Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Abdulaziz Mohamed Abood

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Mjini

Primary Question

MHE. ABDUL-AZIZ M. ABOOD aliuliza:- Kuna mgogoro wa ardhi kati ya Jeshi la Wananchi kwenye mipaka katika Kata ya Kauzeni na Luhongo ambapo wananchi wanashindwa kufanya shughuli zao za maendeleo hasa kilimo, Jeshi linaweka mipaka na kuingiza ndani ya mashamba ya wananchi wakati miaka yote maeneo hayo yalikuwa nje ya mipaka ya Jeshi:- • Je, ni lini Serikali itawarudishia wananchi maeneo yao ya kilimo? • Je, kwa nini Serikali isichukue hatua kwa kuruhusu wananchi wamiliki maeneo hayo ambayo ni ya asili na Jeshi limewakuta wananchi katika eneo hilo?

Supplementary Question 1

MHE. ABDUL-AZIZ M. ABOOD: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, kwa kuwa, wananchi wa Kauzeni na Luhungo walihamia pale mwaka 1969 wakati wa Vijiji vya Ujamaa na wakapewa maeneo ambayo yalipimwa mwaka 1970 ikawekwa mipaka kati ya shirika na wananchi;
Je, kwa nini Serikali isitumie mipaka hiyo ya mwaka 1970 ili wananchi wakapata haki yao na mashamba yao yakawa katika eneo lao?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, si swali lakini ningemwomba Mheshimiwa Waziri angekuja katika maeneo haya akaangalia yeye mwenyewe na kuweza kukutana na wananchi akapata ukweli ulivyo katika meneo haya. (Makofi)

Name

Dr. Hussein Ali Mwinyi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kwahani

Answer

WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA:
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba upimaji wa awali umefanyika mwaka 1970 na baada ya pale kutokana na migogoro hii ya kuingiliana kati ya maeneo ya Jeshi na Wananchi, mwaka 2002 ulifanyika upimaji mpya ambao ulikuwa na lengo la kuondoa wananchi waliokuwa ndani ya mipaka ya Jeshi kwa hivyo wakaachwa nje, sasa inaonekana baada ya pale mgogoro umeendelea. Nataka nimkubalie na nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba niko tayari kwenda katika eneo hilo pamoja na wataalam wangu ili tukazungumze na wananchi na kutafuta ufumbuzi wa kudumu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee tu kusema kwa ufupi kwamba, matatizo ya mipaka kati ya maeneo ya Jeshi na wananchi yako sehemu nyingi sana. Naomba niwaarifu tu Waheshimiwa Wabunge kwamba nimetengeneza utaratibu maalum wa kupita katika maeneo hayo ili mimi na wataalam wangu tuthibitishe mipaka hiyo na kuhakikisha kwamba tunaondoa hii mogogoro ambayo imeendelea kwa siku nyingi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu hapa kwamba kuna mgogoro ambao nimeupata kutoka kwa Mheshimiwa Mwakyembe kwenye Kata za Bondeni, Ipiyana na Kajunjumele katika Wilaya ya Kyela, nimhakikishie pia kwamba katika utaratibu nitakaopanga wa kuzunguka katika maeneo haya nitafika na pale nizungumze na wananchi ili hatimaye tuondoe matatizo yanayowakabili wananchi katika maeneo hayo. (Makofi)