Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Mwanne Ismail Mchemba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Tabora Mjini

Primary Question

MHE. MWANNE I. MCHEMBA aliuliza:- Hali ya nyumba za Polisi na Magereza nchini ni mbovu sana. Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga nyumba za askari hao?

Supplementary Question 1

MHE. MWANNE I. MCHEMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niulize maswali madogo ya nyongeza kama ifuatavyo:-
Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, pamoja na jitihada zote zinazofanywa na Serikali kutatua tatizo la makazi ya askari. Je, kwa kipindi hiki cha 2017/2018 Mkoa wa Tabora umetengewa kiasi gani?
Swali la pili, kwa kuwa hivi karibuni kumekuwa na wimbi kubwa la wakimbizi kutoka Congo na kwa kuwa hivi karibuni pia wamesema kwamba baadhi ya wakimbizi wale wametawanyika katika Mkoa wa Kigoma inawezekana wakaja na Mkoa wa Tabora. Je, Serikali inatoa kauli gani kwa sasa?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI:
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nichukue fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Mwanne Mchemba kwa swali lake zuri la pili la nyongeza kutokana na changamoto ya mfumuko wa Wakimbizi ambao wanaingia nchini kutoka DRC hasa kutoka katika maeneo ya Kivu kutokana na changamoto ya hali ya usalama nchini DRC. Kabla sijatoa ufafanuzi wa swali lake hilo la pili nimjibu kwamba kwa bajeti ambayo nimeizungumza ya maendeleo ambayo nilisema ni takribani bilioni 12.3 ya mchanganuo mbalimbali ikiwemo shilingi bilioni 7.2 ya Magereza ni fedha ambazo zimetengwa kwa maendeleo nchi nzima.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa Jeshi la Magereza hakuna utaratibu wa sub vote kwenye Jeshi hilo ingawa Jeshi la Polisi ipo lakini kwa ujumla kwa mwaka huu wa fedha hakuna fedha ambayo imetengwa kwa ajili ya mradi wa maendeleo kwa Tabora specifically, lakini kwa sababu tunatambua kwamba kuna maeneo mengi nchini ambayo kuna majengo mengi ya Polisi ambayo yapo katika hatua za mwisho kukamilika, kwa mfano, kule Mtambaswala
- Mtwara, Njombe, Mabatini Mwanza, Musoma na kadhalika, kwa hiyo fedha hii ya maendeleo mwaka huu tunataka tuilekeze katika majengo ambayo tayari yapo katika hatua za mwisho kukamilika kabla hatujaanza miradi mipya.
Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue fursa hii sasa kuweza kuzungumzia hoja yake ya pili muhimu ya wimbi la wakimbizi kutoka DRC. Mpaka hivi naomba nitoe taarifa rasmi kwamba Wakimbizi ambao wametoka DRC kuingia nchini tokea Januari wanakadiriwa kufika zaidi ya 2,500 na katika hao takribani wakimbizi 1,960 tayari wameshakuwa wamehifadhiwa katika Kambi ya Wakimbizi Nyarugusu na wengine 300 na zaidi wapo kwenye vituo vya kupokelea Wakimbizi. Changamoto ambayo amezungumza ya kwamba kuna baadhi ya wakimbizi ambao wamekuwa wana desturi aidha ya kutoroka kwenye makambi kutoka DRC na kuingia mitaani ama kupita njia za panya kuingia nchini kwetu kwa kisingizio cha machafuko DRC.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nitoe kauli ifuatayo, jambo la kwanza nataka nitoe angalizo ama onyo kali kwa wakimbizi kama hao kuacha desturi hiyo. Tumeshatoa maelekezo katika vyombo vyetu vya usalama nchini kuhakikisha jambo la kwanza kwa Idara ya Uhamiaji kuendelea kufanya msako kwa kushirikiana na vyombo vingine vya dola, ikiwemo Jeshi la Polisi hasa katika Mkoa wa Kigoma ambao una changamoto kubwa sana ya wakimbizi, hii inadhihira na takwimu ambavyo zipo kwa mwaka jana.
Mheshimiwa Naibu Spika, takribani asilimia 30 ya wahamiaji haramu waliokuja Tanzania wametokea katika Mkoa wa Kigoma. Kwa hiyo, tumewekeza nguvu nyingi sana katika Mkoa wa Kigoma kuhakikisha kwamba inadhibiti wimbi la wahamiaji haramu kuingia. Vilevile tumetoa maelekezo kwa Idara ya Wakimbizi ambayo ipo chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kuhakikisha kwamba inafanya uhakiki na kuimarisha ulinzi katika makambi yetu hasa Kambi ya Nyarugusu ambayo ndiyo kambi ambayo inapokea wakimbizi kutoka DRC ili kuhakikisha kwamba wale wote ambao watakiuka sheria na utaratibu wachukuliwe hatua kwa mujibu wa sheria ya wakimbizi kwa kushtakiwa ili baadaye sheria ichukue mkondo wake.
Mheshimiwa Naibu Spika, hiyo ndiyo kauli ya Serikali kuhusiana na swali lake la pili.