Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Tecla Mohamedi Ungele

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. TECLA M. UNGELE aliuliza: - Je, Serikali ina mkakati gani wa kupunguza uhaba wa watumishi katika Idara ya Elimu katika Mkoa wa Lindi?

Supplementary Question 1

MHE. TECLA M. UNGELE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nashukuru kwa majibu ya Serikali, lakini nina maswali ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na upungufu mkubwa wa walimu wa sayansi katika Mkoa wa Lindi na hii inaleta ufaulu hafifu kwa wanafunzi katika masomo hayo.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kupatikana walimu wa sayansi kwa haraka iwezekanavyo kunusuru shida hiyo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia naona kwenye majibu kuna upatikanaji/kibali cha kuajiri walimu 10,000. Katika hilo naomba sana Serikali watupe kipaumbele Mkoa wa Lindi, kwa sababu tuna changamoto kubwa ya walimu. Ahsante sana. (Makofi)

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Tecla Mohamedi Ungele Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli tumekuwa na upungufu wa walimu wa sayansi katika shule zetu za sekondari nchini kote na tumefanya tathmini, kubaini mahitaji ya walimu wa sayansi angalau kuwezesha shule zetu kuwa na walimu wanaoweza kutosheleza mahitaji ya wanafunzi. Ndio maana katika ajira zilizopita asilimia 75.5 ya walimu wote walioajiriwa walikuwa ni walimu, wa masomo ya sayansi na utaratibu wa kuendelea kutoa kipaumbele kwa walimu wa sayansi katika ajira zinazofuata utaendelea.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na suala la kibali cha walimu katika halmashauri hiyo kupewa kipaumbele katika walimu 10,000, tutawapa kipaumbele na kazi iliyofanyika tumeainisha Mikoa yote yenye upungufu mkubwa zaidi wa walimu na watumishi wengine. Mikoa hiyo na Halmashauri hizo zitapewa kipaumbele wakati wa kuajiri watumishi hao. Ahsante. (Makofi)

Name

Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Primary Question

MHE. TECLA M. UNGELE aliuliza: - Je, Serikali ina mkakati gani wa kupunguza uhaba wa watumishi katika Idara ya Elimu katika Mkoa wa Lindi?

Supplementary Question 2

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Spika, nashukuru; Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe ina upungufu wa watumishi zaidi ya 1,700 wa kada ya ualimu. Kwa sababu za kijiografia watumishi wengi wamekuwa wakipangiwa wanaripoti baadaye wanaondoka.

Sasa Serikali haioni sababu za msingi na kwa sababu maalum kutoa kipaumbele kwa watu wenye taaluma ya ualimu, wazawa wa Ukerewe wakaajiriwa na wakapangiwa eneo la Ukerewe kuweza kuwasaidia watu wa jamii ile? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. (Makofi)

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Joseph Mkundi, Mbunge wa Ukerewe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kumekuwa na changamoto ya baadhi ya watumishi hasa wanaoajiriwa katika maeneo ya Halmashauri za vijijini kuomba uhamisho mapema mara baada ya kuajiriwa. Lakini mambo mawili yamefanyika Serikalini; la kwanza, katika ajira zilizopita tulihakikisha kila anayeomba ajira anaomba ajira kwa maana ya shule husika na Halmashauri husika. Tulikubaliana katika mikataba kwamba lazima wakae angalau miaka mitatu katika vituo vyao vile ambavyo wameajiriwa.

Kwa hiyo, suala hilo litakuwa endelevu tutahakikisha kwamba mtumishi yeyote anayeajiriwa, akishaajiriwa katika Halmashauri na shule hiyo lazima akae angalau miaka mitatu ili kuepusha wimbi la kuhama kwa maeneo ya vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini suala la kuwa na watumishi wazawa ni jambo jema na tumeendelea pia kuwapa kipaumbele. Lakini pia tunapenda utaifa kwa maana ya kwamba, waalimu wanaotoka Ukerewe waende maeneo mengine, lakini wanaotoka maeneo mengine waende pia Ukerewe ili kujenga utaifa wa nchi yetu, badala ya kuwa na watu wa aina moja katika eneo lile. Lakini tutaendelea kuhakikisha kwamba waalimu wanaopangiwa maeneo hayo, wanabaki na pia tunaendelea kudhibiti sana uhamisho katika maeneo hayo, ahsante. (Makofi)

Name

Husna Juma Sekiboko

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. TECLA M. UNGELE aliuliza: - Je, Serikali ina mkakati gani wa kupunguza uhaba wa watumishi katika Idara ya Elimu katika Mkoa wa Lindi?

Supplementary Question 3

MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana; pamekuwa na wimbi la vijana wengi waliomaliza vyuo vya elimu, kujitolea kwenye shule zetu za TAMISEMI.

Je, Serikali imejipanga vipi ku-accommodate vijana hao katika kibali cha ajira kilichotoka cha kuajiri vijana 10,000? (Makofi)

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba tumekuwa na walimu wanaojitolea katika shule zetu za Serikali, lakini pia na watumishi wa kada nyingine wakiwemo watumishi wataalam wa afya. Utaratibu ambao umewekwa na Serikali ni kuhakikisha wakati tunakwenda kutoa ajira kupitia vibali vya Serikali, wale waalimu ambao wanatambulika rasmi wanajitolea katika shule zile wanapewa kipaumbele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ndio maana kwenye jibu langu la msingi nimesema kwamba tunakwenda kuweka utaratibu wa kutumia mfumo wa kielektroniki, ambao utawatambua rasmi walimu na watumishi wengine wanaojitolea ili wapewe kipaumbele kwenye ajira zinazofuata. Kwa hiyo, hili tumelichukua tunaendelea kulifanyia kazi ili kuweza kurahisisha utendaji wake. Ahsante. (Makofi)