Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Neema Kichiki Lugangira

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. NEEMA K. LUGANGIRA aliuliza: - Je, Serikali haioni umuhimu wa kupitia upya mfumo wa haki jinai ili kupunguza changamoto ya idadi kubwa ya mahabusu kuliko wafungwa magerezani?

Supplementary Question 1

MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali na Mwanasheria Mkuu natambua kwamba mwaka jana tulibadilisha sheria ya kuzuia ukamataji kabla ya kukamilisha upelelezi, lakini jambo hili bado halitekelezeki na ndiyo maana hata hivi karibuni Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan amelisemea na amelitolea maelekezo; kwa mantiki hiyo nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; je, Serikali haioni umuhimu wa kurekebisha sheria ya mwenendo wa makosa ya jinai (CPA) ili kuweka ukomo wa upelelezi kama ambavyo wenzetu wa upande wa Zanzibar wamefanya na nchi jirani za Kenya, Uganda, Malawi na kadhalika?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; je, Serikali haioni umuhimu wa kuweka masharti nafuu ya dhamana kwa watu ambao hawana mali kwa sababu hivi sasa masharti ya dhamana ni makubwa kuliko makosa hivyo ni kana kwamba tunakomoa wananchi? Ahsante.

Name

Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, naomba kumjibu Mheshimiwa Neema Lugangira swali lake la nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika majibu ya msingi wakati najibu swali la Mheshimiwa Enosy Swalle nilieleza hatua mbalimbali ambazo Serikali imekuwa inaendelea kuzifanya kuboresha ili dhana nzima ya haki jinai na pia nimeeleza katika Bunge lako kwamba katika moja ya hatua kubwa ambayo imefanyika ni mashirikiano na taasisi mbalimbali zisizo za Kiserikali, Asasi za Kiraia na Taasisi za Dini na Vyuo vinavyotoa elimu ya sheria juu ya andiko lililotolewa kutafuta maoni ya watalaam hawa ili tuweze kufikia sehemu ya kujadili mambo yote ya msingi yanayoambatana na issue za haki jinai.

SPIKA: Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na Uratibu.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU: Mheshimiwa Spika Katiba yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na sheria zetu zipo wazi kabisa juu ya masuala ya haki jinai na katika eneo hilo la haki jinai ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge tuna pande mbili kuna wanaotenda jinai na wanaotendewa jinai. Sasa kama mpango mzima utakuwa ni kuwatetea waliotenda jinai uelewe upande wa pili kuna waliotendewa jinai. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivi karibuni tulikuwa tuna tatizo la panya road, sasa inasemwa hapa kama vile polisi wasikamate mpaka upelelezi upatikane na ndiyo maana tulipotunga hii sheria mwaka huu nafikiri tuliweka wazi kwamba kwa baadhi ya makosa ya kawaida ambayo hauoni sababu ya haraka ya kwenda kumkamata mtu kama upelelezi haujakamilika tunaweza tukasema yawe hivyo, lakini kwa kweli ni lazima tujue kwamba watu wanaotendewa makosa ndiyo wanaotakiwa kuonewa huruma zaidi na kusaidiwa kuliko wanaotenda makosa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mimi niombe rai kwamba twende hivyo kwasababu kwa kufanya hivyo ndiyo maana nchi ipo salama hata leo hii. Vinginevyo tukibadilisha jurisprudence hapa tunaweza tukaharibu kabisa haki jinai ikawa ni tatizo, lakini haki jinai inapande mbili. Ahsante. (Makofi)