Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Edwin Mgante Sannda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kondoa Mjini

Primary Question

MHE. EDWIN M. SANNDA aliuliza:- Je, ni lini Serikali itatekeleza Sera ya Elimu Bure kwa kidato cha tano na sita ambalo ndilo kundi pekee lililobaki kugharamiwa na Serikali?

Supplementary Question 1

MHE. EDWIN M. SANNDA: Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, napenda kuuliza maswali mawili ya nyongeza; kama alivyoeleza Naibu Waziri mpaka sekondari elimu bure, lakini pia ukienda Chuo Kikuu kwa elimu ya juu tunayo mikopo ya wanafunzi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kundi lililobaki ni kidato cha tano na cha sita. Kwa kuwa changamoto ya uwezo wa kugharamia elimu iko pia kwa wananchi hasa ambao nao wanakwenda kidato cha tano na cha sita ambapo imepelekea baadhi yetu nikiwemo mimi kuweka mpango mahsusi kwenye Majimbo yetu ya kuwalipia wanafunzi wanaofaulu kwenda kidato cha tano na cha sita; pamoja na changamoto ya uwezo wa Serikali; je, Serikali sasa haioni umuhimu wa kulijumuisha kundi hili la kidato cha tano na cha sita kwenye Mpango wa Elimu Bure? Hilo ni swali la kwanza. (Makofi)
Swali la pili. Ili mpango wowote ufanikiwe, ni lazima kuwe na lengo na dhamira ya dhati ya kuhakikisha jambo hili linafanikiwa na kuwekewa mikakati. Kama tunavyozungumzia kwenye upande wa maji, tunasema mpaka 2020/2021 tuwe tumefikia asilimia 85 ya Watanzania wawe wanapata maji safi na salama; je, Serikali haioni umuhimu sasa kuweka muda mahususi kwa maana ya time frame na malengo lini tutaanza kutoa elimu bure kwa kidato cha tano na cha sita kama ilivyo kwenye maeneo mengine? (Makofi)

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijaingia kwenye maswali, naomba nikiri kwamba Mheshimiwa Sannda ni mmoja kati ya Wabunge wanaofuatilia sana masuala ya elimu. Pale Wizarani amezoeleka sana kiasi kwamba haulizwi tena kwamba anataka kuonana na nani? Kila siku utamkuta yupo mlangoni.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu kama Serikali ina nia ya kuhakikisha kwamba hata kidato cha tano na sita nao wanapata mpango ule wa elimu bure, kwa sasa Serikali imeweka nguvu nyingi katika kukabiliana na changamoto ambazo zimejitokeza baada ya elimu bila malipo kuanza kutekelezwa, lakini baadae kadri fedha na uwezo utakapoimarika tutafikiria hata kwa elimu ya kidato cha tano na sita.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwamba kwa nini angalau tusiweke basi mpango wa muda mrefu; nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba pamoja na kwamba haionekani kwenye mipango yetu kuhusu muda, lakini nia yetu kama Serikali ni kuhakikisha kwamba kadri uwezo unavyoongezeka kuendelea kutoa changamoto zinazowakabili wananchi kwenye Sekta ya Elimu na ikiwezekana huko mbele kadri uchumi wetu utakapoimarika kama nchi, hakuna shida hata mpaka Chuo Kikuu inaweza ikawa elimu bure kama ilivyo kwenye baadhi ya mataifa ya Ulaya.