Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Sebastian Simon Kapufi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Mjini

Primary Question

MHE. SEBASTIAN S. KAPUFI K.n.y. MOSHI S. KAKOSO Aliuliza:- Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi ya shilingi milioni 400 aliyoahidi Waziri Mkuu kuchangia katika ujenzi wa Kituo cha Afya cha Kasekese kinachojengwa na wananchi?

Supplementary Question 1

MHE. SEBASTIAN S. KAPUFI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Ninayo maswali madogo mawili ya nyongeza kama ifuatavyo. Awali ya yote naishukuru Serikali kwa kutimiza ahadi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Maswali yangu madogo ni kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Kata ya Ikola wamefanya kazi nzuri ya ujenzi wa Hospitali Teule: Nini kauli ya Serikali katika kuwaunga mkono wananchi hawa?

Mheshimiwa Spika, swali la pili: Awamu ya tatu na ya nne kwa maana ya upelekaji vifaatiba katika vituo vya afya, tunacho Kituo cha Afya cha Ilembo, kwa bahati mbaya hakikubahatika kupata fedha hizo: Nini kauli ya Serikali katika kupeleka vifaatiba?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kapufi, Mbunge wa Mpanda Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza namshukuru sana kwa kupongeza juhudi za Serikali za kupeleka fedha kwa ajili ya ujenzi wa vituo hivi vya afya, lakini hizi kazi zote zinazofanywa ni dhamira ya Serikali hii ya Awamu ya Sita na Rais wetu Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora za afya kule walipo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Kata hii ya Ikona ambayo wananchi wamechangia nguvu zao kujenga kituo cha afya, kwanza niwapongeze sana kwa kuchangia nguvu zao, nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge pia kwa kuhamasisha wananchi hawa, lakini nimhakikishie kwamba Serikali inaendelea na mipango yake ya kuchangia nguvu za wananchi kwa kupeleka fedha ili kukamilisha vituo vya afya ambavyo tayari wananchi wameanza na ujenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo, hii itawekwa kwenye mipango na kadri ambavyo tutapata fedha tutakwenda kuhakikisha kwamba kituo hiki pia kinasaidiwa ili kikamilike na kuanza kutoa huduma bora za afya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na Kituo cha Afya cha Ilembo nayo kuhusiana na vifaatiba, tumeweka mkakati na katika mwaka huu wa fedha tumetenga zaidi ya shilingi bilioni 100 zinazotokana na tozo kwa ajili ya vifaatiba katika vituo vyetu. Kwa hiyo, tutaenda kuhakikisha vituo kama hivi pia vinapata fedha.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge tutampa kipaumbele katika kituo hicho. Ahsante sana.

Name

Ester Amos Bulaya

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SEBASTIAN S. KAPUFI K.n.y. MOSHI S. KAKOSO Aliuliza:- Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi ya shilingi milioni 400 aliyoahidi Waziri Mkuu kuchangia katika ujenzi wa Kituo cha Afya cha Kasekese kinachojengwa na wananchi?

Supplementary Question 2

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, moja ya kazi ya Serikali ya ujenzi wa vituo vya afya vilevile ni kupandisha hadhi vituo vya afya kuwa Hospitali za Wilaya. Hospitali ya Manyamanyama ni hitaji la Halmashauri ya Bunda kuwa Hospitali ya Wilaya. Hili swali nimeuliza huu ni mwaka wa 11; na liliamuliwa tangu enzi ya Mheshimiwa Mama Anna Abdallah, Mheshimiwa Mwakyusa, mpaka leo wameweka kibao cha Hospitali ya Wilaya, lakini vifaatiba na madawa mnatoa mgao wa kituo cha afya:-

Mheshimiwa Spika, ni lini sasa Serikali hii itaipa Hospitali ya Manyamanyama mgao wa vifaatiba na madawa kama Hospitali ya Wilaya na siyo tena kituo cha afya, maana kinatoa huduma mpaka katika Wilaya za jirani? Ahsante. (Makofi)

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ester Bulaya, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, utaratibu wa kupandisha vituo vya afya kuwa hospitali una vigezo kadhaa ambavyo vimewekwa. Moja ni kuwa na Halmashauri ambayo haina Hospitali ya Wilaya ndipo kituo kimojawapo cha afya ambacho kinakidhi sifa, kinapandishwa hadhi kuwa Hospitali ya Halmashauri. Kwa mfumo, sera na miongozo ya sasa,

Mheshimiwa Spika, Hospitali ya Wilaya ipo moja tu katika Halmashauri. Kwa hiyo, kwa sababu Halmashauri ya Mji wa Bunda ina Hospitali ya Halmashauri; na hiki kituo cha afya kwa nature yake kinahudumia wananchi wengi, tutahakikisha tunaongeza mgao wa dawa na vifaatiba ili iweze kuendana na idadi ya wananchi wanaopata huduma pale wakati tunaendelea kuboresha Hospitali hii ya Wilaya iliyopo katika Halmashauri ya Bunda. Ahsante sana.