Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Dr. Christine Gabriel Ishengoma

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kutatua tatizo la upungufu wa wataalamu wa afya hasa ma-nurse katika Vituo vya Afya na Zahanati Mkoani Morogoro?

Supplementary Question 1

MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, licha ya majibu mazuri niliyoyapata kutoka Serikalini, naomba kuuliza maswali mengine madogo mawili.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; je, kuna mkakati gani wa kutatua tatizo la upungufu wa dawa unaojitokeza kwenye Mkoa wa Morogoro?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; je, kuna mkakati gani wa Serikali kukabiliana na changamoto zinazojitokeza kwenye upande wa chanjo, hasa chanjo za akina mama wajawazito na watoto wachanga ambao unajitokeza Mkoani Morogoro, hususan Manispaa ya Morogoro? Ahsante.

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Christine Gabriel Ishengoma, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mkakati wa kutatua changamoto za upatikanaji wa baadhi ya dawa katika vituo vyetu, kwanza Serikali imeongoza bajeti ya dawa inayopelekwa Bohari ya Dawa (MSD) kwa zaidi ya mara saba na hivi sasa Serikali ilishapeleka MSD takribani shilingi bilioni 300 kwa ajili ya dawa, lakini pia mpango umewekwa kupeleka angalau kila mwezi shilingi bilioni 15 ili kuhakikisha kwamba dawa zinapatikana.

Mheshimiwa Spika, mpango wa pili ni kuhakikisha kwamba dawa zinazonunuliwa na kupelekwa kwenye vituo vyetu zinatumika ipasavyo na kuepuka matumizi mabaya ya dawa kwa maana ya upotevu wa dawa, lakini pia na fedha zitokanazo na uchangiaji wa huduma za dawa.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na mkakati wa kukabiliana na changamoto za chanjo katika Mkoa wa Morogoro. Kwanza naomba nipokee hoja ya Mheshimiwa Mbunge na baada ya hapa nitajifunza changamoto ni zipi ili tuweze kuona namna ya kwenda kuzitatua. Lakini jambo la muhimu ni kwamba ni haki ya msingi ya watoto na akina mama kupata chanjo na Serikali imeendelea kuhakikisha chanjo zinapatikana ili kuboresha huduma za wananchi. Ahsante.

Name

Yustina Arcadius Rahhi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kutatua tatizo la upungufu wa wataalamu wa afya hasa ma-nurse katika Vituo vya Afya na Zahanati Mkoani Morogoro?

Supplementary Question 2

MHE. YUSTINA A. RAHHI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na mimi kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Serikali imejenga hospitali za Halmashauri katika Halmashauri za Wilaya za Mbulu na Babati, na kwa sehemu kubwa hospitali hizo zimekamilika. Sasa Serikali inapeleka lini watalaam kulingana na ikama, lakini vilevile na vifaatiba? Ahsante.

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Rahhi, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa Hospitali za Halmashauri ni hatua moja ya kusogeza huduma za afya karibu zaidi na wananchi, lakini hatua ya pili ni kupeleka watendaji, kwa maana ya watumishi wa kada mbalimbali za afya, vifaatiba, lakini pia na kupeleka dawa.

Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba baada ya ujenzi wa hospitali hizo mpango wa Serikali ni kuendelea sasa kupeleka wataalam ili huduma ziendelee kutolewa kwa wananchi.

Name

Dennis Lazaro Londo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mikumi

Primary Question

MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kutatua tatizo la upungufu wa wataalamu wa afya hasa ma-nurse katika Vituo vya Afya na Zahanati Mkoani Morogoro?

Supplementary Question 3

MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kuna upungufu mkubwa sana wa kada ya uuguzi na madaktari katika vituo vyetu vya afya na zahanati zetu, na kwa kuwa tunaona kuna wimbi kubwa la wastaafu wa kada hizo wanaopewa barua za kustaafu kila siku.

Je, Serikali haioni umefika wakati sasa wa TAMISEMI kukaa na Wizara ya Utumishi ama kuwaongezea mkataba watumishi hawa ama kutoa fursa ya kutoa ajira ku-replace hawa watu ambao wanaondoka kwenye ajira kwa sababu bado wanakuwa kwenye bajeti?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dennis Londo, Mbunge wa Mikumi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kumekuwa na upungufu wa watumishi kwenye vituo vyetu, lakini jitihada za wazi za Serikali zimeendelea kuonekana, kwanza kwa kuajiri watumishi katika vituo hivyo. Kwa mwaka uliopita Serikali iliajiri zaidi ya watumishi 2,726 wa kada za afya na kuwasambaza nchini kote.

Mheshimiwa Spika, lakini upungufu huu wa watumishi pia unatokana na kasi kubwa ya Serikali ya kujenga zahanati, vituo vya afya na hospitali. Kwa sababu idadi sasa ya vituo hivyo imekuwa kubwa na automatically upungufu wa watumishi unaonekana. Kwa hiyo ni hatua nzuri sana kwanza ya kusogeza huduma kwa wananchi, lakini hatua ya pili ni kupeleka watumishi hao.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na kuwaongezea mkataba waliostaafu; tunafikiri ni busara kwa sababu kuna vijana wengi wamehitimu masomo ya utabibu, ya uuguzi, ni vyema wakaajiriwa badala ya kuongeza mikataba ya wale ambao wamefika umri wa kustaafu kwa mujibu wa sheria. Kwa hiyo, tutaendelea kuhakikisha kwamba fursa za ajira zikitokea vijana wanajiriwa kwenda kupunguza mapengo ya watumishi katika kada za afya. Ahsante.