Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Agnesta Lambert Kaiza

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. AGNESTA L. KAIZA Aliuliza:- Je, ni nini kauli ya Serikali kuhusu ucheleweshaji wa kupandisha vyeo kwa Askari wa Jeshi la Polisi katika ngazi ya Wakaguzi Wasaidizi na kwa Wakaguzi?

Supplementary Question 1

MHE. AGNESTA L. KAIZA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa nafasi hii ili niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu na takwimu zilizotolewa na Serikali, ukweli ni kwamba kutoka ngazi ya Mkaguzi Msaidizi kwenda Mkaguzi kamili inapaswa kufanyika ndani ya mwaka mmoja mpaka miaka miwili. Je, Mheshimiwa Waziri anayo taarifa kwamba kuanzia mwaka 2015 mpaka muda huu ambapo nimesimama mbele ya Bunge hili Tukufu kuna Wakaguzi Wasaidizi ambao hawajapandishwa madaraja?

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, Mheshimiwa Waziri atueleze hapa ikiwa anazo hizo taarifa ni kwa nini basi hao Wakaguzi hawajapandishwa madaraja?

Name

Khamis Hamza Khamis

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Uzini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Agnesta Lambert Kaiza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, si kweli kwamba tangu 2015 mpaka hapa tulipo watu hawajapandishwa madaraja. Kama ataangalia kwenye jibu langu la msingi nilitoa takwimu ambazo zinaonyesha kwamba kuna watu walipandishwa madaraja.

Mheshimiwa Spika, kingine nimfahamishe tu Mheshimiwa kwamba ni vizuri wakapata nafasi wakaipitia hii PGO (Police General Order) itawasaidia kujua baadhi ya taratibu ambazo zinatumika kupandisha madaraja. Kuna mambo ya msingi huwa yanaangaliwa, siyo kwamba watu wanapandishwa tu kwa sababu hawajapandishwa muda mrefu. Kwanza, lazima kipatikane kibali cha kupandisha majaraja. Pili, tunaangalia pia uwezo wa kiuongozi wa yule ambaye anatakiwa kupandishwa daraja. Tatu, tunazingatia zaidi vigezo vya kimaadili kwamba tunayekwenda kumpandisha cheo ana maadili gani katika kutumikia Taifa hili. Nne, tunaangalia kama hana mashtaka mengine. Tano, huwa tunaangalia na bajeti maana tukimpandisha cheo lazima tumpandishie na mshahara wake.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Mheshimiwa afahamu kwamba utaratibu ndiyo huo lakini tumeanza na tumepandisha madaraja mbalimbali kwa watumishi wa Jeshi la Polisi kama ambavyo taratibu zimeeleza.