Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Primary Question

MHE. LEAH J. KOMANYA aliuliza:- Moja ya mkakati wa EQUIP – Tanzania ni kuinua ubora wa elimu inayotolewa kwa watoto wa kike ili waweze kuhitimu Shule ya Msingi na kuendelea na Sekondari, lakini mtoto wa kike ana vikwazo vinavyoweza kukatiza ndoto hii:- (a) Je, mpango huu umejikita vipi katika kutokomeza mimba na ndoto za utotoni, udhalilishaji kingono, ukeketaji na masuala ya adhabu zenye kudhuru mwili na akili za watoto? (b) Je, ni upi usaidizi wa mpango wa wanafunzi walio katika hatari zaidi kwa makundi kama vile waliotelekezwa, walio katika umasikini wa kupindukia, yatima na walionusurika kutokana na unyanyasaji?

Supplementary Question 1

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri sana ya Serikali. Nina maswali mawili madogo ya nyongeza. Kwa kuwa fedha za mafunzo zimekuwa zikibaki kila mwaka kutokana na wawezeshaji kutoka Vyuo vikuu Vya Tanzania; fedha hizo zimekuwa zikibaki kwa sababu wakati wa kutekeleza, wawezeshaji kutoka Vyuo Vikuu wamekuwa na programu nyingine katika vyuo vyao. Je, Serikali haioni ipo haja ya kutengeneza TOT wa Mkoa ili hata kama mradi utakapokwisha wanafunzi waendelee kupewa mafunzo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali ya mimba katika Mkoa wa Simiyu bado ni kubwa. Kwa mwaka 2017 wanafunzi 37 wa Shule za Msingi walipata ujauzito; 2018 wanafunzi 38; halikadhalika katika Sekondari kwa mwaka 2017 wanafunzi 159 walipata ujauzito; na mwaka 2018 wanafunzi 153.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa uchungu huo mkubwa wananchi waliamua kuanzisha ujenzi wa bweni katika Shule ya Sekondari ya Kata ya Mwanjoro: Je, Serikali ipo tayari kuunga nguvu za wananchi waliofikisha jengo usawa wa boma? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru? (Makofi)

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA):
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nimpongeze Mheshimiwa Leah Komanya kwa kuendelea kutaka watoto wa kike wapate elimu nzuri na juhudi hizi za kuunga mkono Serikali ambazo imeziweka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza anasema kuna fedha zinabaki kwenye programu hii. Ni kweli katika mazingira mbalimbali fedha inaweza kubaki, lakini maelekezo ya Serikali ni kwamba fedha ikibaki, wahusika wanapewa taarifa kwenye Wizara na inapangiwa majukumu mengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mawazo Mheshimiwa Mbunge aliyotoa ni mazuri, tuyapokee; kuandaa TOT ili programu itakapoisha wawezeshwe watu wa eneo husika kwani itapunguza gharama, wenyewe kwa wenyewe watafundishana kwa lugha zao za nyumbani, hii kazi itaenda vizuri. Kwa hiyo, tunapokea wazo hili, tunalifanyia kazi. Ni wazo jema sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, anazungumza habari ya mimba na kuunga mkono juhudi za kujenga mabweni. Utakumbuka tangu juzi mpaka jana kumekuwa na mjadala katika Bunge hili Tukufu la kumalizia maboma ya madarasa lakini pia na mabweni na Vituo vya Afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme tu kwamba kazi hii inatekelezwa na Serikali inaunga mkono juhudi za wananchi, tunafanya mpango, tukipata fedha tutaweka nguvu katika maeneo hayo. Mkoa wa Simiyu ni miongoni mwa mikoa ambayo imepewa miradi mingi ya kuwezesha watoto wa kike wasome, kujenga madarasa, matundu ya vyoo na mabweni. Jambo hili tunalifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba katika programu ijayo, fedha ikipatikana tutatoka hapa kuunga mkono nguvu za wananchi katika kumalizia mabweni ambayo wananchi wamechangia wenyewe.

Name

Joseph Roman Selasini

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Rombo

Primary Question

MHE. LEAH J. KOMANYA aliuliza:- Moja ya mkakati wa EQUIP – Tanzania ni kuinua ubora wa elimu inayotolewa kwa watoto wa kike ili waweze kuhitimu Shule ya Msingi na kuendelea na Sekondari, lakini mtoto wa kike ana vikwazo vinavyoweza kukatiza ndoto hii:- (a) Je, mpango huu umejikita vipi katika kutokomeza mimba na ndoto za utotoni, udhalilishaji kingono, ukeketaji na masuala ya adhabu zenye kudhuru mwili na akili za watoto? (b) Je, ni upi usaidizi wa mpango wa wanafunzi walio katika hatari zaidi kwa makundi kama vile waliotelekezwa, walio katika umasikini wa kupindukia, yatima na walionusurika kutokana na unyanyasaji?

Supplementary Question 2

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Mimba za watoto mashuleni ni jambo la aibu kweli kweli; nasi kama wazazi lazima tulichukulie very serious.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama tulivyoanza programu ya kujenga madarasa ya Shule za Kata, tukajenga mabweni, ni kwa nini Serikali isiagize Halmashauri kwa makusudi kabisa kwamba ni lazima katika Halmashauri bajeti itengwe ili mabweni yajengwe, lisiwe ni suala la hiari? Kwa sababu hawa watoto wanapata mimba kutokana na bodaboda, kutokana na njaa, watoto wamechoka kwa sababu ya umbali wa shule; kwa nini Serikali isiamue kabisa kwamba mwaka huu wa fedha kila Halmashauri ihakikishe angalau wamejenga mabweni mawili au matatu? (Makofi)

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Ni kweli kwamba jambo la kujenga mabweni na hasa ya watoto wa kike ni jambo ambalo haliepukiki, ni jambo la lazima na naomba pia tulizingatie. Ndiyo maana kwenye miradi mbalimbali ya Serikali, kwa mfano mradi wa EP4R tumeshajenga mabweni 533 katika shule zote za Sekondari katika maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa sababu hoja ni kwamba tutenge fedha kwenye bajeti hii, Mheshimiwa Mbunge ni Mbunge; na Waheshimiwa Wabunge wote nawaomba sana, wakati huu ndiyo tunaandaa bajeti zetu za Halmashauri. Kila Halmashauri ina maelekezo mahususi ya Serikali, asilimia 40 au 60 kulingana na mapato ya Halmashauri inaenda kwenye shughuli za maendeleo na hasa miundombinu ikiwepo mabweni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Mbunge kwenye bajeti ambazo zinaandaliwa sasa, hiki kipengele tumetoa maelekezo, Serikali ngazi ya juu ya Taifa tunapanga fedha, Halmashauri zitenge fedha. Wakuu wa Mikoa wameelekezwa, tunapozungumza maboma ni pamoja na madarasa na mabweni haya. Nasi tunapanga, Waheshimiwa Wabunge mtusaidie, tunalisimamia hilo. Kwenye ziara zangu zote, katika maeneo mbalimbali tunazingatia kukagua hosteli ambazo zinajengwa na wananchi, wadau mbalimbali na Serikali Kuu.