Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Lucia Ursula Michael Mlowe

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. LUCIA M. MLOWE aliuliza:- Mfumo wa mabomba ya maji kwenye maeneo mengi nchini ni chakavu hivyo kusababisha upotevu mkubwa wa maji:- Je, Serikali ina mpango gani wa kubadilisha mabomba yote chakavu katika nchi ili kuokoa maji yanayopotea kutokana na uchakavu huo?

Supplementary Question 1

MHE. LUCIA M. MLOWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali ya nyongeza, nina maswali mawili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, Waziri amekiri kwamba kuna tatizo la upotevu wa maji kutokana na miundombinu mibovu. Hivi navyoongea bado kuna tatizo kubwa sana la uvujaji wa maji, mfano, Kisasa kuna mabomba hivi sasa yanaendelea kutiririsha maji lakini sioni juhudi inayoendelea hadi sasa hivi. Je, wana mkakati gani kuhakikisha tatizo hili linatatuliwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, katika Jimbo la Njombe Kusini, Kata ya Ihungilo kuna mradi wa Utengule – Ngalanga ambao vifaa vilivyonunuliwa vilinunuliwa chini ya kiwango na hadi sasa hivi vifaa hivi, mabomba na viungio vyake vinaendelea kutitirisha maji na wananchi wanakosa huduma ya maji. Je, Waziri yuko tayari kwenda kutatua tatizo hili katika Kata hii ya Ihungilo?

Name

Eng. Isack Aloyce Kamwelwe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Katavi

Answer

WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Mlowe, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, upotevu wa maji ni changamoto kubwa kwa sababu lina sehemu mbili, kwanza ni miundombinu yenyewe na pili ni wafanyakazi tunasema non commercial revenue water losses ambalo linatokana na baadhi ya wafanyakazi kushirikiana na wananchi katika kuiba maji. Tunapamba na mambo yote haya mawili na kuhakikisha kwamba tatizo la upotevu wa maji linamalizika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Mheshimiwa Mbunge alivyosema sasa hivi kuna changamoto hizo lazima mtu akiona changamoto hiyo tuwasiliane na Mamlaka za Maji, tuwape taarifa ili waweze kwenda kumaliza tatizo hilo. Kila kwenye Mamlaka ya Maji tumeweka toll free number ambayo ni namba ya simu ambapo unaweza kupiga simu bure kueleza wapi kuna tatizo la upotevu wa maji na mara moja utakapofanya hivyo sisi tutachukua hatua za kuweza kupambana na upotevu huo wa maji. Hili la Kisasa kama alivyosema Mheshimiwa naamini wataalam wangu wamesikia na watakwenda kulishughulikia mara moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ni kuhusu vifaa vilivyo chini ya kiwango. Ni kweli kabisa katika miradi mingi sana iliyojengwa vijijini, vifaa vingi vilivyopelekwa na wakandarasi viko chini ya kiwango na tumechukua hatua mbalimbali za kisheria na tutaendelea kuchukua. Naomba tu nikubaliane na Mheshimiwa Mbunge kwamba tutakwenda pamoja tuhakikishe kwamba tatizo hili tunaliondoa ili wananchi wale waweze kupata maji safi na salama.

Name

Willy Qulwi Qambalo

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Karatu

Primary Question

MHE. LUCIA M. MLOWE aliuliza:- Mfumo wa mabomba ya maji kwenye maeneo mengi nchini ni chakavu hivyo kusababisha upotevu mkubwa wa maji:- Je, Serikali ina mpango gani wa kubadilisha mabomba yote chakavu katika nchi ili kuokoa maji yanayopotea kutokana na uchakavu huo?

Supplementary Question 2

MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Miradi ya maji katika Vijiji vya Getamok, Endonyawed, Kansai, Matala na Fusmai katika Wilaya ya Karatu ambayo ni zaidi ya asilimia 50 ya ile miradi kumi katika kila Wilaya haifanyi kazi kwa sababu ya kujengwa chini ya kiwango. Tatizo kubwa ni kama ilivyoelezwa katika swali la msingi mabomba yanavuja. Mheshimiwa Waziri yuko tayari sasa kuja Karatu ili ajionee mwenyewe jinsi wananchi na Serikali walivyohujumiwa lakini pia akae na Halmashauri ili kuona ni namna gani miradi hiyo inafufuliwa? Ahsante.

