Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Anatropia Lwehikila Theonest

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ANATROPIA L. THEONEST Aliuliza:- Je, ni likizo ya muda gani wamekuwa wakipewa wazazi (watumishi wanawake na wanaume) pale wanapopata watoto mapacha zaidi ya wawili au watoto njiti?

Supplementary Question 1

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Swali la kwanza, Serikali imekiri kwamba matukio ya kujifungua watoto njiti au mtoto zaidi ya mmoja hayakuwa makubwa hapo awali ila tunaongea kujifungua watoto njiti na mtoto zaidi ya mmoja ni matukio ambayo yamezidi kuongezeka.

Je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka wa kutengeneza kanuni ya kuongeza siku kwa familia ambayo inapata hususan watoto njiti au watoto zaidi ya mmoja kwa sababu changamoto yake ni kubwa badala ya kuacha ilivyo leo inakuwa kama amnesty ya kupewa hiyo nafasi ya kulea hao watoto? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa wanaume ni kiungo muhimu katika familia na hasa familia inavyopitia changamoto ya kupata watoto njiti au watoto zaidi ya mmoja. Serikali haioni umuhimu pia wa kubadilisha kanuni ya kumruhusu mwanaume kukaa nyumbani kusaidiana na familia kwa si chini ya zaidi ya wiki mbili mpaka tatu ukizingatia kwamba hiyo likizo inatolewa mara moja kwa miaka mitatu ili akaisaidie familia pia? Nakushukuru. (Makofi)

Name

Dr. Mary Machuche Mwanjelwa

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Mbeya Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali madogo mawili ya nyongeza ya mdogo wangu Mheshimiwa Anatropia, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza nampongeza sana kwa kuona umuhimu wa maternity na paternity kwa watumishi wa Umma. Hata hivyo, kama nilivyojibu kwenye swali la msingi ni kwamba katika kile kifungu cha Kanuni za Kudumu za Utumishi wa Umma cha 12(3) kama Serikali tumeongezea siku 14 zaidi kwa wale wamama wote wazazi ambao wanajifungua watoto ya wawili.

Mheshimiwa Spika, hii ni kuonesha umuhimu kwa mama mzazi kwa sababu sote humu ndani ni wanawake na wanaume, tumezaliwa tumelelewa na wanawake na tunajua kabisa huyu mama mzazi anapojifungua anakuwa na complications nyingi lakini vilevile ndiyo anayenyonyesha watoto hata afya ya yule mama inahitaji kuimarika. Ndiyo maana kwa msingi huo tumeweza kuongeza siku 14 zaidi kwa mama mzazi huyu ambaye atajifungua watoto zaidi ya wawili.

Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili kuhusu paternity; vilevile nimeshajibu kwenye jibu langu la msingi kwamba katika kifungu kile cha 13 cha Kanuni za Kudumu za Utumishi wa Umma baba mzazi na yeye anatambuliwa kuwa ni baba wa mtoto na ndiyo maana tumetoa kile kifungu kisheria kabisa kwamba angalau siku tano maana siku tano zile za mwanzoni mama akijifungua ndiyo kipindi hatarishi ambacho mama naye anamuhitaji baba awepo nyumbani.

Mheshimiwa Spika, vilevile huyu baba endapo mazingira kutokana na ile familia hayaruhusu, basi anaweza akaomba kibali kutoka kwa Katibu Mkuu Utumishi kupitia kwa mwajiri wake. Ahsante.

Name

Hawa Mchafu Chakoma

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ANATROPIA L. THEONEST Aliuliza:- Je, ni likizo ya muda gani wamekuwa wakipewa wazazi (watumishi wanawake na wanaume) pale wanapopata watoto mapacha zaidi ya wawili au watoto njiti?

Supplementary Question 2

MHE. HAWA M. CHAKOMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Kanuni za Utumishi wa Umma hazikuainisha waziwazi mtumishi mwanamke anayezaa watoto zaidi ya wawili ama mtoto njiti anaongezewaje siku; na kwa kuwa Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini imetoa fursa ya kuingia mikataba ya hali bora mahali pa kazi, je, Serikali haioni umefika sasa wakati kwa kutumia hii fursa ya kutengeneza ama ya kuingia mikataba ya hali bora ya kazi kwa watumishi wanawake wanaopata watoto zaidi ya wawili ama kwa mwanamke anayezaa mtoto njiti? Ahsante. (Makofi)

Name

Dr. Mary Machuche Mwanjelwa

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Mbeya Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali moja dogo la nyongeza la Mheshimiwa mdogo wangu Mheshimiwa Hawa Mchafu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, wakati najibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge Anatropia nimesema kwamba Serikali inatambua na inajali wanawake wote ambao wanajifungua watoto zaidi ya wawili na ndiyo maana kama Serikali tumeweza kuongezea zile siku 14 ili kwa pamoja ziweze kuwa siku 98 kwa sababu likizo ya uzazi ni siku 84. Kwa maana hiyo wale wote wanaojifungua watoto njiti au watoto zaidi ya wawili tumewaongezea siku 14. Hii iko kisheria ili kuthibitisha na kuhakikisha kwamba huyu mama mzazi anastahili kupewa haki yake.

Mheshimiwa Spika, hili jambo naomba niwaambie Wabunge wote kwamba liko kisheria na tumeongeza hizo siku 14 zaidi kwa ajili ya akina mama wote wanaojifungua mtoto zaidi ya mmoja. Ahsante.

Name

Susan Anselm Jerome Lyimo

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ANATROPIA L. THEONEST Aliuliza:- Je, ni likizo ya muda gani wamekuwa wakipewa wazazi (watumishi wanawake na wanaume) pale wanapopata watoto mapacha zaidi ya wawili au watoto njiti?

Supplementary Question 3

MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nataka pia kujua, kwa kuwa nchi yetu tuna watumishi wa umma na watumishi katika sekta binafsi na siku zote tumekuwa tukihamasisha PPP, Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kwamba kama kuna hilo tatizo waajiri wawasiliane na Katibu Mkuu Utumishi.

Je, wale wafanyakazi au watumishi wanawake wenye matatizo hayohayo lakini wanafanya kwenye sekta binafsi, wao watasaidiwaje kwa sababu nchi ni moja? Ahsante. (Makofi)

Name

Jenista Joackim Mhagama

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Peramiho

Answer

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika, kwanza, naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa niaba ya Ofisi ya Rais, Utumishi wa Umma kwa majibu mazuri aliyoyatoa.

Mheshimiwa Spika, Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini Na. 6 ya mwaka 2004, kifungu cha 33 kimeweka masharti ya kuhakikisha kwamba huduma bora kwa akina mama wote wajawazito, wanaojifungua na wanaume kwa maana ya waume wa akina mama hao kwenye private sector na wao wanapewa haki sawa na stahili katika kuhakikisha kwamba suala la uzazi linapewa kipaumbele pia kwa watumishi wa sekta binafsi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee kutoa wito kwa waajiri wote nchini kuhakikisha wanatekeleza matakwa hayo ya Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini Na. 6 ya mwaka 2014 na hivyo kuwafanya wanawake wote wa Tanzania waweze kuthaminiwa katika suala hili muhimu sana la kukuza uhai katika dunia hii. Ahsante.