Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Angelina Adam Malembeka

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA aliuliza:- Majanga ya moto yamekuwa yakitokea mara kwa mara hasa Viwandani, Majumbani na katika majengo ya Serikali:- (a) Je, Serikali ina mkakati gani wa kutoa mafunzo kwa Wafanyakazi na wananchi juu ya mbinu za kujihami na kujiokoa katika majanga ya moto? (b) Je, Serikali imejipangaje katika kutoa mafunzo katika maeneo ya kazi na wananchi juu ya matumizi ya mitungi ya kuzima moto (Fire Extinguishers)? (c) Je, Serikali ina mpango gani wa kukagua mitungi hiyo kama bado inafaa kwa matumizi au imeshapita muda wake wa kutumika?

Supplementary Question 1

MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza. Kwanza nimpongeze Naibu Waziri kwa majibu mazuri ambayo yanaonesha kabisa Serikali ina nia nzuri ya kusaidia wananchi wake. Kwa niaba ya wanawake wa Mkoa wa Kaskazini Unguja nilikuwa nina maswali mawili ya kuongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nilitaka kujua: Je, huduma ya uokoaji na kuzima moto kuna gharama zozote ambazo mhudumiwa anatakiwa alipe?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili: Je, kama gharama hizo zipo, ni utaratibu gani unatakiwa ufanywe ili aliyepatiwa huduma aweze kulipa bila kuwa na taharuki? Maana kipindi kile anakuwa amechanganyikiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kwa dhati kabisa nimpongeze sana Mheshimiwa Malembeka kwa kazi nzuri ambayo anayoifanya katika Mkoa wake wa Kaskazini. Kwa kweli anawatendea haki wapiga kura wake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, nikijibu maswali yake pamoja, kwanza huduma za kuzima moto ni za bure, hakuna gharama. Hata hivyo, kwa mujibu wa sheria ya Jeshi la Uokoaji na Zimamoto ya mwaka 2007 Sura ya 427, inaeleza kwamba Jeshi la Zima Moto na Uokoaji lina Mamlaka ya kuweza kutoa leseni kwa makampuni binafsi kutoa huduma hizo ikiwemo huduma ya kuzima moto pamoja na vifaa.

Mheshimia Naibu Spika, kwa hiyo, makampuni haya ndiyo ambayo yanaingia mikataba na Taasisi binafsi na ndiyo yanakubaliana malipo, lakini kwa maana ya huduma hizi za zimamoto ni bure.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na utaratibu ambao unatumika, unapiga namba 114 na kikosi chetu kinafika pale haraka iwezekanavyo kutoa huduma hizo bila malipo yoyote. (Makofi)