Name

Eng. Isack Aloyce Kamwelwe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Katavi

Answer

WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mbunge, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa kama nilivyosema maeneo mengi hasa ya vijijini miradi mingi iliyotekelezwa ilitekelezwa chini ya viwango. Wameweka mabomba ambayo yako chini ya viwango, wameweka valve ambazo ziko chini ya viwango. Sisi tunahakikisha kwamba sasa tatizo hili linamalizika na pale ambapo mkandarasi ameweka vifaa ambavyo viko chini ya viwango anatakiwa aviondoe na afanye kazi hiyo na aweke vifaa ambavyo vina viwango vinavyokubalika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekubaliana na Mheshimiwa Mbunge tutakwenda tutaona tatizo hilo na tutalitatua kwani nia ya Serikali naendelea kusema tena ni kuhakikisha kwamba tunawapelekea wananchi maji safi na salama.

Name

Deogratias Francis Ngalawa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ludewa

Primary Question

MHE. LUCIA M. MLOWE aliuliza:- Mfumo wa mabomba ya maji kwenye maeneo mengi nchini ni chakavu hivyo kusababisha upotevu mkubwa wa maji:- Je, Serikali ina mpango gani wa kubadilisha mabomba yote chakavu katika nchi ili kuokoa maji yanayopotea kutokana na uchakavu huo?

Supplementary Question 3

MHE. DEOGRATIAS F. NGALAWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Wananchi wa Jimbo la Ludewa huwa wana kawaida ya kujiongeza. Miradi mingi ambayo inafanyika kwenye Jimbo la Ludewa wananchi wanakuwa wameianza kabla ya Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni shahidi alipofika maeneo ya Mlangali alishakuta watu wameshajichangisha shilingi milioni 90 na wakawa wanaiomba Serikali shilingi milioni 50 kwa ajili ya kumalizia. Niishukuru Serikali ilitupa ile hela. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna miradi mbalimbali inaendelea kwenye Kata ya Mavanga na Ludewa Mjini. Je, Serikali ipo tayari kutusaidia na kuhakikisha mfano miradi ile ya Ludewa Mjini, Iwela na Lifua inakamilika katika kipindi kifupi iwezekanavyo? (Makofi)

Name

Eng. Isack Aloyce Kamwelwe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Katavi

Answer

WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Ludewa, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kawaida nia ya Serikali ni kuhakikisha kwamba Watanzania wanapata huduma ya maji safi na salama na kwa muda mfupi. Kwa hivyo, nitahakikisha kwamba miradi ya Ludewa Mjini na maeneo mengine aliyoyataja Mheshimiwa Mbunge tutatekeleza kwa muda mfupi ili Watanzania wa maeneo yale na maeneo mengine yote Tanzania waweze kupata maji safi na salama. (Makofi)

Name

Ruth Hiyob Mollel

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. LUCIA M. MLOWE aliuliza:- Mfumo wa mabomba ya maji kwenye maeneo mengi nchini ni chakavu hivyo kusababisha upotevu mkubwa wa maji:- Je, Serikali ina mpango gani wa kubadilisha mabomba yote chakavu katika nchi ili kuokoa maji yanayopotea kutokana na uchakavu huo?

Supplementary Question 4

MHE. RUTH H. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ni miaka zaidi ya 50 ya Uhuru lakini maeneo mengi ya wafugaji bado wanakunywa maji kwenye mabwawa pamoja na wanyama, binadamu wanachota maji, wanyama pia wanakunywa hapo. Nimeona hili Mkuranga Kijiji cha Beta, nimeona hili juzi Monduli katika Kata ya Nararami. Kwa nini hii shilingi milioni 50 iliyotolewa kwa kila kijiji isitumike kwenda kuchimba visima virefu katika yale maeneo ambayo hakuna maji na binadamu wanakunywa maji kwenye mabwawa na wanyama? (Makofi)

Name

Eng. Isack Aloyce Kamwelwe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Katavi

Answer

WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ruth, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaelewa kwamba maeneo mengi ya nchi yetu yana changamoto kubwa ya maji, mijini na vijijini. Serikali tumejipanga vizuri, kwa mfano tu, juzi tumepata mkopo wa bei nafuu kutoka Benki ya Dunia ambapo tumepata takribani shilingi za Kitanzania bilioni 800 na pesa nyingi kati ya hizo zitapelekwa vijijini kutatua changamoto ya maji kama Mheshimiwa Mbunge alivyosema. Siyo hivyo tu, kwenye bajeti yetu hii ya mwaka huu tuna takribani shilingi bilioni 630 kwa ajili ya kupeleka maji vijijini. Nataka niwahakikishie Watanzania kwamba Serikali tumejipanga na kila kijiji tutawapelekea maji safi na salama.