Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Ali Hassan Omar King

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Jang'ombe

Primary Question

MHE. ALI HASSAN OMAR KING aliuliza:- Je, wizi unapotokea kwenye akaunti ya benki ya mteja uliofanywa na mtumishi wa benki ni nani mwenye wajibu wa kumlipa mteja?

Supplementary Question 1

MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa jawabu hili zuri naipongeza sana Serikali kwa kuwa na utaratibu mzuri wa kuwajali wananchi wake dhidi ya vitendo hivi vya uhalifu vinavyotokeza katika mabenki ambavyo hufanywa na watumishi ambao sio waaminifu. Nimepata tamaa sasa na mimi. Swali la kwanza; je, ni lini Serikali itawalipa wateja 103 wa Tawi la NBC la Zanzibar Forodhani ambao fedha zao kiasi cha milioni 400 ziliibwa na watumishi wa benki hii ya NBC Forodhani kule Zanzibar pamoja na kuichukulia hatua au adhabu hiyo benki ya NBC kwa kutowalipa wateja hao?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili; ili kuhakikisha kwamba hawa wazee wanalipwa fedha zao hizi za kiinua mgongo ambao wengine tayari wameshafariki; je, Serikali iko tayari kufuatilia kwa haraka pamoja na mimi kuhakikisha kwamba haya waliyosema yanatokea?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ali Hassan King kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo nimejibu katika swali la msingi nilieleza kwamba, kwanza nieleze kwa mujibu wa Sheria ya Benki Kuu ya Tanzania ya Mwaka 2006 inaeleza kwamba moja ya majukumu ya Benki Kuu ni kusimamia ufanisi na usalama wa wateja, kusimamia na benki nyingine ili kuhakikisha usalama na ufanisi wa amana za wateja katika benki. Hiyo ndiyo dhamana yake kubwa. Kwa hiyo ikiwa tukio hili ambalo limejitokeza katika Benki ya National Bank of Commerce (NBC) ya uhalifu ambao umetokezea sasa haijaelezewa na muuliza swali kwamba uhalifu huu umesababishwa na nani. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge muuliza swali kwamba nitakapotoka hapa nitafuatilia suala hili tujue kwamba je, wizi huu ulivyofanyika, uchunguzi umeshafanyika kama ambavyo nimejibu katika swali la msingi? Kama uchunguzi huu umefanyika ni nani ambaye amesababisha uhalifu huu? Kama suala hili limesababishwa na wafanyakazi watumishi wa benki, basi hatua zitachukuliwa. Kama suala hili limesababishwa na mifumo ya Benki, basi Benki Kuu ya Tanzania itachukua dhamana ya kuhakikisha kwamba fedha zile zinarudishwa na benki ile na zitachukuliwa hatua benki husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niseme kwa sababu suala lake sio suala ambalo ni mahsusi, nahitaji kufahamu kwa undani hasa kujua hasa wizi huu uliojitokeza chanzo chake ni nini na kama uchunguzi umefanyika, umefikia katika hatua gani ili tuweze kutoa maelekezo ya jinsi gani hatua zitachukuliwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili kwamba tutakuwa tayari kufuatilia, ndiyo maana nikaeleza kwamba kwa sababu jambo hili ni jambo ambalo yeye Mheshimiwa Mbunge analifahamu zaidi tutakuwa tayari mimi na yeye tushirikiane tufuatilie ili tufahamu kabisa kwamba jambo hili limefika katika hatua gani na tuweze kuchukua hatua pale ambapo tumefikia.

Name

Zaytun Seif Swai

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ALI HASSAN OMAR KING aliuliza:- Je, wizi unapotokea kwenye akaunti ya benki ya mteja uliofanywa na mtumishi wa benki ni nani mwenye wajibu wa kumlipa mteja?

Supplementary Question 2

MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa huduma za fedha za Kibenki na huduma za fedha za mtandao zote ziko chini ya Sheria ya Fedha ya Benki Kuu ya Tanzania, naomba kuuliza; je, Serikali ina mpango gani kukomesha na kudhibiti wizi wa mitandao ambao imekuwa ni kero kubwa kwa wananchi wetu? (Makofi)

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Zaytun Swai, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli wizi wa mtandao ni moja kati ya njia ambazo zinatumika kuweza kufanya uhalifu wa kibenki na pale ambapo inabainika wizi huo wa kimtandao umefanywa na watumishi wa benki husika, basi watumishi hao huchukuliwa hatua.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyozungumza awali kwamba Benki Kuu ya Tanzania (BOT) inasimamia benki zingine kuhakikisha kwamba kwanza inaajiri wataalam au wafanyakazi ambao wanakuwa ni wenye weledi na wenye maadili ili kuhakikisha kwamba inasimamia sera na rasilimali watu kwenye benki. Benki Kuu yenyewe ya Tanzania inafanya tathmini kila mwaka kuhakikisha kwamba Menejimenti ya benki zote nchini inasimamiwa na Mameneja au Wakurugenzi ambao watakuwa na uadilifu.

Tatu, kumekuwa kuna utaratibu wa kuwa na registry ya kuhakikisha kwamba kuna orodha ya watumishi wote ambao wanakuwa sio waaminifu na pale ambapo wanakuwa sio waaminifu orodha ile inatawanywa katika benki zote ili watumishi wale wasiweze kupata fursa ya ajira katika benki nyingine kupunguza uhalifu wa aina kama hiyo ambao unakuwa unasababishwa na baadhi ya wafanyakazi au mameneja wa benki husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali kupitia Benki Kuu ya Tanzania inafanya jitihada kubwa sana kuona benki zetu nchini zinadhibiti uhalifu wa kimtandao usijitokeze hasa pale ambapo uhalifu huo unasababishwa na benki.

Mheshimiwa Naibu Spika, uhalifu wa mtandao mwingine ambao uko nje ya benki kama ambavyo unatokezea katika taasisi mbalimbali na wenyewe Serikali inashirikiana na vyombo vya dola ikiwemo Jeshi la Polisi kufanya uchunguzi pale ambapo yanajitokeza matatizo kama hayo na kuchukua hatua stahiki kwa mujibu wa sheria.