Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Rehema Juma Migilla

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ulyankulu

Primary Question

MHE. REHEMA J. MIGILLA aliuliza:- Je, Serikali ipo tayari kutenga fedha kwa ajili ya kumalizia ujenzi wa Vituo vya Afya vya Mwangozo na Uyowa katika Jimbo la Ulyankulu?

Supplementary Question 1

MHE. REHEMA J. MIGILLA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza niipongeze Serikali na kuishukuru pia kwa kuweza kutupatia fedha hizi ambazo nina uhakika zinakwenda kumaliza Kituo cha Afya cha Uyowa, lakini niendelee kuiomba Serikali basi hiki Kituo cha Mwangozo na chenyewe kiweze kufikiriwa ili kiweze kuendelea kutoa huduma. Hata hivyo, nina maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza; kwa taaluma mimi ni Mwalimu na tunajua vigezo ambavyo vinatumika kuanzisha hizi shule zetu, lakini ningeomba kujua, je, wataalam wa Afya na TAMISEMI huwa wanatumia vigezo gani wanapoamua kujenga hizi zahanati zetu, kwani tunaona baadhi tu ya majengo ndiyo yanajengwa pasipokuwa na maabara ambapo tunajua maabara ndiyo kigezo kimojawapo ili Daktari aweze kutoa huduma vizuri. Je, kwa nini zahanati nyingi huko vijijini hazina maabara?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kama vigezo hivyo vinazingatiwa, je, Serikali sasa haioni umuhimu wa kutujengea hizi maabara katika zahanati zetu ili kuweza kuwapunguzia mzigo hawa wananchi wetu ambao wanatembea umbali mrefu kwenda kufuata huduma za maabara? (Makofi)

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Rehema Juma Migilla, Mbunge wa Ulyankulu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, napokea pongezi zake kwa Serikali kwa kupeleka fedha shilingi milioni 600 kwa ajili ya kujenga Kituo cha Afya cha Uyowa. Pili, vigezo ambavyo vinatumika kujenga zahanati zetu ni michoro ambayo imepitiwa kitaalam na ambayo kimsingi kwa ramani zetu kwa sasa za Ofisi ya Rais, TAMISEMI za zahanati zina provision ya maabara. Kwa hiyo, ramani zote za vituo vya afya, zahanati na Hospitali za Halmashauri zina maabara. Hivyo, tutaendelea kuhakikisha tunatenga fedha kwa awamu kukamilisha yale majengo ya zahanati lakini pia na vyumba vya maabara kwa ajili ya kuhakikisha kwamba wananchi wetu wanapata huduma bora za afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, tunaona of course umuhimu wa kuhakikisha kwamba tunaendelea kujenga maabara na ndiyo maana kwenye swali la msingi nimeeleza ambavyo Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya kujenga vituo hivyo zikiwemo maabara katika maeneo hayo.

Name

George Ranwell Mwenisongole

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbozi

Primary Question

MHE. REHEMA J. MIGILLA aliuliza:- Je, Serikali ipo tayari kutenga fedha kwa ajili ya kumalizia ujenzi wa Vituo vya Afya vya Mwangozo na Uyowa katika Jimbo la Ulyankulu?

Supplementary Question 2

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa niaba ya wananchi wa Mbozi napenda kuuliza swali langu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Hayati Rais Magufuli akiwa kwenye kampeni aliahidi wananchi wa Mji Mdogo wa Mlowo kwamba kutajengwa kituo cha afya kikubwa cha kisasa pale. Tayari wananchi wameshapeleka site matofali 150,000 na tayari heka 10 zimeshatengwa. Sasa ni lini Serikali itapeleka fedha kuanza ujenzi wa kituo hicho cha afya katika Mji Mdogo wa Mlowo?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa George Mwenisongole, Mbunge wa Mbozi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ahadi za Viongozi wetu wa Kitaifa ni ahadi ambazo lazima Serikali tutakwenda kuzitekeleza na hivyo tumeandaa mpango kabambe wa kuhakikisha kwamba tunaratibu utekelezaji wa ahadi zote zilizotolewa na Viongozi wetu wa Kitaifa ikiwemo Kituo cha Afya cha Mlowo katika Jimbo la Mbozi. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaendelea kuweka mpango na kutafuta fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi wa Kituo cha Afya cha Mlowo, Mbozi.

Name

Simon Songe Lusengekile

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Busega

Primary Question

MHE. REHEMA J. MIGILLA aliuliza:- Je, Serikali ipo tayari kutenga fedha kwa ajili ya kumalizia ujenzi wa Vituo vya Afya vya Mwangozo na Uyowa katika Jimbo la Ulyankulu?

Supplementary Question 3

MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Serikali katika Jimbo la Busega imeanzisha vituo vya afya viwili ambavyo mpaka sasa vimeshaanza lakini bado vinakosa wodi ya wazazi, wanaume pamoja na wodi ya wanawake. Nini kauli ya Serikali ili kupeleka fedha kwa ajili ya kumalizia vituo hivyo vya afya?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Lusengekile, Mbunge wa Busega, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Serikali imejenga vituo vya afya viwili katika Jimbo la Busega na ujenzi ule unaendelea kwa awamu. Tumejenga awamu ya kwanza lakini tunafahamu kwamba kunakosekana wodi ya wazazi, lakini pia wodi ya wanaume na baadhi ya miundombinu mingine ambayo bajeti ijayo tutatenga fedha kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunakamilisha ujenzi wa miundombinu hiyo.