Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Zaynab Matitu Vulu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ZAYNAB M. VULLU (K.n.y. MHE. MAULID S. MTULIA) aliuliza:- Serikali inafanya juhudi kubwa ya kuzuia biashara ya ukahaba kwa kuwakamata wauzaji na wanunuzi na kuwafikisha mbele ya vyombo vya sheria. Pamoja na jitihada hizo bado biashara hiyo haramu inaendelea kwa kasi ileile:- Je, Serikali ina mpango gani mbadala wa kuzuia biashara hii haramu?

Supplementary Question 1

MHE. ZAYNAB M. VULLU: Mheshimiwa Mwenyekiti, asante sana. Kwa kuwa, biashara mara nyingi ni muuzaji na mnunuaji; na kwa kuwa, biashara ya ukahaba mara nyingi inaita machangudoa; na kwa kuwa, katika bahari kuna changudoa, kuna changuchole, kuna changufatundu. Je, Serikali haioni kuna haja sasa ya hawa machangu wengine wakakamatwa na wakapewa elimu ya kutosha, waachane na vitendo vya ukahaba kwa sababu, wao kama hawakwenda sokoni, hii biashara haitakuwepo. Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kuhakikisha wasichana wote wanawawezesha kwa mikopo na elimu ya ujasiriamali, pamoja na juhudi alizozisema Mheshimiwa Naibu Waziri? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, pamoja na juhudi za Serikali, Taasisi Zisizo za Kiserikali, na baadhi ya raia kumekuwa na mkusanyiko mkubwa wa biashara hii maeneo mbalimbali, ikiwemo eneo maarufu kwa Uwanja wa Fisi, Mburahati, Dar-es-Salaam na biashara hii inafanyika katikati ya maeneo wanayoishi wananchi. Je, Serikali haioni sasa kuna haja ya kwenda katika maeneo hayo kwa kushirikiana na wadau mbalimbali kuvunja hayo maeneo, kujenga miundombinu ambayo itawawezesha wasichana waliojiingiza katika biashara hizo kwa kutokutarajia kutokana na hali ngumu ya maisha na pia wataepukana na maradhi ya UKIMWI; Serikali ikiweza kujenga hiyo miundombinu na kuwapa mikopo hawa wasichana haioni kwamba, tutakuwa tumekwamua Taifa ambalo tunalitegemea? (Makofi)

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza swali lake na concern yake Mheshimiwa Mbunge kuhusiana na janga hili. Naungana mkono na yeye kabisa kuhusiana na umuhimu wa kushughulika sio tu na wauzaji, lakini wanunuzi, lakini si tu na wanunuzi, mpaka na mazingira ambayo wale wanayaweka. Maana kuna wengine sio wanaouza, kwa mfano wenye madanguro, ni watu ambao sio wauzaji na sio wanunuzi, lakini wanahamasisha hivi vitendo. Kwa hiyo, yote hayo na wote ambao wanashiriki kwa namna moja ama nyingine katika hii biashara kuna haja ya kuhakikisha kwamba, tunachukua hatua na ndivyo ambavyo Serikali inafanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kumekuwa na changamoto mbalimbali ambazo nadhani Bunge hili ni wakati muafaka wa kuzitafakari. Moja ni changamoto ya sheria; labda nitoe mfano wa sheria ambazo pengine zinakwaza mapambano dhidi ya vita ya makahaba. Ukiangalia kwenye Kanuni ya Adhabu Namba 176(a), Sura ya 16, adhabu ambayo inatakiwa itolewe kwa watu ambao wanafanya biashara ya madanguro wanasema ni fine isiyozidi 500/= ama iwapo ni kosa la mara ya pili na kuendelea atatozwa fine isiyozidi 1,000/=.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mtaona kwamba, adhabu kama hii inaweza kuwa inahamasisha utendaji wa huu uhalifu. Kwa hiyo, kuna haja ya Mheshimiwa Mbunge na Bunge lako Tukufu kuangalia na kutafakari juu ya sheria hizi ambazo zimepitwa na wakati ili hatimaye kazi kubwa ambayo inafanywa ya kuwakamata hawa makahaba kila siku, pamoja na wahamasishi wanaoshiriki na wanunuzi iweze kuwa na tija kwani mara nyingi wanapokamatwa wanarudia tena makosa kwa sababu, ya wepesi wa sheria zilizopo. Kwa hiyo, kimsingi hilo ni jibu la swali lake la kwanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuhusiana na elimu; nimhakikishie kwamba, tunaendelea kutoa elimu, lakini vilevile na mamlaka nyingine kama ambavyo nimezungumza katika swali la msingi kwamba, kwa sababu, suala hili ni mtambuka tumekuwa tunashirikiana kama Serikali na mamlaka nyingine na taasisi mbalimbali, ili kuweza kutoa elimu kwa jamii juu ya madhara haya, ikiwemo kuwashirikisha vilevile viongozi wa dini ambapo nilizungumza kwamba, viongozi wa dini ni sehemu muhimu sana katika kutoa elimu ya maadili juu ya wananchi.