Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Faida Mohammed Bakar

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. FAIDA MOHAMMED BAKARI aliuliza:- Kiswahili ndiyo lugha ya Taifa letu na kinapaswa kutumika katika nyanja zote ili kukipa hadhi yake:- Je, kwa nini baadhi ya Mahakama nchini zinatumia lugha ya Kiingereza wakati zinapoendesha mijadala yake na katika kutoa hukumu?

Supplementary Question 1

MHE. FAIDA MOHAMMED BAKARI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri niko na maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa hizi sheria naona kama zitakuwa zimepitwa na wakati; na kwa kuwa Mheshimiwa Rais wetu amekuwa mfano mzuri wa kuhamasisha utumiaji wa lugha ya Kiswahili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu ni je, Mheshimiwa Waziri atakubaliana nami kwamba sasa umefika wakati muafaka wa kumuunga mkono Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa matumizi ya Kiswahili katika Mahakama, katika kuandika maamuzi yake kwa lugha hii ya Kiswahili?
Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa hata hapa Bungeni unaletewa hii Miswada hii unaiona hii kwa lugha ya Kiingereza, hii ni Tanzania tunaletewa Miswada kwa lugha ya Kiingereza na humu Bungeni kuna watu tofauti na elimu zetu tofauti, watu wanaweza wakajadili wakawa hawapati muafaka mzuri kwa sababu hawaelewi hii lugha iliyomo katika Miswaada mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, je, Mheshimiwa Naibu Waziri atakubaliana nami sasa kwamba ni wakati muafaka katika nchi yetu ya Tanzania tutumie lugha yetu ya Kiswahili, Lugha ya Taifa katika Mahakama na katika Mabunge na katika sehemu zote? Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. (Makofi)

Name

Dr. Adelardus Lubango Kilangi

Sex

Male

Party

Ex-Officio

Constituent

None

Answer

MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie katika majibu ambayo Mheshimiwa Naibu Waziri ameshayatoa. Kuhusiana na lile suala la kwanza la kuendesha mashitaka kwa Kiswahili halafu hukumu zinatolewa kwa lugha ya Kiingereza ametoa maelezo ya kutosha na nafasi ipo kwamba kama mashtaka yanaendeshwa Hakimu au Jaji anaweza kuruhusu yaendelee kwa Kiswahili au kwa Kiingereza; na sababu nadhani amezitoa za kutosha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kuhusu Miswada na pengine sheria kuandikwa kwa lugha ya Kiswahili hilo lipo katika mpango wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kuanza na kutafsiri karibu sheria zote ziwe na zisomeke kwa lugha ya Kiswahili kwa sababu ndiyo lugha inayozungumzwa na kueleweka na watu wote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, suala hili linahitaji rasilimali na tuna changamoto kidogo za rasilimali lakini pia hata utaalam wa kutosha kwa sababu kuna hatari, sheria ina lugha yake unapoitafsiri tu moja kwa moja kwenda Kiswahili kuna hatari kubwa pia ya kupoteza mantiki iliyokusudiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tuna changamoto pia ya kuwa na wataalam wanaoweza kutufanyia kazi hii kwa usahihi. Hata hivyo, hilo ni kati ya mambo ambayo tumeyawekea mipango tuanze kuyafanyia kazi sheria zote ziandikwe kwa Kiswahili. Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.