Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Livingstone Joseph Lusinde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtera

Primary Question

MHE. LIVINGSTONE J. LUSINDE aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga kituo kikubwa cha polisi katika Jimbo la Mtera hususani katika Kijiji cha Mvumi Misheni ili kukabiliana na wimbi kubwa la uhalifu katika Jimbo la Mtera?

Supplementary Question 1

MHE. LIVINGSTONE J. LUSINDE: Mheshimiwa Spika, nikushukuru tena kunipa nafasi ili niweze kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Jimbo la Mtera lina kata 22, na lina vijiji zaidi ya 60 na kitu, Mheshimiwa Naibu Waziri kwenye jibu lake la msingi anasema wana mpango wa kujenga vituo kila kata, haelezi mpango huo unaanza lini? Lakini Jimbo la Mtera lina Tarafa tatu.

Swali langu la kwanza dogo la nyongeza linasema, kama kwenye Tarafa tu hawajajenga Kituo hata kimoja, je hiyo kwenye kata itawezekana? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, barabara kubwa ya Iringa - Dodoma inayopita kwenye Jimbo la Mtera, Kibakwe, Isimani Waheshimiwa Wabunge wengi na Mawaziri wanapita njia ile lakini haina Kituo cha Polisi hata kimoja chenye gari. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, matokeo yake ajali zote kubwa zinazotokea njia ile, polisi inawachukua muda mrefu sana kufika, kwa mfano wiki mbili zilizopita ilitokea ajali mbaya sana mama mmoja mzazi alipoteza maisha, nesi alipoteza maisha, pamoja na wasindikizaji, polisi walikuwa wanakuja wengine na lori, fuso iliwachukua muda sana kwenda kumaliza tatizo pale.

Je, Serikali ni basi itakipatia Kituo cha Mvumi Misheni gari, walau liweze kusaidia kufanya mzunguko katika barabara hiyo kubwa? Ahsante sana. (Makofi)

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza linahusu ujenzi wa Kituo cha Polisi kutokana na majibu yangu ya msingi kwamba nilimwambia tuna mpango wa kujenga vituo vya polisi nchi nzima katika kila kata.

Mheshimiwa Spika, nataka nimweleze Mheshimiwa Mbunge kwamba ujenzi huu au mpango huu wa ujenzi wa vituo ni mchakato ambao mchakato unahusisha pia upatikanaji wa rasilimali fedha.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo dhamira tunayo, sababu tunayo na uwezo pia tunao, lakini uwezo huo utaenda sambasamba na kadri ambavyo hali ya kibajeti itaruhusu kwa awamu, kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ujenzi wa Kituo cha Polisi katika Kata ya Mvumi Misheni utapewa kipaumbele pale ambapo bajeti itakaa vizuri na mpango wetu utaanza utekelezaji wake mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Lusinde kwa sababu inaonekana ni Mbunge ambaye hapendi kujipa ujiko mwenyewe, lakini kiukweli hili jambo tulilizungumza mimi na yeye pamoja na Mheshimiwa Chumi ambao Majimbo yao yanapakana katika eneo hilo na wenyewe wao walikuja na wazo zuri sana la upatikanaji wa magari mawili katika eneo hilo na mchakato huo umeshaanza, naamini kabisa mimi nikishirikiana na wao tutafanikisha kupata hayo magari mawili kwa utaratibu ambao tumeuzungumza mimi, yeye pamoja na Mheshimiwa Chumi na wananchi wasikie waone jitihada za Mheshimiwa Lusinde katika hili na manufaa yake watayaona muda siyo mrefu kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu. (Makofi)