Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Taska Restituta Mbogo

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. TASKA R. MBOGO aliuliza:- Mkoa wa Katavi hauna umeme wa Gridi ya Taifa. Je, ni lini Mkoa huo utapatiwa umeme wa Gridi ya Taifa?

Supplementary Question 1

MHE. TASKA R. MBOGO: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, ninaomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa umeme wa gridi mpaka kufika Mkoa wa Katavi utachukua muda mrefu; na kwa kuwa umeme hautoshi Mkoani Katavi, lakini pia napenda kuishukuru Serikali kwa kushirikiana na Serikali ya Uholanzi kwa ujenzi wa jenereta mbili na jenereta hizo zimeanza kufanya kazi kutoka tarehe 27 Mei, 2017 , lakini jenereta hizo hazitoshi.
Mheshimiwa Spika, umeme unaotakiwa Mkoa wa Katavi ni megawati tano, jenereta zinazalisha megawati 2.2. Je, Serikali haioni umuhimu wa kuongeza jenereta nyingine mbili kwa Mkoa wa Katavi? Kwa sababu mahali pa kuzifunga jenereta hizo tayaripameshajengwa, maana eneo la hizo jenereta limejengwa sehemu za kufunga jenereta nne, lakini Serikali pamoja na Serikali ya Uholanzi imefunga jenereta mbili, eneo hilo lipo. (Makofi)
Meshimiwa Spika, je, Serikali haioni umuhimu wa kuongeza jenereta mbili?
Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; kwa kuwa jenereta hizi zinatumia mafuta ya dizeli na ni gharama zaidi, je, Serikali haioni kwamba matumizi ya jenereta kwa Mkoa wa Katavi ni gharama zaidi kuliko kufunga umeme wa gridi? Naomba kuwasilisha. (Makofi)

Name

Eng. Isack Aloyce Kamwelwe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Katavi

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI (K.n.y. WAZIRI WA NISHATI NA MADINI): Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa, maswali yake ni mazuri na kwa faida ya Mkoa wa Katavi ambao na mimi mwenyewe natoka kule siwezi kuahidi lakini niseme kwamba nitalifikisha hili ili waweze kuongeza jenereta nyingine mpya kuongeza umeme. Lakini pia haya masuala ni ya kiuchumi. Ipo historia kwamba matumizi ya umeme katika mkoa wetu, hasa katika masuala ya viwanda bado hatujawa na viwanda vingi, kwa hiyo umeme sehemu kubwa unatumika majumbani tu na taarifa iliyopo ni kwamba TANESCO imekuwa inatoa gharama kubwa zaidi kuliko makusanyo yanayofanywa kutokana na matumizi ya umeme, lakini suala hili tutalifikisha.
Mheshimiwa Spika, kuhusu swali la pili linalozungumzia dizeli. Ni kweli kabisa kwamba kutumia dizeli ni gharama kubwa kabisa na ndiyo maana sasa hivi Serikali nzima inataka kwenda kwa kutumia umeme ama wa gesi au wa maji, na ndiyo maana sasa Serikali imeshalitambua hili, inaleta umeme wa msongo mkubwa ambao sehemu kubwa utatumia uzalishaji kwa kutumia maji badala ya kutumia dizeli. Kwa hiyo, mawazo yako Mheshimiwa Mbunge ni mazuri na tayari Serikali imeshaanza kuyatekeleza.

Name

John John Mnyika

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Kibamba

Primary Question

MHE. TASKA R. MBOGO aliuliza:- Mkoa wa Katavi hauna umeme wa Gridi ya Taifa. Je, ni lini Mkoa huo utapatiwa umeme wa Gridi ya Taifa?

Supplementary Question 2

MHE. JOHN J. MNYIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
Mheshimiwa Spika, tatizo la umeme wa Gridi ya Taifa kutokufika kwa wananchi haliko tu Mkoa wa Katavi, bali pia liko katika Jimbo la Kibamba, Jijini Dar es Salaam ambapo kwenye Kata ya Mbezi maeneo kama ya Msumi kwa Londa hayana kabisa miundombinu ya umeme. Kata ya Goba kuna mitaa ambayo haina umeme, Kata ya Msigani kuna mitaa ambayo haina umeme, Kata ya Kwembe kuna mitaa haina umeme, Kata ya Saranga kuna mitaa haina umeme na Kata ya Kibamba kuna mitaa haina umeme.
Sasa kwa kuwa TANESCO iko jirani kabisa na Jimbo la Kibamba, je, Serikali iko tayari baada ya Mkutano huu wa Bunge kufanya ziara maalum kwenye kata hizi zote sita kwenda kuwaeleza wananchi ni lini hasa maeneo haya yatapata umeme?

Name

Eng. Isack Aloyce Kamwelwe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Katavi

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI (K.n.y. WAZIRI WA NISHATI NA MADINI): Mheshimiwa Spika, niseme kwanza Serikali iko tayari ndiyo maana imeanzisha REA III, na tayari maeneo mengi miradi imezinduliwa kuhakikisha kwamba vijiji vyote tulivyonavyo katika Tanzania vinapata umeme. Kwa hiyo, tayari imeshaanza, lakini niseme Mheshimiwa Mbunge mimi na wewe ni Madiwani tuna uwakilishi ndani ya Bunge.
Mheshimiwa Spika, ni kazi yetu sasa kwamba wewe kwasababu ni Mbunge uko ndani ya Bunge na matamshi haya ya Serikali umeyasikia, urudi kwenye Jimbo lako ukawaambie kuwa “jamani sasa Awamu ya Tatu ya REA inafika na kwetu tunapatiwa vijiji moja, mbili, tatu” na vijiji vyako vimeainishwa kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, kwa hiyo uende ukatoe taarifa.