Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Maftaha Abdallah Nachuma

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Mtwara Mjini

Primary Question

MHE. MAFTAHA A. NACHUMA aliuliza:- Je, Serikali inahakikishaje amani na utulivu vinakuwepo katika chaguzi mbalimbali nchini?

Supplementary Question 1

MHE. MAFTAHA A. NACHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri nina maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; hivi sasa Manispaa ya Mtwara Mikindani kumekuwa na baadhi ya Viongozi wa vyama vya siasa wa wilaya na mkoa ambao wameweza kuratibu vikundi mbalimbali kwa ajili ya kufanya uhalifu kwenye uchaguzi unaotarajia kufanyika mwaka huu 2020. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, je Serikali Mheshimiwa Waziri yuko tayari hivi sasa kuja Mtwara kuweza kuchukua ushahidi ambao nitampatia kwa mikono yangu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili Manispaa ya Mtwara Mikindani kuna baadhi ya viongozi wa vyama vya siasa wanachukua na kuwatumia baadhi ya askari polisi kwenda kuwafanyia hujuma Wapinzani usiku saa nane, saa tisa na kuwagongea majumbani kwao na kuwakamata bila sababu yoyote ya msingi na kwenda kuwaweka ndani eti kwa sababu tu wanafanya kazi ya kunadi Chama cha Wananchi - CUF na vyama vingine vya Upinzani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, je, Serikali iko tayari hivi sasa kuwachukulia hatua Askari wa aina hiyo wanaotumika kwa ajil ya Chama Tawala? (Makofi)

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Maftaha Nachuma kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la kwanza ameuliza kama nipo tayari kwenda kuchukua ushahidil; nimuhakikishie kwamba niko tayari kufanya hivyo kama ushahidi huo ni kweli anao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili ametoa tuhuma nzito kwa Jeshi letu la Polisi kwamba linashirikiana na vyama sijui chama gani. Mimi nimuhakikishie Mheshimiwa Maftaha na Waheshimiwa Wabunge na wananchi kwa ujumla kwamba tunavyotambua na ilivyo kabisa, si tunavyotambua, na uhalisia ulivyo, Jeshi letu la Polisi kwa kiwango kikubwa wanajitahidi kufanya kazi zake kwa kufuata weledi, sheria na maadili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kwa kuwa yeye Mheshimiwa Maftaha ambaye mimi ninamheshimu sana kama ni miongoni mwa viongozi wasio wengi sana makini wa upinzani anaweza kusema ana ushahidi wa jambo kama hilo wa tuhuma hizo nzito; imani yangu ni kwamba nitakapokuwa nimeambatana naye kama alivyoomba katika swali lake la msingi basi atatupatia ushahidi huo ili tuweze kuchukua hatua. (Makofi)