mbalimbali nchini. Hivyo basi nichukua hoja hii ya kituo cha Chemba tuona kama tunaweza kumaliza kupitia Mfuko wa Tuzo na Tozo katika kipindi cha mwaka huu wa fedha unaokuja.

Mheshimiwa Spika, tuangalie kimefikia kiwango gani na mahitaji ni kiasi gani na uwezo wa fedha zilizopo ni kiasi gani na vipaumbele vilivyopo ni vipi.(Makofi)

Name

Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Primary Question

MHE. FRANCIS K. NDULANE aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga Vituo vya Polisi katika Tarafa za Kipatimu, Njinjo na Nanjilinji Wilayani Kilwa?

Supplementary Question 5

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Spika, ninashukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Katavi na Wilaya zake kumekuwa na wimbi la mauaji ya mara kwa mara hii ni kwa sababu hakuna vituo vingi vya polisi.

Je, ni lini mtatujengea kituo cha Polisi katika Kata ya Kasekese Wilaya ya Tanganyika?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Selemani Kakoso kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ninaomba nilichukue hili tulifanyie kazi ili tuone hatua ya kuchukua.