Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Justin Lazaro Nyamoga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilolo

Primary Question

MHE. LAZARO J. NYAMOGA aliuliza:- Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa Makao Makuu ya Polisi ya Wilaya ya Kilolo?

Supplementary Question 1

MHE. LAZARO J. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri lakini nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, Serikali inatarajia kupata fedha hizo lini ili wale wananchi waweze kulipwa fidia badala ya kuendelea kusubiri kwa muda mrefu?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kutokana na umbali uliopo kati ya Makao Makuu ya Wilaya na Kituo cha Polisi ambacho kinatumika kama Makao Makuu ya Polisi, Serikali ina mpango gani wa kuongeza fedha za OC ili ofisi ile ya Polisi ya Wilaya iweze kujiendesha bila karaha wala kuombaomba fedha kwa wadau wengine?

Name

Khamis Hamza Khamis

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Uzini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nyamoga, Mbunge wa Kilolo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ameuliza, je, lini Serikali italipa fidia? Nataka nimjibu Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inao mpango na italipa fidia wananchi hao kwa ajili ya eneo hilo kwa sababu inatambua umuhimu wa uwepo wa Kituo hicho cha Polisi ili wananchi waweze kupata huduma hizo. Kubwa zaidi tayari tumeshatoa maelekezo na wameshafanya tathmini wataalam kutoka Halmshauri ya Wilaya ya Kilolo inayohitajika kwa ajili ya fidia hiyo na tayari tumeshaelekeza pa kwenda kupata fedha hizo kwa ajili ya kulipa fidia wananchi hao. Kwa hiyo, nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inaendelea kufanya juhudi kuona namna bora ya kuwalipa fidia wananchi hao. Kubwa Mheshimiwa Mbunge aendelee kuzungumza na wananchi wake ili waendelee kuwa na subra jambo hilo limo mbioni kushughulikiwa.

Mheshimiwa Spika, swali la pili anauliza kama Serikali ipo tayari kuongeza OC. Niseme tu kwamba Serikali ipo tayari kuongeza OC lakini ni pale ambapo tutakuwa na fedha ya kutosha kufanya hivyo. Kwa hiyo, kwa sasa waendelee kuwa na subra hivyo hivyo tubananebanane lakini tunao mpango huo.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo upo mbadala ambao tumeshauchukua, kwanza tumeongeza operesheni ama doria za mara kwa mara katika maeneo ambayo wananchi wako mbali na vituo vya polisi ili waweze kupata hizo huduma za ulinzi. Vilevile tunaendelea kusisitiza ulinzi shirikishi ambapo inasaidia huduma za ulinzi kufika mpaka maeneo ya vijijini kwenye kata. Lengo na madhumuni ni wananchi waendelee kupata huduma za ulinzi na waishi kwa amani.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.