Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Edward Olelekaita Kisau

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kiteto

Primary Question

MHE. EDWARD O. KISAU aliuliza: - Je, Serikali ina mkakati gani wa kutoa ajira za upendeleo kwa vijana na fursa nyingine za kibiashara kwa wananchi wa Jimbo la Kiteto kupitia mradi mkubwa wa kimkakati wa Bomba la Mafuta (Hoima – Tanga) ambalo linapita katika Wilaya ya Kiteto?

Supplementary Question 1

MHE. EDWARD O. KISAU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi hii ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Nimshukuru Naibu Waziri kwa majibu yenye furaha kidogo kwa wananchi wangu.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kuna ajira nyingi sana zinasemwa kuwepo katika mradi huu, je, hawaoni kwamba wananchi wangu wa Kiteto hususan vijiji saba vile; Mwitikira, Ndorokoni, Dareta, Ovoponi, Kimana na Amei wakatengewa kabisa fursa za kibiashara na ajira za upendeleo kwa kuwa wao ndiyo wanabeba burden ya mradi huo kwa kilometa hizo 117?

Mheshimiwa Spika, swali lingine la pili dogo, je, Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kuwa amesema Wizara itaendelea kuhamasisha wananchi wajitokeze kuchukua fursa hizi atakuwa tayari kuongozana na mimi tutembelee vijiji hivi saba ili tutumie wasaa huu kuendelea kuwaandaa wananchi wetu kwa fursa hizo, tena ikizingatiwa kwamba Mheshimiwa Rais, Mama Samia Hassan Suluhu jana amekwenda kwenye kutiwa saini sasa kwa mkataba huu na kwamba karibu sasa mradi unaanza? Nakushukuru.

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kwanza napenda nitoe shukrani kwa jibu zuri la Mheshimiwa Naibu Waziri katika swali la msingi la Mheshimiwa Mbunge.

Mheshimiwa Spika, napenda kutoa taarifa ya jumla kwa wananchi wa Kiteto pamoja na maeneo mengine kwamba utekelezaji wa mradi huu unaanza mwezi huu Aprili, tulipanga tuanze mwezi Julai kama ambavyo tumeeleza kwenye jibu la msingi lakini tunaanza rasmi mwezi huu wa Aprili kwa muda wa miaka mitatu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya wananchi wa Tanzania ni kweli mimi nilishiriki nikiwa na Mheshimiwa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan utiaji saini utekelezaji wa mradi huu jana nchini Uganda. Mradi huu ni mkubwa utapita katika mikoa 8, wilaya 24, vijiji 127, vitongoji 502 vikiwemo vijiji na vitongoji vya Mheshimiwa Mbunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mradi utatoa ajira kwa zaidi ya Watanzania 10,000 katika hatua za awali na hadi ajira za Watanzania 15,000 katika shughuli za ujenzi na shughuli za kawaida. Kwa hiyo, nichukue nafasi hii kuwaomba sana wananchi hasa katika maeneo ambapo mradi utapita wajitokeze kuchukua hizi fursa kwa sababu tumeziweka rasmi kwa ajili ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spili, swali la pili la kufuatana naye, tumepanga kuanzia Kyaka nchini Tanzania kule Kagera hadi Tanga Chongoleani, tutaanza kufanya ziara wilaya kwa wilaya, mkoa kwa mkoa ili kuhamasisha Watanzania kuchukua fursa hiyo. Kwa hiyo, tutafika na katika eneo lake na kutembelea vijiji hivyo saba ambavyo Mheshimiwa amevitaja.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)