Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Cecilia Daniel Paresso

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. CECILIA D. PARESSO (K.n.y. MHE. CONCHESTA L. RWAMLAZA) Aliuliza:- Je, ni lini Serikali itatengeneza eneo la Katokoro linalounganisha Kata za Katoro na Kyamulaile katika Jimbo la Bukoba Vijijini ili kuondoa adha ya usafiri inayowakabili wananchi wa maeneo hayo?

Supplementary Question 1

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana lakini kwenye tablets zetu hatuna Order Paper.

Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi, naomba kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza. Swali la kwanza, kumekuwa na utamaduni wa fedha nyingi zilizopangwa kwa ajili ya utekelezaji miradi mbalimbali ya barabara kucheleweshwa hivyo ufanisi wa kile kinachokusudiwa hakifikiwi. Je, Serikali sasa mko tayari kuhakikisha kama fedha zinatengwa kwa ajili ya ujenzi wa barabara yoyote zinatoka kwa wakati ili barabara hizo zitengenezwe?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, barabara ya Karatu inatoka Njia Panda – Mang’ola - Lalago ni barabara ambayo inaunganisha Mkoa wa Arusha na Mkoa wa Simiyu. Barabara hii imekuwa ikiahidiwa kujengwa kwa kiwango cha lami hasa kipindi cha uchaguzi ahadi inakuwa ni tamu kweli masikioni mwa wananchi lakini baada ya hapo barabara hiyo haijengwi kiwango cha lami. Serikali mtuambie ni lini kwa hakika barabara hiyo itajengwa kwa sababu Sera ya Wizara ya Ujenzi inasema kuunganisha barabara za Mikoa na Mikoa kwa kiwango cha Lami na barabara ile inaunganisha Mkoa wa Arusha na Mkoa wa Simiyu?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kuhusu fedha za miradi mbalimbali ya barabara kuchelewa kupelekwa katika miradi hiyo, utaratibu wa fedha kupelekwa katika miradi mbalimbali unazingatia upatikanaji wa fedha ambazo zimetengwa kwenye bajeti husika. Hivyo, kutokana na kutegemea mapato ya ndani kupata fedha kwa ajili ya kutekeleza miradi hiyo, mara nyingi kumekuwa na ucheleweshwaji na miradi hiyo kwa sababu ya upatikanaji wa fedha. Hata hivyo, Serikali imeendelea kuongeza jitihada kuhakikisha kwamba mapato yanakusanywa kwa wakati na fedha za miradi hiyo zinawasilishwa kwenye miradi husika kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, kwa kipindi cha mwaka huu wa fedha mpaka sasa takribani asilimia 48 ya fedha ya miradi ya barabara tayari imekwishawasilishwa katika mamlaka ya Serikali za Mitaa na kazi za utekelezaji wa miradi hiyo zinaendelea. Suala hili litaendelea kufanyiwa kazi kwa karibu zaidi.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na barabara ya Arusha Simiyu inayotokea Karatu, ni kweli hii ni barabara muhimu sana na inaunganisha mikoa hii miwili. Serikali ina dhamira ya dhati kuhakikisha kwamba barabara hizi kuu ambazo zinaunganisha mikoa zinajengwa kwa kiwango cha lami ili kurahisisha shughuli za kiuchumi na za kijamii.

Mheshimiwa Spika, kama alivyouliza kwamba Serikali imekuwa ikitoa ahadi, ni kweli na ahadi ya Serikali hakika itatekelezwa. Nimhakikishie tu kwamba mara fedha zikipatikana barabara hiyo itajengwa ili wananchi waweze kupata huduma zilizokusudiwa.

Name

Neema Kichiki Lugangira

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. CECILIA D. PARESSO (K.n.y. MHE. CONCHESTA L. RWAMLAZA) Aliuliza:- Je, ni lini Serikali itatengeneza eneo la Katokoro linalounganisha Kata za Katoro na Kyamulaile katika Jimbo la Bukoba Vijijini ili kuondoa adha ya usafiri inayowakabili wananchi wa maeneo hayo?

Supplementary Question 2

MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Kwanza kabisa, napenda kuipongeza Serikali kwa jitihada kubwa za kuboresha miundombinu ya barabara.

Mheshimiwa Spika, napenda kumfahamisha Mheshimiwa Conchesta kwamba tayari kazi ya kuboresha barabara ile inaendelea ili iweze kupitika ambapo sasa hivi wanafanya kazi za kuchepua maji, kuweka mawe na changarawe. Vilevile napenda kumfahamisha Conchesta kwamba mimi pamoja na Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Bukoba Vijijini tumeshawasiliana na Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI na barabara hii itafanyiwa kazi kwa kuzingatia mpango kazi uliowasilishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, aidha, kwa kuwa umuhimu wa kipande hicho cha barabara unafanana na barabara ya Kanazi - Kyaka kupitia Katoro, ni lini barabara hiyo nayo itatengewa fedha na kujengwa kwa kiwango cha lami?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE):
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Neema Lugangira, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, dhamira ya Serikali ni kuboresha miundombinu ya barabara ikiwepo barabara hii ya Kanazi, Kyaka kupitia Katoro. Kimsingi tathmini na upatikanaji wa fedha kwa ajili ya kujenga barabara hizi unaendelea. Mpango umeandaliwa kwa ajili ya kufanya tathmini lakini kuhakikisha kwamba barabara hizi zinatafutiwa fedha ili ziweze kujengwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali itaendelea kutekeleza mipango yake hii ya kufanya tathmini lakini pia kutafuta fedha ili barabara hizi ziwezwe kujengwa na kusogeza huduma kwa wananchi.